Hubiri Ufalme
1 Kwenye Waebrania 10:23, twahimizwa ‘tulishike sana ungamo la tumaini letu.’ Na tumaini letu lautegemea Ufalme wa Mungu. Yesu aliamuru hususani kwamba habari njema ya Ufalme lazima ihubiriwe kwa mataifa yote. (Mk. 13:10) Twahitaji kukumbuka jambo hili tunaposhiriki katika huduma yetu.
2 Tunapofikia watu, twajaribu kuanzisha mazungumzo juu ya jambo linalowapendeza au linalowahangaisha. Kwa kawaida sisi hutaja mambo wanayojua, kama vile uhalifu katika ujirani, matatizo ya vijana, mahangaiko kuhusu kutafuta riziki, au tatizo fulani katika mambo ya ulimwengu. Kwa kuwa akili za watu walio wengi zimekazia haya “masumbufu ya maisha,” tunapowaonyesha kwamba tunajali na kuelewa, watu mara nyingi wataeleza yaliyo akilini mwao. (Luka 21:34) Hili laweza kutufungulia njia ya kushiriki pamoja na wengine tumaini letu.
3 Hata hivyo, tusipokuwa waangalifu, mazungumzo yaweza kuwa juu ya mambo yaliyo hasi mpaka tushindwe kutimiza kusudi la kuzuru kwetu, yaani, kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ingawa twavuta uangalifu kwenye hali mbaya zinazoleta msononeko mwingi sana, mradi wetu ni kuvuta uangalifu kwenye huo Ufalme ambao mwishowe utatatua matatizo yote ya wanadamu. Tuna tumaini zuri ajabu kwelikweli ambalo watu wanahitaji sana kulisikia. Kwa hiyo ijapokuwa huenda mara ya kwanza tukazungumzia baadhi ya mambo ya hizi “siku za mwisho zenye hatari,” twapaswa upesi kukazia fikira ujumbe wetu mkuu, ile “Injili [“habari njema,” NW] ya milele.” Kwa njia hii tutatimiza huduma yetu kikamili.—2 Tim. 3:1; 4:5; Ufu. 14:6.