Tunapaswa Kuwa Wenye Subira Katika Huduma
1. Yehova amewatendea wanadamu kwa subira jinsi gani?
1 Sikuzote Mungu amewatendea wanadamu kwa subira. (Kut. 34:6; Zab. 106:41-45; 2 Pet. 3:9) Kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani kote inadhihirisha upendo na subira ya Yehova Mungu. Yehova amewasaidia wanadamu kwa subira kwa karibu miaka 2,000, na bado anaendelea kuwavuta watu wanaotaka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Yoh. 6:44) Tunaweza kuonyesha subira kama ya Yehova katika huduma yetu jinsi gani?
2. Tunaweza kuonyesha subira jinsi gani tunapohubiri katika eneo letu?
2 Utumishi wa Nyumba kwa Nyumba: Tunaiga subira ya Yehova kwa kuendelea kuhubiri “bila kuacha” katika eneo ambako watu hawajaanza bado kupendezwa na ujumbe wetu. (Mdo. 5:42) Kwa subira, tunaendelea na utumishi wetu licha ya dhihaka, upinzani, na watu wasiopendezwa. (Marko 13:12, 13) Tunaonyesha subira pia tunapojitahidi bila kuacha kuzitia maji mbegu za kweli, hata wakati ambapo ni vigumu kuwapata tena watu waliopendezwa.
3. Kwa nini subira inahitajika tunapofanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia?
3 Mafunzo ya Biblia: Baada ya kupanda mmea tunahitaji subira. Tunaweza kutunza mmea tuliopanda lakini hatuwezi kuharakisha ukuaji. (Yak. 5:7) Hali kadhalika, mtu anakua kiroho polepole na hatua kwa hatua. (Marko 4:28) Huenda wanafunzi wetu wa Biblia wanaona vigumu kuacha mafundisho ya dini za uwongo au mila zisizopatana na Maandiko. Hatupaswi kujaribu kuwakaza wanafunzi wetu wafanye mabadiliko ili kuharakisha ukuaji wa kiroho. Subira inahitajika ili kuruhusu muda wa kutosha kwa roho ya Mungu kufanya kazi katika moyo wa mwanafunzi.—1 Kor. 3:6, 7.
4. Subira itatusaidiaje kuwahubiria kwa njia inayofaa watu wetu wa ukoo wasio waamini?
4 Watu wa Ukoo Wasio Waamini: Ijapokuwa tunatamani sana watu wetu wa ukoo wakubali kweli, tunasubiri wakati unaofaa wa kuwaeleza kuhusu imani yetu, na kwa busara tunaepuka kuwaeleza mambo mengi mno. (Mhu. 3:1, 7) Matendo yetu yanaonyesha manufaa za kweli za Biblia tunapongoja wakati unaofaa wa kuwahubiria, huku tukiwa tayari kuwaeleza kuhusu imani yetu kwa upole na heshima. (1 Pet. 3:1, 15) Bila shaka, tukiwa wenye subira, tutafanikiwa zaidi katika huduma yetu na tutampendeza Baba yetu wa mbinguni.