Je, Wahubiri Ukiwa na Kusudi?
1 Yehova ni Mungu wa kusudi. (Isa. 55:10, 11) Twasihiwa tumwige. (Efe. 5:1) Hakika hilo lapaswa kuonekana katika njia tunayotimiza huduma yetu. Kwa hiyo swali hili lafaa: “Je, wahubiri ukiwa na kusudi?”
2 Kuhubiri kwako mlango hadi mlango, ukitoa ushahidi wa vivi hivi, na kugawanya fasihi ni sehemu ya huduma yenye kusudi. Lakini kumbuka kwamba utume wetu hautii ndani kuhubiri tu bali pia kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Baada ya kupanda mbegu za kweli ya Ufalme, twahitaji kurudi ili kuzimwagia maji na kuzitunza kwa ukawaida tunapomtegemea Yehova alete ongezeko. (1 Kor. 3:6) Twahitaji kuhangaikia kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia.
3 Panua Huduma Yako: Mara nyingi unahisi vizuri unapoweza kukumbuka uliyofanya wakati uliopita katika utumishi na kujiambia: “Nilitimiza yale niliyokuwa nimeazimia kufanya.” Kama ilivyorekodiwa kwenye 2 Timotheo 4:5, Paulo alisihi hivi: “Timiza kikamili huduma yako.” Hiyo yatia ndani kuongeza jitihada zako za kufuatia watu wote wenye kupendezwa waliopatikana. Katika ratiba yako ya utumishi ya kila juma, panga wakati hususa wa kufanya ziara za kurudia. Jitahidi kufikia mradi wa kuanzisha mafunzo ya Biblia na wale wenye mwelekeo wa uadilifu. Hilo lapasa kuwa kusudi lako unaposhiriki katika huduma.
4 Uliza wahubiri jinsi walivyohisi walipoona wanafunzi wao wa Biblia wakibatizwa kwenye kusanyiko. Walishangilia, labda kama wale waliobatizwa. Walikuwa wametimiza kusudi kuu! Mmoja ambaye hufanya wanafunzi alieleza hivi: “Kufanya wanafunzi huleta wasifaji zaidi wa Yehova. Huletea wale wanaoikubali kweli uhai. Napenda kuwafundisha wengine kweli, ni jambo lenye kupendeza sana! . . . Wengi kati ya wale ambao wamekuja kumpenda Yehova wamekuwa rafiki zangu wa karibu sana.”
5 Ebu wazia kumsaidia mtu awe mtumishi aliyejiweka wakfu kwa Yehova! Hiyo ni sababu yenye shangwe kama nini! Matokeo hayo hutokana na kuhubiri ukiwa na kusudi katika huduma.—Kol. 4:17.