Wafariji Wale Wanaoomboleza
1. Kwa nini watu wanaoomboleza wanahitaji faraja?
1 Kumpoteza mpendwa katika kifo ni jambo lenye kufadhaisha sana, hasa kwa watu wasio na tumaini la Ufalme. (1 The. 4:13) Kwa kawaida, watu wengi wanajiuliza hivi: ‘Kwa nini watu wanakufa? Wanaenda wapi? Je, kweli nitawaona tena wapendwa wangu?’ Hapa chini pana mapendekezo machache tunayoweza kutumia kuwafariji watu tunaokutana nao katika utumishi wa shambani ambao wanaomboleza kwa sababu ya kifo cha mtu wao wa ukoo au rafiki.—Isa. 61:2.
2. Mwenye nyumba akituambia kwamba anaomboleza, je, ni lazima tujaribu kumhubiria kwa muda mrefu?
2 Tunapohubiri Nyumba kwa Nyumba: Huenda mwenye-nyumba akatuambia kwamba mtu fulani wa familia yake alikufa hivi karibuni. Je, analia au amehuzunika kupita kiasi? Je, nyumba imejaa watu wa ukoo ambao wanaomboleza? Katika hali kama hizo, huenda isifae kumhubiria kwa muda mrefu. (Mhu. 3:1, 7) Labda tunaweza kumpa pole, kisha tumwachie trakti, gazeti, au broshua inayofaa, halafu tuondoke. Kisha tunaweza kurudi wakati mwingine unaofaa na kumfariji zaidi kupitia Biblia.
3. Hali zikiruhusu, ni maandiko gani tunayoweza kumwonyesha mwenye nyumba anayeomboleza?
3 Nyakati nyingine, tunaweza kuona kwamba hali zinaturuhusu kusema mengi katika ziara ya kwanza. Ingawa huo si wakati wa kupinga maoni yasiyofaa, tunaweza kuwasomea ahadi za Biblia kuhusu ufufuo. (Yoh. 5:28, 29) Au tunaweza kuwaonyesha yale ambayo Biblia inasema kuhusu hali ya wafu. (Mhu. 9:5, 10) Simulizi la Biblia la mtu fulani aliyefufuliwa linaweza pia kuwafariji. (Yoh. 11:39-44) Au tunaweza kuchunguza pamoja naye maneno ambayo Ayubu alisema kuhusu tumaini lake katika Yehova. (Ayu. 14:14, 15) Kabla ya kuondoka, tunaweza kumwachia mwenye nyumba broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa?, Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, au trakti au broshua nyingine inayofaa. Au tunaweza kumwachia kitabu Biblia Inafundisha na kumwonyesha habari iliyo katika sura ya 6, na kupanga kuzungumzia habari hiyo tutakaporudi.
4. Tuna pindi gani nyingine za kuwafariji wengine?
4 Katika Pindi Nyingine: Ikiwa hotuba ya mazishi au ya ukumbusho itatolewa katika Jumba la Ufalme, je, watu wasio Mashahidi watahudhuria? Wanaweza kupewa vichapo vya kuwafariji. Wafanyakazi wa nyumba fulani za kuhifadhia maiti wamethamini sana kupokea vichapo vya kuwapa watu wa familia zinazoomboleza. Nyakati nyingine, matangazo ya mazishi yaliyo katika magazeti yamewapa wahubiri fursa ya kuandika barua fupi za kufariji familia zinazoomboleza. Pindi moja, baada ya kupokea barua pamoja na trakti kadhaa, mjane mmoja mwanamume pamoja na binti yake walienda kwenye nyumba ya mhubiri aliyewaandikia barua hiyo na kumuuliza hivi: “Je, ninyi ndio mlionitumia barua hii? Ningependa kujua mengi zaidi kuhusu Biblia!” Mwanamume huyo na binti yake walikubali kujifunza Biblia nao wakaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko.
5. Kwa nini tunapaswa kuwa macho kutambua nafasi za kuwafariji wale wanaoomboleza?
5 Andiko la Mhubiri 7:2 linasema hivi: “Ni afadhali kwenda katika nyumba ya maombolezo kuliko kwenda katika nyumba ya karamu.” Kwa kawaida, mtu anayeomboleza ana mwelekeo wa kusikiliza Neno la Mungu kuliko yule anayesherehekea. Sote tunapaswa kuwa macho kutambua nafasi zinazofaa za kuwafariji wale wanaoomboleza kwa sababu ya kifo cha mpendwa wao.