“Dhihirisheni Subira”
1 Tuonapo mwisho wa mfumo wa kale wa Shetani ukikaribia kuliko wakati wowote, ni muhimu ‘tudhihirishe subira’ tungojapo siku ya Yehova ya ukombozi. Hasa kwenye wakati huu uliosonga sana, majeshi maovu ya adui yameazimia kukengeusha fikira zetu kutoka kwa suala kuu la enzi kuu ya Yehova na kutushawishi tukengeushwe na mambo mengi zaidi ya kibinafsi. Kwa njia hiyo, Shetani anaweza kutudanganya kwa werevu tukate tamaa au tupunguze mwendo katika kazi ya kuhubiri Ufalme. (Yak. 5:7, 8; Mt. 24:13, 14) Twaweza kudhihirisha subira hiyo inayohitajiwa katika njia gani?
2 Kwa Kuwa na Uvumilivu: Tunapokabili ubaridi au upinzani katika huduma yetu, uvumilivu waweza kutusaidia tuvumilie tunapohubiri. Hatutatishwa au kuudhika kwa urahisi watu tunaokutana nao wanapokuwa wakali au wasio na fadhili. (1 Pet. 2:23) Nguvu hiyo ya ndani yaweza kutuzuia kusema isivyofaa kuhusu watu katika eneo letu ambao wanaonyesha ubaridi au uhasama kuelekea kazi yetu, tukitambua kwamba mazungumzo hayo yatatuvunja moyo na wale tunaohubiri nao katika huduma.
3 Kwa Subira Yenye Kuendelea: Baada ya mazungumzo mazuri katika utumishi wa shambani, subira yetu yaweza kujaribiwa tunapomkosa tena nyumbani mtu mwenye kupendezwa. Yaweza kuwa hivyo ikiwa wale tunaojifunza nao hawafanyi maendeleo haraka au kuchukua msimamo kwa ajili ya kweli. Hata hivyo, subira yenye kuendelea mara nyingi huthawabishwa kwa matokeo mazuri. (Gal. 6:9) Dada mmoja alifanya ziara kadhaa za kurudia kwa mwanamke mchanga kabla ya kuanzisha funzo la Biblia. Katika ziara tano za kwanza, mwanamke huyo alikuwa na shughuli nyingine. Alipojaribu mara ya sita, dada huyo alilowa chepechepe katika mvua ya radi, na kumkosa mtu nyumbani. Hata hivyo, akiazimia kumpa mwanamke huyo nafasi nyingine zaidi, dada huyo alirudi tena na kumpata mwanamke huyo akiwa tayari kujifunza. Baada ya hapo, mwanafunzi huyo alifanya maendeleo mazuri na kwa muda mfupi akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova.
4 Twajua kwamba siku ya Yehova haitakawia. Kwa hiyo twangoja atekeleze mambo yake, tukijua kwamba subira ya Mungu itatokeza matokeo mazuri. (Hab. 2:3; 2 Pet. 3:9-15) Lazima tudhihirishe subira kama Yehova afanyavyo na tusiiache huduma. “Kupitia imani na subira,” mtegemee Yehova akuthawabishe kwa kazi yako ngumu.—Ebr. 6:10-12.