Sanduku La Swali
◼ Ni nini kinachopaswa kufanywa msiba utokeapo unaoathiri ndugu zetu moja kwa moja?
Msiba Utokeapo Sehemu Yenu: Usiwe na hofu ya ghafula. Tulia, ukazie fikira yaliyo ya thamani, yaani uhai, si mali. Angalia mahitaji ya kimwili ya wakati huo ya familia yako. Kisha ujulishe wazee kuhusu hali zako na mahali uliko.
Wazee na watumishi wa huduma huwa na fungu la maana katika kuandaa usaidizi wa kitulizo. Onyo la mapema la msiba litolewapo, kama ilivyo na vimbunga fulani vikubwa, ndugu hawa wanapaswa kuhakikisha kwamba kila mtu yuko mahali salama, na wakati ukiruhusu, wanapaswa kupata na kugawanya vitu ambavyo huenda vikahitajiwa.
Baadaye, viongozi wa mafunzo ya kitabu wanapaswa kutafuta na kujua hali yao. Mwangalizi-msimamizi au mzee mwingine apaswa kujulishwa kuhusu hali ya kila familia, hata ingawa mambo yote yako sawa. Ikiwa mtu ameumizwa, wazee watajaribu kupanga kwa ajili ya matibabu. Pia wataandaa vitu vyovyote vya kimwili kama vile chakula, mavazi, makao, au vyombo vya nyumbani ambavyo vyahitajiwa. (Yn. 13:35; Gal. 6:10) Wazee wa kwenu watatoa tegemezo la kiroho na la kihisia-moyo kwa kutaniko na watapanga haraka iwezekanavyo kuanza tena mikutano ya kutaniko. Baada ya kadirio kamili kufanywa, mzee apaswa kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko kwa niaba ya baraza la wazee amwarifu kuhusu majeraha yoyote, kuharibiwa kwa Jumba la Ufalme, au kuharibiwa kwa makao ya akina ndugu, na vilevile kuhusu mahitaji ya pekee yoyote. Ndipo mwangalizi wa mzunguko atakapopigia simu ofisi ya tawi akiwa na ripoti ya hiyo hali. Ofisi ya tawi itaratibu hatua kubwa za kitulizo zinazohitajiwa.
Msiba Ukitokea Kwingine: Kumbuka akina ndugu na dada katika sala zako. (2 Kor. 1:8-11) Ukitaka kutoa msaada wa kifedha, unaweza kutuma michango yako kwa Sosaiti, ambako fedha za kitulizo huwekwa kando kwa kusudi hili. Anwani ni: I.B.S.A., Box 47788, Nairobi. (Mdo. 2:44, 45; 1 Kor. 16:1-3; 2 Kor. 9:5-7; ona Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 1985 kurasa 20-22, la Kiingereza.) Usipeleke vitu au vifaa mahali penye msiba isipokuwa uombwe hususani na akina ndugu wenye kushughulika. Jambo hili litahakikisha kuwako kwa jitihada ya kitulizo yenye utaratibu na ugawanyaji mzuri wa vitu. (1 Kor. 14:40) Tafadhali usipigie simu Sosaiti isivyo lazima, kwa kuwa hili laweza kufunga njia za simu zinazohitajiwa kushughulikia simu zinazokuja kutoka eneo la msiba.
Baada ya ukaguzi mzuri kufanywa, Sosaiti itaamua kama halmashauri ya kitulizo itafanyizwa. Ndugu wenye madaraka watajulishwa. Wote wanapaswa kushirikiana na wazee wanaoongoza ili mahitaji ya maana ya akina ndugu yatimizwe vya kutosha.—Ona Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom, kurasa 310-315.