Ziara za Kurudia Zenye Mafanikio Zahitaji Kufundisha Kwenye Matokeo
1 Ziara za kurudia ni sehemu muhimu na yenye shangwe ya huduma yetu ya shambani. Kwa nini twapaswa kuwa wenye juhudi kurudia watu wenye kupendezwa? Jina la Yehova lajulishwa na kuheshimiwa kwa kazi hii ya kufanya wanafunzi, nao wenye kuhofu Mungu wanasaidiwa kupata njia ya kuelekea kwenye uhai. (2 Kor. 2:17–3:3) Kutambua kwamba kutakaswa kwa jina la Yehova na maisha ya wengine pia yahusika kwapaswa kutuchochee tujitayarishe vizuri kabla ya kurudi.
2 Mwalimu mzuri atasaidia mwanafunzi ajenge kwenye msingi uliowekwa tayari. Kama vile tu mwalimu wa shule ajengavyo kwenye ujuzi ambao wanafunzi hupata siku kwa siku, twapaswa kwa ukawaida kufuatia ziara zetu za kwanza kwa maelezo zaidi ya habari ileile. Hili hutokeza kuendelezwa kwa wazo na kufikiri kwenye maendeleo.
3 Unaporudi baada ya kuangusha broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?” huenda ukaona huu ukiwa wenye matokeo:
◼ “Wakati wa ziara yangu iliyopita, tulikuwa tukizungumzia ‘siku za mwisho’ zinazotajwa katika Biblia na linalomaanisha kwetu. Huenda ukashangaa jinsi tujuavyo kwamba tunaishi katika siku za mwisho. (2 Tim. 3:1) Wanafunzi wa Yesu walikuwa na hamu ya kupata jibu la swali hilo. [Soma Mathayo 24:3.] Katika kujibu kwake, Yesu alifafanua hali ambazo tunaona leo karibu yetu. Hizi zatia ndani mikazo na jeuri ambazo hazijapata kuonekana mwanzoni.” Onyesha sehemu ya ishara inayozungumziwa katika fungu la 3 na 4 kwenye ukurasa 19. Ikiwa itikio ni zuri, onyesha sehemu nyingine za ishara katika mafungu 5 hadi 8 kwenye ukurasa 20. Jitolee urudi mzungumzie maswali yanayotokezwa mbele ya broshua hiyo.
4 Kufuatia kupendezwa katika broshua “Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?—Wewe Waweza Kulipataje?” waweza kusema:
◼ “Nimekuwa na hamu ya kuendeleza mazungumzo yetu juu ya kusudi letu la kuishi. Nafikiri sisi sote twakubaliana kwamba Mungu alikusudia tuishi kwenye dunia hii katika hali zenye furaha na amani badala ya mateseko tunayopata leo. Wafikiri atatimiza ahadi yake?” Ruhusu itikio. Soma Isaya 55:11, kisha uzungumzie mawazo yaliyo katika mafungu 25 hadi 27 kwenye ukurasa 30. Pendekeza funzo la kibinafsi la Biblia kuwa njia bora ya kupata kusudi lifaalo maishani.
5 Ili kufuatia kupendezwa kulikoonyeshwa wakati uliopita katika broshua “Furahia Milele Maisha Duniani!” ungeweza kuionyesha tena na kusema:
◼ “Tuliongea kuhusu ulimwengu maridadi unaoonyeshwa kwenye jalada la broshua hii. Nataka kukuambia ni kwa nini imani katika Yesu Kristo ni ya maana sana kwa watu wanaotaka kuishi hapa.” Fungua picha 41, na usome Isaya 9:6. Rejezea kwenye picha 62, na usome Yohana 3:16, ukikazia uhitaji wa utii. Eleza kwamba Mashahidi wa Yehova wanasaidia watu kujifunza jinsi ya kuonyesha imani kwa kujifunza Biblia na kujaribu kuishi kupatana na shauri layo.
6 Baada ya kila ziara ya kurudia, ichanganue ukiwa na lengo la kuboresha matokeo yako. Jiulize mwenyewe: Nilikuwa na jambo hususa akilini la kusema? Nilikazia uangalifu kwenye Biblia? Nilijenga kwenye msingi uliowekwa kulingana na ziara ya kwanza? Utoaji wangu ulikusudiwa kuongoza kwenye funzo la Biblia? Majibu yaliyo chanya yatoa uhakikisho kwamba unajitahidi kuwa mwalimu mzuri wa Neno la Mungu.