Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 34 uku. 202-uku. 205 fu. 4
  • Uwe Mwenye Kujenga na Kutia Moyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe Mwenye Kujenga na Kutia Moyo
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi ya Kuboresha Stadi za Mazungumzo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Uwe Mwenye Kujenga
    Huduma Yetu ya Ufalme—1995
  • Uwe Mwenye Kujenga na Mwenye Kutia Moyo
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 34 uku. 202-uku. 205 fu. 4

SOMO LA 34

Uwe Mwenye Kujenga na Kutia Moyo

Unahitaji kufanya nini?

Badala ya kuzungumzia sana mambo yenye kuvunja moyo, zungumzia mambo yanayoleta tumaini.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Watu wamelemewa na ulimwengu usio na upendo. Wengi wana matatizo makubwa. Tukitangaza ujumbe wa Biblia kwa njia inayofaa, tunaweza kuwapa tumaini watu wenye mioyo minyofu.

TUMEAGIZWA tutangaze habari njema. Yesu alisema: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Mk. 13:10) Yesu mwenyewe alituwekea mfano kwa ‘kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 4:43) Mahubiri ya mitume pia yalitajwa kuwa “habari njema ya Mungu” na “habari njema juu ya Kristo.” (1 The. 2:2; 2 Kor. 2:12) Ujumbe kama huo unajenga na kutia moyo.

Sisi huwahimiza watu ‘wamhofu Mungu na kumpa utukufu’ kulingana na himizo la “malaika arukaye katika mbingu ya kati” la kutangaza “habari njema idumuyo milele.” (Ufu. 14:6, 7) Kila mahali sisi huzungumza juu ya Mungu wa kweli, jina lake, sifa zake bora, kazi zake za ajabu, kusudi lake lenye upendo, wajibu wetu kwake, na matakwa yake. Habari njema inatia ndani ujumbe wa kwamba Yehova Mungu atawaharibu waovu ambao wanamshushia heshima na kuharibu maisha ya wengine. Lakini si kazi yetu kuhukumu wale tunaowahubiria. Tunataka watu wengi iwezekanavyo wakubali ujumbe wa Biblia ili ujumbe huo kwa kweli uwe habari njema kwao.—Mit. 2:20-22; Yn. 5:22.

Usizungumzie Sana Matatizo. Ni kweli kwamba maisha yana matatizo. Na hatuyapuuzi matatizo hayo. Ili kuanzisha mazungumzo, unaweza kutaja tatizo wanalopata watu wa eneo lenu na ulizungumzie kwa ufupi. Lakini kwa ujumla hakuna faida ya kuzungumzia tatizo kwa urefu. Watu husikia daima habari zenye kuhuzunisha, kwa hiyo ikiwa unazungumzia matatizo wanaweza kufunga milango yao au kukataa kusikiliza. Mwanzoni-mwanzoni mwa mazungumzo, jaribu kumwonyesha kweli zenye kuburudisha za Neno la Mungu. (Ufu. 22:17) Kisha, hata kama hataki kuendelea na mazungumzo, utakuwa umemweleza jambo lenye kujenga ambalo anaweza kufikiria. Hiyo inaweza kumfanya asikilize zaidi wakati mwingine.

Vivyo hivyo, ukialikwa kutoa hotuba, usiwalemee wasikilizaji kwa kukazia mno matatizo kwa sababu tu kuna habari chungu nzima za matatizo. Msemaji akizungumzia kwa urefu kushindwa kwa watawala wa kibinadamu, ripoti za uhalifu na ujeuri, na kuenea sana kwa ukosefu wa adili, wasikilizaji wanaweza kuhuzunika. Zungumzia mambo yasiyopendeza ikiwa tu mambo hayo ni muhimu katika hotuba. Kutaja kidogo tu mambo kama hayo kunaweza kuthibitisha kwamba hotuba hiyo inafaa wakati huo. Pia hotuba yako inaweza kutaja visababishi vya hali fulani na uitumie kuonyesha ubora wa suluhisho linalotajwa katika Biblia. Inapowezekana, taja mambo hususa bila kuzungumzia matatizo kwa urefu.

