“Wanawake Wanaofanya Kazi kwa Bidii Katika Bwana”
1 Kwa maneno yaliyo juu, Paulo alifafanua Trifaina na Trifosa, dada wawili wenye bidii katika kutaniko la Roma. Kuhusu mwingine aitwaye Persisi, alisema hivi: “Mwanamke huyo alifanya kazi nyingi za jasho katika Bwana.” Vilevile alimtaja vizuri Fibi kuwa “mtetezi wa wengi.” (Rom. 16:2, 12) Katika Maandiko, Dorkasi anatajwa kuwa “alizidi katika vitendo vyema na zawadi za rehema alizokuwa akitoa.” (Mdo. 9:36) Wanawake wa kiroho ni baraka iliyoje katika kutaniko!
2 Je, twathamini akina dada wanaofanya kazi kwa bidii katika kutaniko letu? Wao hushiriki fungu kubwa zaidi katika kazi ya kuhubiri, wanaongoza mafunzo zaidi ya Biblia, na kusaidia wapya wengi. Pia wao hutumia wakati mwingi kusaidia watoto wafanye maendeleo ya kiroho. Wanawake Wakristo hufanya sehemu yao katika kujenga roho ya upendo, shangwe, amani, na bidii katika kutaniko. Wao huunga mkono katika njia nyingi ili waume zao na washiriki wa familia zao waweze kufanya mengi katika utumishi wa Yehova.
3 Akina Dada Katika Utumishi wa Wakati Wote: Miongoni mwa wale wenye kufanya kazi ya jasho kwa bidii katika Bwana ni dada wamishonari, wengi wameshiriki katika kuanzisha kazi katika nchi za kigeni. Katika makutaniko yanayotumikiwa na waume zao, wake wa waangalizi wasafirio ni wenye shughuli katika huduma ya shambani, wakiwatia moyo dada wengi. Wasiopasa kusahauliwa ni akina dada wa Betheli, ambao kwa bidii hutoa utumishi mtakatifu katika kutegemeza tengenezo la Yehova. Na dada zetu mapainia wa kawaida, kwa jitihada zao za uaminifu katika kumtukuza Mungu, wanasaidia maelfu wajifunze kweli.
4 Wanawake hawa waaminifu hupata uradhi mwingi katika njia yao ya maisha ya kujinyima. (1 Tim. 6:6, 8) Wanastahili pongezi na kitia-moyo chochote na tegemezo tunaloweza kuwapa.
5 Wanawake Wakristo ni wenye thamani sana kwa tengenezo la Yehova, wakitoa utumishi mwaminifu ambao ni baraka kwa wote. Na twendelee kuthamini wanawake hao na kusali baraka za Yehova ziwe pamoja nao waendeleapo “kufanya kazi kwa bidii katika Bwana.”