Yehova Hutoa Nguvu
1 Tukiwa watu wa Yehova, tumepewa mgawo wa kuhubiri habari njema huku tukidumisha mwenendo “mzuri kati ya Mataifa.” (1 Pet. 2:12; Mt. 24:14) Kwa sababu ya nyakati za hatari pamoja na udhaifu na mapungukio yetu, hatungeweza kamwe kutimiza kazi hii sisi wenyewe tu. (2 Tim. 3:1-5) Twafurahi kama nini kwamba twaweza kumtazamia Yehova atupe msaada!
2 Mtume Paulo alivumilia majaribu mengi. (2 Kor. 11:23-27) Yeye aliweza kukabilianaje na hayo na kumaliza kazi yake aliyogawiwa? Yehova alimpa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Kor. 4:7, NW) Paulo alitambua msaada huo wa kimungu alipoandika hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) Yehova atatusaidia kwa njia hiyohiyo. Twaweza kupataje usaidizi huu?
3 Kwa Kusali Bila Kukoma: Yesu alitusihi ‘tuendelee kuomba, kutafuta, na kubisha,’ na tusikate tamaa. (Luka 11:5-10) Udumifu wetu katika sala waonyesha Yehova kina cha hangaikio letu, kiwango cha tamaa yetu, na uhalisi wa nia yetu. (Zab. 55:17; 88:1, 13; Rum. 1:9-11) Paulo alitambua umuhimu wa udumifu katika sala alipotusihi ‘tuombe bila kukoma.’ (1 The. 5:17) Sala ni mojapo njia za msingi tunazopata msaada wa Yehova.
4 Kwa Kufuata Mwelekezo wa Kitheokrasi: “Theokrasi” humaanisha “utawala wa Mungu,” ambaye ni upendo. Sisi hunufaika kutokana na utawala wake kwa kukubali mamlaka yake na kufuata maagizo yake katika maamuzi makubwa na madogo. “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” huwakilisha utawala wa kitheokrasi kwenye dunia hii. (Mt. 24:45-47) Kushirikiana na tengenezo analotumia huyo “mtumwa” ni kwa muhimu ikiwa tutapata baraka za Yehova. (Linganisha Waebrania 13:17.) Yehova atathawabisha uaminifu-mshikamanifu wetu kwake na utayari wetu wa kutii sheria zake kwa kuandaa nguvu tunayohitaji kwa wakati unaofaa.—Ebr. 4:16.
5 Kwa Kuwa na Uhusiano wa Karibu na Ndugu Zetu: Upendo ni alama ya kutambulisha ya wanafunzi wa Yesu. (Yn. 13:34, 35) Kukiwa na nyutu mbalimbali, mabishano yaweza kutokea miongoni mwetu kwa sababu ya tofauti za kibinafsi. Twahitaji kuwa wenye shauku nyororo, tukisameheana kabisa. (Efe. 4:32) Kufanya hivi hutuwezesha tubaki na uhusiano wa karibu na ndugu zetu katika imani na tutiwe moyo na uvumilivu wao ulio imara chini ya jaribu. ‘Tukijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu [zetu] walioko duniani,’ tuna nguvu ya kupewa na Mungu ya kushughulika na misongo kama hiyo.—1 Pet. 5:9.
6 Kwa Kudumisha Kawaida Nzuri ya Funzo la Kibinafsi: Kuimarisha akili na mioyo yetu kiroho hutuwezesha kukinza mashambulio ya Shetani. (1 Pet. 5:8) Kawaida nzuri ya funzo la kibinafsi itaongezea akiba yetu ya ujuzi wa kimungu. Twaweza kutwaa kutokana nao tunapokabili matatizo ya kila siku. Paulo alikazia kwamba “ujuzi sahihi” huwa na sehemu muhimu sana katika kupata wokovu. (1 Tim. 2:3, 4, NW) Ni muhimu kutwaa chakula cha kiroho kwa ukawaida.
7 Maandalizi yote ya lazima ya kutusaidia tuendelee tukiwa wenye nguvu yanapatikana kupitia kutaniko la Kikristo. Uungaji mkono wa moyo mzima kwa utendaji walo utatuhakikishia kwamba ‘tutakwenda kwa miguu, wala hatutazimia.’—Isa. 40:29-31.