SOMO LA 35
Kurudia Ili Kukazia Mambo
UFUNDISHAJI bora hutia ndani kurudia mambo makuu. Jambo muhimu likitajwa zaidi ya mara moja, inaelekea wahudhuriaji watalikumbuka. Jambo hilo likirudiwa kwa njia tofauti kidogo, wanaweza kulielewa vizuri zaidi.
Ikiwa wasikilizaji hawatakumbuka mambo unayosema, maoni yao na maisha yao hayatabadilika. Labda wataendelea kufikiria mambo ambayo unakazia kwa njia ya pekee.
Mwalimu wetu Mkuu Zaidi, Yehova, anatuwekea mfano mzuri wa kukazia jambo kwa kulirudia. Alilipatia taifa la Israeli Amri Kumi. Kupitia malaika aliyekuwa msemaji, taifa hilo lilisikia amri hizo kwenye Mlima Sinai. Baadaye aliandika amri hizo na kumpa Musa. (Kut. 20:1-17; 31:18; Kum. 5:22) Musa alifuata mwongozo wa Yehova akalitajia tena taifa hilo amri hizo kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, na kupitia roho takatifu, aliziandika katika Kumbukumbu la Torati 5:6-21. Miongoni mwa sheria ambazo Waisraeli walipewa, waliagizwa wampende Yehova na kumtumikia kwa moyo wao wote, nafsi yao yote, na nguvu zao zote. Jambo hilo lilirudiwa tena na tena. (Kum. 6:5; 10:12; 11:13; 30:6) Kwa nini? Kama Yesu alivyosema, ni kwa sababu sheria hiyo ni “amri kubwa zaidi sana na ya kwanza.” (Mt. 22:34-38) Yehova alimtumia nabii Yeremia kuwakumbusha watu wa Yuda zaidi ya mara 20 kuhusu umuhimu wa kutii mambo yote aliyowaamuru. (Yer. 7:23; 11:4; 12:17; 19:15) Na Mungu alimtumia Ezekieli kutaja zaidi ya mara 60 kwamba mataifa ‘watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA.’—Eze. 6:10; 38:23.
Maandiko yanayohusu huduma ya Yesu pia yanarudia-rudia maneno fulani kwa mkazo. Kwa mfano, kuna vitabu vinne vya Injili, na kila kitabu kinazungumzia kwa njia tofauti kidogo matukio muhimu ambayo yanatajwa katika kitabu kingine au vitabu vingine vya Injili. Yesu mwenyewe alipokuwa akifundisha, alikuwa akirudia kutaja jambo kuu zaidi ya mara moja na kwa njia tofauti-tofauti. (Mk. 9:34-37; 10:35-45; Yn. 13:2-17) Na Yesu alirudia kukazia shauri muhimu kwenye Mlima wa Mizeituni siku chache kabla ya kifo chake: “Fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja.”—Mt. 24:42; 25:13.
Katika Huduma ya Shambani. Unapohubiria watu, unatumaini kwamba watakumbuka mambo unayosema. Kurudia mambo makuu kwa njia nzuri kunaweza kuwakumbusha mambo hayo.
Kurudia jambo wakati linapozungumzwa hufanya libaki akilini. Basi, baada ya kusoma andiko, unaweza kulikazia kwa kuonyesha sehemu fulani ya andiko hilo na kuuliza, “Je, umeona maneno ambayo yametumiwa hapa?”
Pia unaweza kutumia vizuri maneno ya kumalizia mazungumzo. Kwa mfano, unaweza kusema: “Jambo kuu ambalo natumaini utakumbuka katika mazungumzo yetu ni . . . ” Kisha rudia kutaja jambo hilo kwa njia rahisi. Unaweza kusema hivi: “Kusudi la Mungu ni kuigeuza dunia kuwa paradiso. Kusudi hilo litatimizwa hakika.” Au labda: “Biblia inaonyesha wazi kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Ili tusiangamizwe, ni lazima tujifunze matakwa ya Mungu.” Au tunaweza kusema: “Kama tulivyoona, Biblia ina mashauri mazuri yanayotusaidia kushughulikia matatizo ya familia.” Nyakati nyingine unaweza tu kurudia kunukuu andiko la Biblia ili alikumbuke. Ili ufaulu, unahitaji kufikiri kwanza.
Unapofanya ziara za kurudia au unapoongoza mafunzo ya Biblia, unaweza kurudia mambo makuu kwa kuuliza maswali ya pitio.
Mtu anaposhindwa kuelewa shauri la Biblia au kulifuata, unaweza kuzungumzia jambo hilo zaidi ya mara moja. Jaribu njia kadhaa. Si lazima mazungumzo hayo yawe marefu lakini yanapaswa kumtia moyo mwanafunzi aendelee kulifikiria. Kumbuka kwamba Yesu alitumia mbinu hiyo alipokuwa akiwasaidia wanafunzi wake wasiwe na tamaa ya umashuhuri.—Mt. 18:1-6; 20:20-28; Luka 22:24-27.
Unapotoa Hotuba. Unapotoa hotuba jukwaani, lengo lako lisiwe tu kuzungumza. Unataka wasikilizaji waielewe, waikumbuke, na kuitumia maishani. Ili ufaulu, rudia mambo makuu kwa njia nzuri.
Lakini ukirudia kutaja mambo makuu kupita kiasi, wasikilizaji watachoka kukusikiliza. Chagua kwa makini mambo yanayopaswa kukaziwa kwa njia ya pekee. Mara nyingi hayo ni mambo makuu ya hotuba yako, lakini pia yanaweza kutia ndani mambo ambayo yatawafaidi sana wasikilizaji.
Ili urudie vizuri mambo makuu, kwanza unaweza kuyataja kwenye utangulizi. Yataje kwa sentensi fupi-fupi ambazo zinaonyesha kwa ujumla mambo ambayo utazungumzia, au kwa maswali, au kwa mifano mifupi inayoonyesha mambo mtakayozungumzia. Unaweza kutaja idadi ya mambo unayotaka kuzungumzia na kuyaorodhesha. Kisha fafanua kila moja ya mambo hayo katika hotuba yako. Unaweza kutia mkazo kwenye sehemu kuu ya hotuba kwa kutaja tena kila jambo kuu kabla ya kuzungumzia jingine. Au unaweza kutumia mfano unaoonyesha jinsi ya kutumia jambo hilo maishani. Pia unaweza kukazia mambo makuu kwa kutumia umalizio unaorudia kuyataja, au unaoonyesha tofauti iliyoko kati ya mambo hayo makuu na mambo mengine, au unaojibu maswali yaliyozushwa, au unaotaja kifupi suluhisho la mambo ambayo ulizungumzia.
Mbali na mambo hayo ambayo tumetaja, msemaji mwenye uzoefu huwaangalia wasikilizaji kwa makini. Ikiwa baadhi yao hawaelewi vizuri jambo fulani, msemaji atatambua. Ikiwa ni jambo muhimu, analitaja tena. Lakini, labda haifai kurudia tu maneno yaleyale. Kufundisha kunatia ndani mambo mengine pia. Ni lazima msemaji awe mwenye kubadilikana. Huenda akahitaji kuongeza mambo mengine kwenye hotuba yake akiwa jukwaani. Kujifunza kubadilikana kulingana na mahitaji ya wasikilizaji kunaonyesha jinsi ulivyo mwalimu bora.