Wazazi—Wekeeni Watoto Wenu Kielelezo Chema
1 Neno la Mungu hutuambia kwamba “Baba [na mama] yake mwenye haki atashangilia.” (Mit. 23:24, 25) Hiyo ni baraka kama nini kwa wazazi ambao wameweka kielelezo chema kwa wazao wao! Mshiriki mmoja wa Halmashauri ya Tawi alisema hivi kuhusu wazazi wake: “Maisha yao yote yaliitegemea ile kweli, nami nilitaka maisha yangu yote yaitegemee pia.” Watoto wanapaswa kuona nini kwa wazazi wao?
2 Adabu na Staha Yenye Kina Kirefu: Ni daraka la wazazi kutia ndani ya watoto wao tabia zenye kujenga. Mtu hujifunza adabu, si kwa mafundisho ya mdomo tu, bali kwa kutazama na kuiga. Kwa hiyo, wewe huonyesha adabu za aina gani? Je, watoto wako hukusikia ukisema “kunradhi,” “tafadhali,” na “asante”? Katika familia, je, nyinyi hutendeana kwa staha yenye kina kirefu? Je, wewe husikiliza wengine wasemapo? Je, wewe husikiliza watoto waongeapo nawe? Je, tabia hizo nzuri zaonyeshwa kwenye Jumba la Ufalme na nyumbani kwenu?
3 Hali ya Kiroho Yenye Nguvu na Utendaji Wenye Bidii: Ndugu mmoja ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 50 akumbuka hivi: “Mama na baba yangu walikuwa kielelezo bora katika kuthamini mikutano na katika bidii yao kwa ajili ya huduma.” Wewe waonyeshaje watoto wako kwamba unajali kudumisha hali ya kiroho ya watu wa nyumbani mwako? Je, nyinyi huchunguza andiko la kila siku pamoja? Je, mna funzo la familia la kawaida? Je, watoto wako wanakuona ukisoma Biblia na vichapo vya Sosaiti? Wao husikia nini unaposali kwa niaba ya familia? Je, wewe hushiriki katika mazungumzo ya kiroho yajengayo pamoja na watoto wako, mkizungumzia mambo yafaayo kuhusu kweli na kutaniko? Je, una hamu ya kuhudhuria mikutano yote na kushiriki katika huduma ya shambani mkiwa familia?
4 Wazazi, fikirieni kielelezo mnachowekea watoto wenu. Wekeni kielelezo bora kabisa, nao watakithamini katika maisha yao yote. Mke wa mwangalizi asafiriye, ambaye sasa ana umri wa miaka 70 na kitu, alisema hivi: “Ningali nanufaika na kielelezo chema cha wazazi wangu wapendwa Wakristo. Nami nasali kwa bidii kwamba nithibitishe kwamba nathamini kikamili urithi huo kwa kuutumia vizuri katika miaka yote inayokuja.”