Kutoa Kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
1 Tulifurahia wee wakati kitabu kipya, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilipotolewa! Kimekusudiwa kusaidia watu wapate upesi ujuzi sahihi kuhusu kweli. Katika Machi tutakuwa na fursa ya kwanza ya kutoa kitabu hiki katika eneo letu. Twaweza kusema nini ili kuamsha kupendezwa?
2 Unaweza kutumia utoaji unaoonyesha Biblia kuwa chanzo kinachofaa cha mwongozo, kwa kusema:
◼ “Tunazungumza na jirani zetu tunakoweza kupata chanzo kinachofaa cha mwongozo wa kukabiliana na matatizo ya maisha. Zamani watu wengi kwanza waliiendea Biblia. Lakini sasa mitazamo ya watu imebadilika; watu fulani wana shaka kuhusu Biblia, wakiiona kuwa kitabu kilichoandikwa na wanadamu. Maoni yako ni nini? [Ruhusu itikio.] Kuna sababu nzuri sana zinazofanya Biblia iweze kusemwa kuwa ni yenye kufaa siku yetu. [Soma 2 Timotheo 3:16, 17.] Kanuni za Biblia hutumika pia leo kama vile zilivyotumika wakati Mungu alipulizia uandikaji wa Biblia.” Fungua ukurasa wa 16 katika kitabu Ujuzi, na utoe maelezo kifupi juu ya mwongozo unaofaa upatikanao katika Mahubiri ya Mlimani ya Yesu. Soma nukuu lililo kwenye fungu la 11 au lile lililo kwenye fungu la 13. Toa kitabu, na upange kurudi ili kujibu swali hili, Sisi binafsi twaweza kunufaikaje na ujuzi upatikanao katika Biblia?
3 Kwa kuwa sala ni jambo la kupendeza watu wengi, huenda ukataka kuizungumza kwa kuuliza:
◼ “Kukiwa na magumu ambayo lazima tukabili katika maisha ya siku ya kisasa, je, wafikiri kwamba sala yaweza kuwa yenye msaada kwetu? [Ngojea itikio.] Wengi wanahisi kwamba wamemkaribia Mungu kwa kumwomba na kwamba kufanya hivyo kumewapa nguvu ya ndani, jambo ambalo Biblia inaahidi. [Fungua kitabu Ujuzi kwenye ukurasa wa 156, na usome Wafilipi 4:6, 7.] Hata hivyo, huenda mtu akahisi sala zake wakati mwingine hazijibiwi. Sura hii yazungumzia ‘Jinsi Unavyoweza Kumkaribia Mungu.’ [Toa kitabu.] Sura hii pia hueleza jinsi tunavyoweza kumsikiliza Mungu, kwa kuwa mawasiliano naye si ya upande mmoja. Twaweza kuzungumzia hayo nitakaporudi.”
4 Ukikutana na mzazi, waweza kukazia uangalifu familia:
◼ “Wazazi walio wengi hukubali kwamba kuna matatizo mengi katika kujaribu kudumisha maisha ya familia yenye furaha. Ni nini unayoona kuwa vizuizi vikubwa zaidi? [Ruhusu itikio.] Wengi wetu hufanya yote tuwezayo, lakini mara nyingi twathamini usaidizi ambao utatusaidia tupate matokeo bora. Biblia hutoa ushauri mzuri zaidi. [Soma sehemu za Wakolosai 3:12, 18-21.] Biblia ina mengi zaidi ya kusema kuhusu habari hii, kama ionyeshwavyo katika sura ya 15 ya kitabu hiki, yenye kichwa ‘Kujenga Familia Inayomheshimu Mungu.’ Hiyo sura hupitia shauri linalotolewa katika Biblia kuonyesha jinsi ya kupunguza mkazo wa ndoa na jinsi ya kukabiliana na matatizo yanayowapata watoto wetu. Nina hakika utafurahia kukisoma.”
5 Ikiwa wapendelea jambo fupi, waweza kujaribu hili:
◼ “Je, umepata kujiuliza ni kwa nini tunazeeka na kufa? Sura ya 6 katika kitabu hiki yaeleza kisababishi cha kifo na jinsi Mungu atakavyokiondoa. Biblia hutuambia kwamba Mungu ameahidi uhai udumuo milele kwa wale wanaompenda. [Soma Yohana 17:3.] Ikiwa ungependa kusoma kuhusu hili, utaona hiki kitabu kuwa chenye kuelimisha zaidi.”
6 Tukiwa tumejitayarisha vizuri, twaweza kutumia kitabu hiki ‘kufunulia wengine Maandiko’ kwa njia itakayowaletea shangwe kubwa!—Luka 24:32.