Tunawaambia Wengine Kuhusu Tumaini Letu la Ufalme
1 Katika siku hizi za mwisho zilizo hatari, watu wengi katika ulimwengu hawana tumaini. (Efe. 2:12) Wengine kwa kukosa hekima wameweka tumaini lao katika vitu vya kimwili, watawala wa kibinadamu, sayansi ya kisasa, na kadhalika. Tunafurahi sana kwamba tuna tumaini la kweli la wakati ujao, tumaini ambalo ni “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara”!—Ebr. 6:19.
2 Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, dunia itageuzwa kuwa paradiso. Wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa. (Mdo. 24:15) Umaskini, ukosefu wa haki, magonjwa, uzee, na kifo havitakuwapo tena. (Zab. 9:18; Mt. 12:20, 21; Ufu. 21:3, 4) Hizo ni baadhi ya ahadi za Yehova ambazo zitatimia hivi karibuni. Unatamani kuona ahadi gani hasa ikitimizwa?
3 Tangaza Habari Njema: Hatupaswi kuwanyima wengine tumaini la Ufalme. Kumpenda Mungu na jirani kutatuchochea kumwiga Yesu na “kuwatangazia maskini habari njema, . . . kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru.” (Luka 4:18) Mtume Paulo alihubiri habari njema sokoni na mahali popote pale ambapo watu walipatikana. Alijishughulisha sana na huduma. (Mdo. 18:5) Kuiga mfano wake na kuhubiri kwa bidii, kutafanya tumaini letu la Kikristo lisidhoofishwe na “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri.”—Marko 4:19.
4 Tumaini letu la Ufalme halififii tunapokutana na watu ambao hawajali, hawapendezwi na ujumbe wa Ufalme, au wanaotupinga waziwazi. ‘Tunashika imara tangazo la hadharani la tumaini letu bila kuyumba-yumba.’ (Ebr. 10:23) ‘Hatuionei aibu habari njema.’ (Rom. 1:16) Huenda hatimaye usadikisho wetu unaoonekana wazi na uvumilivu wetu ukawachochea watu fulani wasikilize.
5 Ingawa inafaa kutaja hali za ulimwengu zinazozidi kuzorota ambazo zinatimiza unabii wa Biblia, sisi si wahubiri wa maangamizi. Badala yake, huduma yetu inakazia tumaini letu la Ufalme, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu. Acheni tuhubiri habari hiyo njema kwa usadikisho na bidii “ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.”—Ebr. 6:11.