‘Vaeni Utu Mpya’
1 Wakristo wanathamini kuijua kweli! Tumejifunza jinsi ya kuishi ili kuepuka mwendo wa walimwengu. Wakiwa ‘wamefanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu,’ wamo “katika giza kiakili.” (Efe. 4:18) Tumefundishwa kufanyiza upya akili zetu mbali na kufikiri kilimwengu kwa kuuvua utu wa zamani na kuvaa ule mpya.—Efe. 4:22-24.
2 Utu wa zamani huongoza kwenye mwendo wenye kuendelea ulioshuka kiadili, ukitokeza unajisi na kifo. Kwa hiyo, twawaomba wale ambao watasikiliza ujumbe wa Ufalme waweke mbali hasira ya kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu. Wale wanaotamani kibali cha Mungu wanapaswa kuazimia kabisa kuweka mbali utu wa zamani—kwa njia ambayo wangevua vazi chafu.—Kol. 3:8, 9.
3 Kani Mpya Inayotendesha Akili: Kuvaa utu mpya hutia ndani kufanywa upya katika kani inayotendesha akili zetu. (Efe. 4:23) Mtu hufanyaje upya kani hiyo, au mwelekeo wa akili, ili uelekee mahali panapofaa? Ni kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutafakari kile ambacho humaanisha. Kisha, njia mpya ya kufikiri hutokea, na mtu huona mambo kulingana na maoni ya Mungu na ya Kristo. Maisha ya mtu hugeuzwa anapovaa sifa kama za Kristo, kutia ndani, huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, ustahimilivu, na upendo.—Kol. 3:10, 12-14.
4 Kwa kujivika utu mpya, twajitenga na ulimwengu. Njia yetu ya maisha hutufanya tuwe tofauti. Twasema kweli na kutumia usemi unaofaa kujenga wengine. Twadhibiti hasira yetu, uchungu, kupiga kelele, usemi wenye kuudhi, na ubaya wote na badala yake kuwa na uadilifu, na sifa za kimungu. Twafanya zaidi ya yale tunayohitajiwa kwa kuwa wenye kusamehe. Yote hayo yanafanywa kwa nia kutoka moyoni.—Efe. 4:25-32.
5 Usiuvue utu mpya kamwe. Hatuwezi kumtumikia Yehova kwa kukubalika bila huo. Uruhusu ukusaidie kuvutia watu katika kweli, na uruhusu umtukuze Yehova, Muumba wa utu wetu mpya mzuri ajabu.—Efe. 4:24.