Wazazi—Zoezeni Watoto Wenu Kuhubiri
1 Makutaniko yetu yamebarikiwa kuwa na watoto wengi wenye tamaa ya moyo mweupe ya kumtumikia Mungu. (Mhu. 12:1) Wanatiwa ndani miongoni mwa wale ambao Yehova amealika kushiriki katika kumsifu yeye. (Zab. 148:12-14) Kwa sababu hiyo, mazoezi ya siku kwa siku ambayo wazazi huwapa watoto wao yapaswa kutia ndani maagizo ya jinsi ya kushiriki imani yao na wengine katika kazi ya kuhubiri Ufalme.—Kum. 6:6, 7.
2 Zoeza Watoto kwa Hatua Zenye Kuendelea: Watoto wanastahili kuzoezwa wakiwa na umri mchanga zaidi waandamane na wazazi wao katika huduma. Kabla ya kwenda katika utumishi, tayarisha watoto wako kushiriki katika njia ifaayo. Amua mapema jambo unalowatazamia wafanye mlangoni. Watoto wachanga zaidi wanaweza kutoa trakti na vikaratasi vya kukaribisha watu na kualika watu kwenye Jumba la Ufalme. Wachanga wanaosoma vizuri wanaweza kualikwa wasome maandiko mlangoni. Wanaweza kutoa magazeti, wakitumia utoaji mfupi. Wanapopata uzoefu, wazoezeni kutumia Biblia katika utoaji wao. Watangazaji wengi wachanga walianzisha njia ya kupelekea watu magazeti kwa ukawaida na wanafanya ziara za kurudia kwa ukawaida. Ni vema mtoto akihubiri pamoja na mtu mzima badala ya kijana mwingine. Mtu mzima anaweza kumweleza mwenye nyumba kwamba kijana anazoezwa katika huduma.
3 Msichana mmoja mdogo aliomba wazee msaada ili aweze kustahili kuwa mtangazaji wa Ufalme. Hata ingawa alikuwa na umri wa miaka mitano tu wakati huo na hakujua jinsi ya kusoma, angeweza kutoa ujumbe wa Ufalme kwa matokeo milangoni. Alikariri mahali ambapo maandiko yalipatikana, akayafungua, akamwomba mwenye nyumba ayasome, kisha akayafafanua.
4 Watoto pia wapasa kufundishwa kwa kielelezo cha mzazi uthamini wa kuwa na ratiba nzuri ya kushiriki kwa ukawaida katika huduma. Wazazi wanahitaji kuweka imara kawaida thabiti ya kila juma kwa ajili ya utumishi na kuifuata kwa uaminifu, ili kwamba watoto wajue ni sehemu gani ya juma ambayo sikuzote huwekwa kando kwa ajili ya kazi ya kuhubiri.
5 Watoto wazoezwapo wakiwa wachanga kupenda na kufurahia huduma, watachochewa kufikia mapendeleo makubwa zaidi wakati ujao, labda kutia ndani utumishi wa painia. (1 Kor. 15:58) Sisi sote twapaswa kutia moyo watoto walio miongoni mwetu kufanya maendeleo mazuri wakiwa wasifaji wa Yehova.