‘Twalihubiri Neno’
1 Kupatana na ufafanuzi wa Biblia wa “siku za mwisho,” watu walio wengi leo ni wa “namna ya ujitoaji-kimungu” tu. (2 Tim. 3:1, 5, NW) Hii ni kwa sababu viongozi wa kidini wameshindwa kutoa mwongozo wa kweli kwa makundi yao. Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo hawafundishi Biblia. Wanapendelea kurudia-rudia mafundisho ya bure ya wanafalsafa na wanatheolojia au kuzungumza masuala ya kijamii na kisiasa badala ya kuhubiri Neno la Mungu. Viongozi wengi wa kidini hawaamini Biblia. Wao huhisi kwamba hiyo si ya kisasa, nao kwa kupotosha hutetea nadharia ya mageuzi badala ya mafundisho ya Biblia kuhusu Muumba Mtukufu. Makasisi walio wengi hata hawatumii jina la Mungu la kibinafsi, na hawapingi linapoondolewa kwenye tafsiri za Biblia za kisasa.
2 Kama ilivyokuwa na viongozi wa kidini katika siku ya Yesu, leo makasisi wanahubiri bure. (Mt. 15:8, 9) Ni kama vile tu nabii Amosi alivyotabiri. Kuna “[njaa] si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya BWANA.” (Amo. 8:11) Zaidi ya yote, watu wanahitaji chakula cha kiroho cha Neno la Mungu.
3 Jinsi ya Kutosheleza Uhitaji wa Kiroho wa Watu: Paulo alimhimiza sana Timotheo akae katika ‘maandiko matakatifu, ambayo yaweza kumhekimisha [mtu] hata apate wokovu,’ kwa hiyo alimwagiza kwa uzito ‘kuhubiri neno’ kwa wengine. (2 Tim. 3:14, 15; 4:2) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, lazima tukae katika yale ambayo Biblia hufundisha tunapohubiri, kwa njia hiyo tukiiga Kielelezo chetu, Yesu, ambaye alisema: “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.” (Yn. 7:16) Twatumia Neno la Mungu kuwa msingi wa mafundisho yetu kwa sababu twatambua kwamba lina hekima ya kimungu, na twataka watu wajue chanzo cha habari tunayoishiriki nao.—1 Kor. 2:4-7.
4 Lazima kwanza watu waisikie kweli kutoka Biblia ili wajifunze juu ya Yehova, wamwamini. Paulo aliandika kiakili hivi: “Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri?” (Rum. 10:14) Kwa kuhubiri Neno la Mungu, twasaidia wengine wapate imani kupitia ujuzi sahihi. Ujuzi huo waweza kubadili nao hubadili maisha yawe mazuri zaidi. Mwandikaji Mwingereza Charles Dickens aliandika hivi kuhusu Biblia: “Ndicho kitabu kizuri zaidi kilichopata kuwamo na kitakachopata kuwamo ulimwenguni, kwa sababu hicho hukufundisha masomo bora zaidi ambayo kiumbe yeyote wa kibinadamu anayejaribu kuwa wa kweli na mwaminifu aweza kuongozwa nayo.”
5 Wale wanaoona njaa ya kweli ya kiroho huja kutambua kwamba inategemezwa na mamlaka ya Neno la Mungu. Huko nyuma katika 1913, Frederick W. Franz, akiwa mwanafunzi mchanga wa chuo, alipewa kijitabu chenye kichwa Where Are the Dead? Baada ya kusoma jibu la Biblia kwa swali hili akiwa na upendezi mkubwa, alitangaza hivi: “Hii ndiyo kweli.” Mamilioni ya watafutaji kweli wamekuja kuhisi vivyo hivyo. Acheni twendelee kuhubiri Neno kwa bidii nyendelevu na juhudi na hivyo tushiriki shangwe ya kusikia wengine wakisema: “Hii ndiyo kweli.”