Rudia Wale Walioonyesha Kupendezwa
1 Alipokuwa akitoa kitabu kipya, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, msemaji wa mkusanyiko alieleza kwamba “wanafunzi wenye mioyo ya haki watazamiwa waweze kujifunza mengi ya kutosha kupitia funzo lacho ili wachukue msimamo upande wa Yehova na wabatizwe.” Kitabu hicho kimekusudiwa kifundishe kweli haraka. Kinaeleza kwa ufupi habari inayoweza kuwachochea wanafunzi wafanye maendeleo ya kiroho. Hutoa kweli katika njia chanya bila kukazia mafundisho bandia. Ili kupata mafanikio katika kutumia kifaa hiki kipya, lazima tufanye ziara za kurudia kwa wale walioonyesha kupendezwa.
2 Kwa wale walioonyesha kupendezwa katika Biblia kuwa mwongozo ufaao, unaweza kurudi ili kutoa funzo, labda kwa kusema:
◼ “Nilipokuwa hapa mbeleni, tulizungumza kwa nini twaweza kutumaini Biblia kuwa chanzo kinachofaa cha mwongozo. Kwa sababu imepuliziwa na Mungu, Biblia pia ni chanzo hakika cha faraja na tumaini, kama vile tu mmojawapo mitume wa Kristo alivyosema. [Soma Warumi 15:4.] Mwishoni mwa mazungumzo yetu yaliyopita, nilitokeza swali, Twaweza kunufaikaje kibinafsi na ujuzi ulio katika Biblia?” Soma fungu la 18 kwenye ukurasa wa 11 katika kitabu Ujuzi. Mweleze kwamba Mashahidi wa Yehova wanaongoza mafunzo ya Biblia yapatayo milioni tano ulimwenguni pote, wakisaidia watu kila mahali watwae ujuzi uongozao kwenye uhai udumuo milele. Toa wonyesho mfupi wa jinsi funzo linavyoongozwa, ukitumia mafungu matano ya kwanza katika sura ya 1.
3 Ikiwa mlizungumza na mtu fulani kuhusu sala mara ya kwanza, unaweza kujaribu mfikio huu katika jitihada ya kuanzisha funzo:
◼ “Natumaini mlifurahia habari iliyohusu sala ambayo tulizungumzia kutoka kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Niliahidi kurudi ili kuchunguza nawe jinsi wale wanaoomba Mungu wanavyoweza kumsikiliza yeye pia. Ona yale yanayosemwa kwenye ukurasa wa 158. [Soma fungu la 18.] Hivyo kwa kujifunza Biblia kibinafsi, twasikiliza yale Mungu hutuambia. Kufanya hivyo hutuleta karibu naye na hutusaidia tushughulike na matatizo ya kila siku ambayo sisi husali kuyahusu. Nitafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe.” Unaweza kuanza na sura ya kwanza ya kitabu Ujuzi.
4 Ikiwa unarudi kumtembelea mzazi anayehangaikia matatizo ya familia yake, waweza kusema hivi:
◼ “Najua kuwa wewe ukiwa mzazi, unawatakia watoto wako mema. Kwa kuwa haiwezekani kuwakinga kutokana na kila kitu kilicho kibaya, wewe wapaswa kuwafundisha jinsi ya kukabiliana na matatizo ya maisha. Je, wafikiri hilo laweza kufanywaje? [Ruhusu itikio.] Mojapo mambo ya maana ambayo mzazi aweza kuandaa ni mazoezi.” Fungua kwenye kurasa 145-146 katika kitabu Ujuzi, na uvute uangalifu katika shauri la Biblia lenye kutumika, ukikazia umaana walo na jinsi kulifuata kwaweza kuwa baraka. Jitolee kurudi tena ili uonyeshe jinsi ya kutumia kitabu hicho ili kujifunza mengi zaidi kuhusu kupata maisha ya familia yenye furaha.
5 Ikiwa unarudi mahali ambapo ulitumia utoaji mfupi, ungeweza kusema:
◼ “Halikuwa kamwe kusudi la Mungu tuzeeke na kufa. Yeye alikusudia kwamba tuishi milele katika dunia iliyo paradiso.” Onyesha kielezi kwenye kurasa 188-189. Soma fungu la 11 kwenye ukurasa 184. Fanya mipango kwa ajili ya ziara nyingine za kurudia.
6 Kwa hakika kitabu hiki kipya ni uandalizi mwingine kutoka kwa Yehova ili ‘kuhimiza’ kazi ya kukusanya katika siku hizi za mwisho. (Isa. 60:22) Tukikitumia kwa matokeo, twaweza kutoa ujuzi uwezao kusaidia mtu apate uhai udumuo milele.