Nawezaje Kumfanya Mtu Anisikilize?
1 Katika jiji la Filipi, ‘mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, . . . akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo.’ (Mdo. 16:14) Kisa hiki chatufunza nini? Kusikiliza ndiko hufungua mlango wa mtu kujifunza kweli. Mafanikio yetu katika kushiriki jumbe za Ufalme hutegemea hasa utayari wa mwenye nyumba wa kusikiliza. Mara tusikilizwapo, ni rahisi kwa kadiri kueleza ujumbe wetu. Lakini kumfanya mtu asikilize kwaweza kuwa kugumu. Twaweza kufanya nini?
2 Kabla ya kushiriki katika utumishi, twapaswa kuangalia sura yetu na vifaa tutakavyokuwa tukitumia. Kwa nini? Watu huelekea kusikiliza mtu anayejiendesha kwa njia ya adhama. Je, sisi huvalia kwa njia ya kupendeza lakini kwa kiasi? Ijapokuwa kuvalia kizembe huenda kukapendwa ulimwenguni, sisi twaepuka ukosefu huo wa kujali kwa sababu sisi ni wahudumu wanaowakilisha Ufalme wa Mungu. Sura yetu iliyo safi na nadhifu huongeza ushuhuda wenye upendezi kwa ujumbe wa Ufalme tunaohubiri.
3 Uwe Mwenye Urafiki na Mwenye Staha: Ijapokuwa mitazamo ya leo yenye kubadilika, watu wengi bado huheshimu Biblia nao wataitikia kwa upendezi mazungumzo yenye staha na ya kirafiki kuhusu yaliyo kwenye Biblia. Tabasamu changamfu na ya kweli yaweza kumtuliza mwenye nyumba na kutoa fursa ya mazungumzo yenye kupendeza. Unyoofu wetu na tabia zetu nzuri zapaswa kuonekana katika usemi na mwenendo wetu, ambao hutia ndani kusikiliza kwa staha maoni ya mwenye nyumba.
4 Kusudi letu ni kushiriki tumaini la Biblia pamoja na wengine. Tukiwa na jambo hili akilini, twapaswa kuhakikisha kwamba mazungumzo yanavutia, yasiyo ya kiadui au yenye kushindana. Hakuna haja ya kupoteza wakati kubishana na mtu ambaye kwa wazi ni mwenye kupinga. (2 Tim. 2:23-25) Twaweza kuteua utoaji kutoka aina mbalimbali za utoaji wenye kutia moyo na wa wakati ufaao tunaoandaliwa kwenye Huduma ya Ufalme Yetu na kitabu Kutoa Sababu. Bila shaka, twahitaji kutayarisha mambo haya vizuri ili tuweze kusema kwa njia changamfu na yenye kusadikisha.—1 Pet. 3:15.
5 Baada ya ziara yetu, ni wenye nyumba wachache wawezao kukumbuka tuliyosema hasa. Hata hivyo, karibu wote watakumbuka njia ambayo mambo hayo yalisemwa. Hatupaswi kamwe kupuuza uwezo wa wema na fadhili. Kwa kweli kuna watu wengi wenye mfano wa kondoo katika eneo letu ambao watasikiliza kweli kama vile Lidia alivyofanya katika karne ya kwanza. Kutoa uangalifu zaidi kwa sura yetu na namna ya usemi wetu kwaweza kutia moyo watu wanyoofu wasikilize Neno la Mungu na kulipokea kwa upendezi.—Mk. 4:20.