Je, Wewe Huona Tu Sura ya Nje?
1 Tufanyapo huduma yetu ya hadharani, maoni tuliyo nayo kwanza kuhusu watu fulani huenda yakatufanya tusite kuwaeleza habari njema. Kwa mfano, ungeitikiaje kama mtu mwenye kutisha sikuzote angekutazama kwa macho yenye kutilia shaka ulipoenda kuhubiria jirani zake ambao walionyesha kupendezwa na kweli? Dada painia aliyejionea hilo aliamua kumfikia mwanamume huyo na kuongea naye. Mwanamume huyo alimsalimia kwa ukali. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba, alisikiliza ujumbe wa Biblia na kwa msisimko akakubali kujifunza. Kwa sababu dada huyo hakuhukumu kwa sura za nje, njia ilifunguliwa kwa mwanamume huyo na mke wake kujifunza kweli.
2 Dada mwingine mwanzoni aliogopeshwa na sura ya nje ya mwanamume mmoja mwenye nywele ndefu lakini akaendelea kumhubiria kifupi alipokuwa akija kwenye duka alimofanyia kazi. Jitihada zake zilitokeza matokeo mazuri na mwanamume huyo mchanga sasa ni Shahidi aliyebatizwa. Ni nini kitakachotuzuia kuamua upesi kwamba watu kama hao hawataitikia?
3 Kuiga Kielelezo cha Yesu: Yesu alijua kwamba angetoa uhai wake kwa kila mtu. Kwa sababu hiyo, hakuvunjwa moyo na sura ya nje ya wengine. Alitambua kwamba hata wale walio na tabia za kuchukiza huenda wakawa tayari kubadilika wakipewa msaada ufaao na kichocheo. (Mt. 9:9-13) Alijaribu kusaidia matajiri na maskini pia. (Mt. 11:5; Mr. 10:17-22) Tusihukumu watu tunaowakuta katika huduma kwa sura yao ya nje, tukikosa kuona ile inayoweza kuwa hali nzuri ya moyo. (Mt. 7:1; Yn. 7:24) Ni nini kinachoweza kutusaidia tuige kielelezo cha Yesu chenye kutokeza?
4 Kupitia funzo letu la Biblia, tumepata kujua kwamba Neno la Mungu lina nguvu ya kubadili kufikiri, mwenendo, na utu wa mtu. (Efe. 4:22-24; Ebr. 4:12) Kwa hiyo, twapaswa kuendelea kuwa na mtazamo ufaao na kumwachia Yehova yote, kwa kuwa Yeye ndiye asomaye mioyo ya binadamu.—1 Sam. 16:7; Mdo. 10:34, 35.
5 Kushiriki kwetu habari njema na watu wa aina zote bila kupendelea wala kujali sura yao ya nje, na kuchangie mengi zaidi katika kazi ya mavuno katika hizi siku za mwisho.—1 Tim. 2:3, 4.