Kutumia Ile Broshua Mpya kwa Matokeo
1 Kwenye mkusanyiko wetu wa wilaya wa hivi karibuni, tulifurahia sana kupokea ile broshua mpya Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa. Yapaswa ivutie watu kutoka tabaka zote za maisha, kwa kuwa wengi wamehuzunika juu ya kifo cha mpendwa. Picha na vielezi vyayo vyenye kuvutia macho vyapaswa kuifanya iwe rahisi kuangusha. Kwenye ukurasa 29 ile picha iliyochorwa yenye kutazamisha ya Lazaro akifufuliwa kutoka kwa wafu yaonyesha ‘kutamani kwa Yesu sana kuondoa madhara ya kifo.’ Kielezi kinachofuatia cha ukurasa mzima chaonyesha mandhari yenye shangwe ya ufufuo katika ulimwengu mpya. Hilo lapaswa kuchangamsha kama nini mioyo ya wale wenye huzuni!
2 Broshua hii yaweza kuwa msaada mkubwa mno katika kufariji waliofiwa. Imekusudiwa kwa ajili ya mazungumzo ya kupata maoni. Maswali ya kukazia mambo makuu yanaonekana katika sanduku lililo mwishoni mwa kila sehemu badala ya kuwa chini ya kila ukurasa. Waweza kutumia hayo “Maswali ya Kufikiriwa Sana” kwa njia yoyote ile ambayo waona itamsaidia zaidi mwanafunzi wako.
3 Unapotembelea watu, uwe mteuzi katika kuzungumzia mambo yanayopatikana katika broshua. Huenda ukahisi kwamba ingefaa kuonyesha jedwali ya yaliyomo kwenye ukurasa 2 na kumuuliza mwenye nyumba aonyeshe jambo linalompendeza. Uwe mwepesi kuona mahitaji ya kila mtu mmoja-mmoja. Mwache aeleze hisia zake, kisha uonyeshe jinsi broshua hiyo inavyotoa faraja. Kila sehemu hutumia vya kutosha maandiko ya Biblia yanayoandaa msingi wa tumaini letu.
4 Kichwa kidogo kwenye ukurasa 5, “Kuna Tumaini Halisi,” chakazia lile tumaini la kufariji lenye msingi wa Biblia kwa wafu. Hilo lapaswa liamshe tamaa ya mazungumzo juu ya “Tumaini Hakika kwa Wafu,” yapatikanayo kwenye kurasa 26-31. Ukurasa 27 watoa “Maandiko Yanayofariji” ya ziada. Mwenye nyumba aliye na huzuni ataona upesi kwamba Yehova kwa kweli ni “Mungu wa faraja.”—2 Kor. 1:3-7.
5 Kwa njia ya kugusa hisia, sehemu za katikati hueleza maitikio tofauti-tofauti kwa kifo cha mpendwa. Zinaonyesha jinsi ya kukabiliana na huzuni na jinsi wengine wawezavyo kusaidia katika nyakati hizo zenye kusononesha. Kuna sanduku kwenye ukurasa 25 lenye kichwa “Kusaidia Watoto Washughulike na Kifo.” Hilo lapaswa kuwa msaada halisi kwa wazazi wanaohitaji kukabiliana na tatizo hili.
6 Uwe na nakala ya ziada, na uitumie kwa ushahidi wa vivi hivi. Huenda ukataka kutembelea majumba ya kuhifadhi maiti ya eneo la kwenu kuona kama wangependa kuwa na nakala kadhaa ili kufariji familia zilizofiwa. Au huenda ukakaribia kwa busara wale wenye huzuni walio kwenye makaburi katika zile pindi ambazo wanarudi kutembelea kaburi la mpendwa.
7 Twashangilia kwamba Yehova ni Mungu “mwenye kuwafariji wanyonge.” (2 Kor. 7:6) Twaliona kuwa pendeleo kushiriki katika ‘kuwafariji wale waliao.’—Isa. 61:2.