Kutoa Habari Njema Tukiwa na Mtazamo Chanya
1 Sisi sote hupenda kupata shangwe na kutimiza tunayofanya, katika kazi ya kufanya wanafunzi. Ni nini kituleteacho uradhi huo? Huanza na kudumisha kwetu mtazamo chanya wa akilini tunapokuwa wenye shughuli katika kazi istahiliyo ya kusaidia wengine. (Mit. 11:25) Namna yetu ya kutangaza habari njema yapaswa ionyeshe kwamba kwa kweli twaamini yale tunayosema. Tukisema kutoka moyoni mwetu, basi weupe wa moyo na usadikisho wetu utaonekana wazi. (Luka 6:45) Kwa kurudia utoaji wetu, tutahisi uhakika zaidi tunaposema na watu katika eneo letu. Kufanya hivyo kutakuwa na thamani hasa wakati wa Septemba tunapotoa vichapo Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? au Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha. Huenda ukaona madokezo yafuatayo kuwa yenye msaada katika kutoa habari njema kwa mtazamo chanya.
2 Unapotoa kitabu “Creation,” unaweza kusema hivi kwenye ziara ya kwanza:
◼ “Katika kuongea na jirani zetu, tumepata kwamba walio wengi wana uhakika katika Mungu. Wengine huona ni vigumu kumwamini. Wewe waonaje? [Ruhusu itikio.] Ona jinsi Biblia husababu juu ya jambo hili. [Soma Warumi 1:20.] Twaweza kuona ithibati ya ‘uweza na Uungu’ wa Mungu kwa kuchunguza vitu alivyoumba.” Soma fungu la mwisho kwenye ukurasa wa 48 wa kitabu Creation, na uvute uangalifu kwenye utata wa chembe iliyo hai. Au tumia fungu la 18 kwenye ukurasa 147 uonyeshe jinsi mfumo wenye kustaajabisha wa mzunguko wa mti unavyokazia kazi ya Muumba. Toa kitabu kwa mchango wa kawaida.
3 Unaporudi kuongea na wale ambao ulizungumza nao kuhusu Uwezo wa Kuumba wa Mungu, unaweza kusema hivi:
◼ “Katika ziara yangu iliyopita, tuliongea juu ya uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu, yaani, uumbaji wake wa ajabu. Je, wewe huona ni vigumu kuamini kwamba Yule aliyeumba ulimwengu wote mzima pia angependezwa na wakati wetu ujao? [Ruhusu itikio.] Inapendeza kuona kwamba wakati ujao tayari umeamuliwa na Muumba.” Soma Isaya 46:9, 10. Tumia picha na maelezo yayo katika sura ya 19 ya kitabu Creation kukazia hali zilizo bora kabisa zilizoahidiwa na Mungu. Soma fungu la 1 la sura ya 20, na umtolee funzo la Biblia. Likikubaliwa, anzisha funzo hilo katika kitabu Ujuzi.
4 Watoto wanahitaji wakati ufaao na mazoezi kutoka kwa wazazi wao. Katika kutoa kitabu “Maisha ya Jamaa,” unaweza kusema:
◼ “Sisi sote twahangaikia wakati ujao wa vijana wetu. Kwa maoni yako, ni njia ipi iliyo bora sana ambayo wazazi wanaweza kusaidia watoto wao wapate wakati ujao wenye uhakika? [Ruhusu itikio.] Sikiliza shauri hili litokalo kwenye mithali ya Biblia iliyoandikwa yapata miaka 3,000 iliyopita. [Soma Mithali 22:6.] Ijapokuwa watoto wanaweza kunufaika sana na maagizo wapokeayo shuleni, mazoezi yao yenye thamani zaidi yanatolewa nyumbani na wazazi wao. Yanahitaji wakati, uangalifu, na upendo, lakini jitihada hiyo yastahili.” Fungua ukurasa 115, zungumza fungu moja au mafungu mawili chini ya kichwa kidogo, kisha ueleze jinsi kitabu hicho kiwezavyo kutumiwa kuwa msingi wa funzo la Biblia la familia.
5 Ikiwa uliongea kuhusu watoto na uhitaji wao wa mazoezi, unaweza kuendeleza mazungumzo kwa njia hii:
◼ “Wakati uliopita tuliongea kuhusu mazoezi ya kiroho ambayo watoto wetu wanahitaji na jinsi wazazi wanavyoweza kuwasaidia. Wazazi walio wengi niliosema nao wanajua kuhusu mwenendo mbaya wa vijana wengi leo. Wewe wafikiri nini kuhusu . . . ? [Taja kielelezo kimoja kinachojulikana cha mwenendo mbaya wa vijana katika jamii yenu. Ruhusu itikio.] Acha nikuonyeshe baadhi ya shauri lenye kutumika lililo katika Biblia.” Fungua kwenye mafungu 3 na 4 kwenye ukurasa 162 katika kitabu Maisha ya Jamaa, zungumza jambo kuu, na usome Maandiko. Kazia kwamba watoto walio wengi kwa kweli wanataka nidhamu na mwongozo. Wazazi wakiwa na bidii kuuandaa, watoto wanakuwa na furaha na wenye staha zaidi katika mwenendo wao. Eleza jinsi tunavyojifunza Biblia na watoto wetu.
6 Unapohubiri duka kwa duka, waweza kutumia mfikio huu mfupi ukiwa na kitabu “Creation”:
◼ “Leo twawatolea utumishi wa pekee wafanyabiashara wa jumuiya. Sisi sote twahangaishwa na ongezeko la uhalifu na jeuri katika eneo letu. Je, wafikiri kuna yeyote aliye na suluhisho la tatizo hili? [Ruhusu itikio.] Mungu ana suluhisho.” Fungua ukurasa 196 wa kitabu Creation; soma na ueleze juu ya Mithali 2:21, 22 katika fungu la 19. Onyesha kichwa cha sura ya 16, na utoe kitabu.
7 Unapofanya ziara ya kurudia kwa mfanyabiashara ambaye ulimwangushia kitabu “Creation,” unaweza kusema hivi:
◼ “Katika ziara yangu ya mwisho, nilitaja kwamba Mungu tu ndiye aliye na utatuzi wa kudumu kwa uhalifu na jeuri. Kulingana na ahadi yake, twaweza kutumaini kwamba dunia yenye amani itakuwapo. Ona uchaguzi unaowekwa mbele ya kila mmoja wetu.” Soma fungu la 11 kwenye ukurasa wa 250 wa kitabu Creation, kutia ndani Zaburi 37:37, 38. Toa maelezo juu ya picha iliyo kwenye ukurasa 251, na usome sentensi ya kwanza ya fungu la 14. Toa funzo la Biblia bila malipo, liongozwe mahali pao pa biashara au nyumbani mwao.
8 Tukiwa “wafanya kazi pamoja na Mungu,” tuna kila sababu ya kuwa chanya tunapotoa habari njema. (1 Kor. 3:9) Kusitawisha kwetu mtazamo huu kutatokeza baraka nyingi za Yehova.