Fanya Ziara za Kurudia kwa Maangusho Yote ya Broshua
1 Mtume Paulo aliwapongeza Wafilipi kwa sababu ‘walihuisha tena fikira zao kwa ajili yake.’ (Flp. 4:10) Tukitumia kielelezo chao kuwa kigezo kwa huduma ya shambani, ‘tutahuisha fikira zetu’ kwa ajili ya wale ambao twawatolea ushahidi na kuchochewa kufanya ziara za kurudia.
2 Ikiwa uliangusha broshua “Serikali Itakayoleta Paradiso,” waweza kusema jambo kama hili:
◼ “Nilikuwa nikifikiria juu ya mazungumzo tuliyokuwa nayo siku ile, na maandiko mawili yalinijia akilini ambayo ningependa kuyashiriki nawe. Huenda unakumbuka kwamba tuliongea kuhusu Mungu akitwaa utawala wa dunia. Katika Biblia, Yehova Mungu ameahidi kwamba jambo hili litatukia. [Soma Danieli 2:44.] Je, waamini kwamba jambo hilo kweli laweza kutokea? [Ruhusu itikio.] Sikiliza anayosema Mungu juu ya uwezo wake wa kutimiza ahadi zake. [Soma Isaya 55:11.] Je, hilo halipaswi kututia moyo tuweke tumaini letu katika Ufalme wa Mungu? Lakini ni lini Mungu atakapotimiza ahadi zake?” Eleza kwamba utajibu swali hilo kwenye ziara yako ijayo.
3 Unaweza kutumia mfikio huu unapofanya ziara ya kurudia kwa mtu aliyechukua broshua “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa”:
◼ “Nilifanya jitihada ya pekee kurudi, kwa sababu ya mazungumzo yetu juu ya kumpoteza mtu fulani katika kifo.” Onyesha kielezi kwenye ukurasa 30 unaposema: “Wakumbuka mandhari hii ya furaha ya watu wakifufuliwa na kuunganishwa na wapendwa wao? Nilikuuliza swali juu ya ni wapi jambo hili litatendeka, mbinguni au duniani. Labda ulipata jibu la Biblia kwenye ukurasa 26 wa broshua hii.” Zungumzia mambo makuu katika fungu la tatu hadi la tano, na usome Yohana 5:21, 28, 29. Wakati ukiruhusu, soma yoyote ya maandiko yaliyobaki kwenye huo ukurasa.
4 Je, ulianzisha funzo katika “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”? Kwenye ziara ya kurudia, unaweza kufanya hivi:
◼ Rejezea tena kwenye ukurasa 30, na uelekeze kwenye lile swali: “Biblia ni yenye kutokeza katika njia zipi?” Fungua kurasa 3 na 4, na upitie mafungu 1-4 pamoja na kielezi kwenye jalada la broshua. Soma andiko moja au mawili yaliyowekwa bila manukuu katika kielezi-chini kwenye fungu la 4. Eleza kwamba Biblia ndicho kitabu pekee ambacho hutoa tumaini ajabu kama hilo. Fanya mipango ya ziara yako ijayo. Baada ya ziara ya tatu, kama yaonekana funzo litaendelea, unaweza kuanza kuripoti funzo jipya!
5 Waweza kuendeleza mazungumzo kwenye “Jina la Mungu Litakaloendelea Milele” kwa njia hii:
◼ “Wakati uliopita, niliweza kukuonyesha jina la Mungu katika Biblia. Kujua na kulitumia jina Yehova ni sehemu muhimu ya ibada yetu.” Fungua ukurasa 31, pitia mambo makuu katika mafungu manne ya mwisho, na usome Yohana 17:3, na Mika 4:5. Eleza kwamba sisi hutoa programu ya funzo la Biblia linaloweza kuonyesha jinsi jina la Mungu litakavyotakaswa kwa njia nzuri na jinsi tunavyoweza kufurahia baraka za dunia iliyo paradiso.
6 Kwa hiyo, huisha fikira zako kwa ajili ya wale uliowafikia. Endelea kurudi tena, na utayarishe jambo lenye manufaa la kushiriki. Unaweza kuwa ‘yule azaaye matunda’ katika kufanya wanafunzi wapya.—Mt. 13:23.