Kwa kawaida, haiwezekani wala haitakikani kuondoa habari zote zinazozungumzia matatizo kwenye hotuba. Jambo muhimu ni kuzungumzia mambo mazuri na mambo mabaya kwa njia ya kwamba mwishowe hotuba yenyewe inakuwa yenye kutia moyo. Ili ufaulu, ni lazima uamue habari za kutaja, habari ambazo hutataja, na mambo ya kukazia. Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu aliwahimiza wasikilizaji waepuke ubinafsi wa waandishi na Mafarisayo, akataja mifano michache inayothibitisha mambo hayo. (Mt. 6:1, 2, 5, 16) Lakini, badala ya kuzungumzia mno matendo mabaya ya wale viongozi wa kidini, Yesu alikazia uhitaji wa kuelewa njia za kweli za Mungu na kuzifuata maishani. (Mt. 6:3, 4, 6-15, 17-34) Maneno yake yalitia moyo sana.

Uwe Mwenye Kutia Moyo. Ikiwa umepewa mgawo wa kutoa hotuba katika kutaniko lenu kuhusu utendaji fulani wa Kikristo, jaribu kuwa mwenye kujenga badala ya kuchambua-chambua. Hakikisha kwamba wewe mwenyewe unafanya kile ambacho unawatia moyo wengine wafanye. (Rom. 2:21, 22; Ebr. 13:7) Maneno yako yachochewe na upendo na wala si hasira. (2 Kor. 2:4) Ikiwa una hakika kwamba waamini wenzako wanataka kumpendeza Yehova, maneno yako yataonyesha uhakika huo, na watafaidika. Ona jinsi mtume Paulo alivyoonyesha uhakika kama huo katika 1 Wathesalonike 4:1-12; 2 Wathesalonike 3:4, 5; na Filemoni 4, 8-14, 21.

Nyakati nyingine inakuwa lazima wazee waonye dhidi ya mwenendo fulani usiofaa. Lakini unyenyekevu utawasaidia wazungumze na ndugu zao kwa roho ya upole. (Gal. 6:1) Jinsi wanavyozungumza ionyeshe kwamba wanaheshimu kutaniko. (1 Pet. 5:2, 3) Biblia inawashauri hasa wanaume vijana watambue jambo hilo. (1 Tim. 4:12; 5:1, 2; 1 Pet. 5:5) Tutegemee Biblia tunapohitaji kukaripia, kutia nidhamu, na kunyosha mambo. (2 Tim. 3:16) Msemaji asilazimishe kamwe au kupotoa Andiko fulani ili liunge mkono jambo ambalo huenda anashikilia sana. Hata kama kuna uhitaji wa shauri, tunaweza kuzungumza kwa njia yenye kutia moyo kwa kukazia hasa jinsi ya kuepuka mwenendo mbaya, kusuluhisha matatizo, kukabili magumu, kurekebisha mwenendo usiofaa, na jinsi matakwa ya Yehova yanavyotulinda.—Zab. 119:1, 9-16.

Unapotayarisha hotuba, fikiria kwa makini jinsi utakavyomalizia kila jambo kuu na jinsi utakavyomalizia hotuba yote. Jambo unalosema mwishowe ndilo hukumbukwa zaidi. Je, litatia moyo?

Unapozungumza na Waamini Wenzako. Watumishi wa Yehova huthamini nafasi za kushirikiana kwenye mikutano ya Kikristo. Hizo ni nyakati za kutiwa moyo kiroho. Biblia inatuhimiza tukumbuke “kutiana moyo” tunapokusanyika kwa ajili ya ibada. (Ebr. 10:25) Mbali na kutiana moyo kupitia hotuba na maelezo wakati wa mikutano, pia tunatiana moyo kwa mazungumzo yetu kabla na baada ya mikutano.

Ingawa ni kawaida kuzungumzia maisha yetu ya kila siku, tunatiwa moyo zaidi tunapozungumzia mambo ya kiroho. Hayo yanatia ndani mambo yaliyoonwa tunayopata katika utumishi wa shambani. Pia kupendezwa na wengine kwa njia inayofaa hujenga.

