“Fuliza Kulinda”
1 Yesu aliposema maneno yaliyorekodiwa kwenye Mathayo 26:38-41 (NW) alikuwa akikaribia wakati ulio mgumu zaidi wa kuwapo kwake kwa kibinadamu. Ungethibitika kuwa wakati wa maana zaidi katika historia yote ya kibinadamu. Wokovu wa wanadamu wote ulikuwa hatarini. Wanafunzi wa Yesu walihitaji ‘kufuliza kulinda.’
2 Leo twasimama ukingoni mwa kufika kwa Yesu katika daraka lake lenye sehemu mbili la mkombozi na mtekeleza-hukumu. Tukiwa Wakristo wenye kulinda wanaotambua uharaka wa nyakati, hatukunji mikono yetu tu na kungoja ukombozi. Twajua kwamba lazima tuwe tayari sikuzote. Ni lazima ‘tujitaabishe na kujitahidi’ katika utumishi wetu kwa Yehova. (1 Tim. 4:10) Vipi kuhusu kila mmoja wetu tukiwa watu mmoja-mmoja? Je, twafuliza kulinda?
3 Kujichunguza Wenyewe: Yesu alionya pia: “Jiangalieni.” (Luka 21:34, 35) Twapaswa kujiangalia wenyewe, tukihakikisha kwamba tunakuwa “wasio na lawama, wala udanganyifu, . . . kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.” (Flp. 2:15) Je, kila siku twaishi tukiwa Wakristo, tukimwiga Yesu na kutembea kupatana na kanuni zilizoonyeshwa katika Neno la Mungu? Twapaswa kuepuka mwenendo usio wa Kikristo wa ulimwengu ambao ‘unakaa katika nguvu ya yule mwovu.’ (1 Yoh. 5:19, NW; Rum. 13:11-14) Tunapojichunguza wenyewe kupatana na Maandiko, je, twalinda kwelikweli kama Yesu alivyoagiza?
4 Wazee lazima wawe chonjo ili kuwa wenye bidii katika kutimiza migao yao katika kutaniko, wakitambua kwamba watatoa hesabu ya jinsi wanavyotunza kundi. (Ebr. 13:7) Vichwa vya familia vina wajibu wa pekee wa kuelekeza nyumba zao katika njia za Yehova. (Mwa. 18:19; Yos. 24:15; linganisha 1 Timotheo 3:4, 5.) Pia, ni muhimu kama nini kwamba sisi sote tutimize amri ya Kimaandiko ya kupendana! Hiyo ni alama ya Ukristo wa kweli.—1 Yn. 13:35.
5 Uwe Chonjo Kuonya Wengine: Kufuliza kulinda hutia mengi kuliko kujiangalia sisi wenyewe. Tuna agizo la kufanya wengine kuwa wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Upendo kwa jirani wapaswa kutuchochea kuwaonya wengine ili waweze kuokoka uharibifu unaokabili ulimwengu huu. Hili ni daraka la Wakristo wote. Ni sehemu muhimu ya ibada yetu. (Rum. 10:9, 10; 1 Kor. 9:16) Mara nyingi sisi hukabiliana na ubaridi au upinzani mkali kwa kazi hii ya kuokoa uhai. Tuna wajibu wa kuendelea, hata kama wengi wanapuuza onyo letu. (Eze. 33:8, 9) Upendo halisi kwa Mungu na jirani utatuchochea tuvumilie.
6 Huu si wakati wa kutulia. Wala hatupaswi kuruhusu mahangaiko ya kila siku ya maisha kutukengeusha wala kujiingiza zaidi katika anasa za mfumo huu hivi kwamba yawe mtego. (Luka 21:34, 35) Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, kuna uharaka. Wakati unakaribia upesi zaidi kwa Yesu Kristo kutekeleza hukumu dhidi ya mfumo huu mbovu. Ni wale tu walio macho, chonjo, na wenye kulinda watakaookoka. Tukitii maagizo ya Yesu na “kuokoka katika hayo yote yatakayotokea,” tutashukuru kama nini!—Luka 21:36.