Kwa sababu ya uvutano wa ulimwengu ambao umetuzingira, tunahitaji kuwa waangalifu sana. Paulo alisema hivi alipowaandikia Wakristo kule Efeso: “Sasa kwa kuwa mmeweka mbali ukosefu wa lililo kweli, semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake.” (Efe. 4:25) Kusema kweli badala ya uwongo kunatia ndani kutotukuza vitu ambavyo watu wa ulimwengu huabudu. Vilevile, Yesu alionya kuhusu “nguvu za udanganyifu wa mali.” (Mt. 13:22) Basi, tunapozungumza na wengine, tunahitaji kuwa waangalifu tusiendeleze udanganyifu huo kwa kutukuza vitu vya kimwili.—1 Tim. 6:9, 10.

Mtume Paulo anapotushauri tuwe wenye kujenga, anatuhimiza tusimhukumu wala kumdharau ndugu ambaye anaweza kuepuka kufanya mambo fulani kwa sababu ya “udhaifu katika imani yake,” yaani, kwa sababu haelewi kabisa mipaka ya uhuru wa Kikristo. Kwa kweli, ili mazungumzo yetu yawe yenye kujenga, ni lazima tujue malezi ya wengine na kadiri ya ukuzi wao wa kiroho. Ingesikitisha kama nini ‘kuweka mbele ya ndugu [au dada] kipingamizi chenye kukwaza au sababu ya kukwaza’!—Rom. 14:1-4, 13, 19.

Wale ambao wanapambana na matatizo makubwa kama vile magonjwa ya kudumu, hufurahia mazungumzo yenye kujenga. Mtu kama huyo anaweza kujitahidi sana kuhudhuria mikutano. Wale wanaojua hali yake huenda wakamwuliza: “Unaendeleaje?” Bila shaka atathamini kwamba wanamjali. Lakini, labda jambo linalomtia moyo zaidi halihusu afya yake. Maneno ya uthamini na pongezi yanaweza kumchangamsha sana. Je, unaona kwamba bado anampenda Yehova na anavumilia magumu? Je, unatiwa moyo anapotoa maelezo? Unaweza kuwa mwenye kujenga zaidi ukikazia sifa zake nzuri na kufikiria jinsi anavyochangia hali nzuri kutanikoni badala ya kukazia mapungufu yake, sivyo?—1 The. 5:11.

Ili mazungumzo yetu yajenge, ni muhimu kufikiria maoni ya Yehova juu ya jambo mnalozungumzia. Katika Israeli la kale, Mungu aliwaadhibu vikali wale waliozungumza dhidi ya wawakilishi wa Yehova na kulalamika juu ya mana. (Hes. 12:1-16; 21:5, 6) Tunaonyesha kwamba mifano hiyo inatufaidi tunapowaheshimu wazee na kuthamini chakula cha kiroho kinachoandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.—1 Tim. 5:17.

Kuna mambo mengi sana yenye faida tunayoweza kuzungumza na ndugu zetu Wakristo. Lakini ikiwa mtu ni mchambuzi sana, chukua hatua ya kubadili mazungumzo yawe yenye kujenga.

Iwe tunahubiri, au tunatoa hotuba jukwaani, au tunazungumza na waamini wenzetu, tuwe wenye busara ili tutokeze moyoni mwetu “usemi wowote ule ulio mwema kwa ajili ya kujenga kama vile kuwezavyo kuwa na uhitaji, ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.”—Efe. 4:29.

JINSI YA KUFAULU

  • Kumbuka kwamba mgawo wetu ni kuhubiri habari njema.

  • Uwe mwenye kujenga badala ya kuchambua.

  • Sitawisha maoni mazuri juu ya wale ambao unazungumza nao.

  • Unapozungumza, fikiria jinsi usemi wako unavyoweza kuathiri mwingine.

MAZOEZI: Mtembelee mtu ambaye ni mlemavu au mgonjwa ambaye hawezi kutoka nyumbani. Anzisha mazungumzo yenye kujenga. Uwe mwenye huruma, lakini maneno yako yawe yenye kutia moyo. Jitayarishe mapema ili ufaulu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki