Ni Nini Kinachoweza Kutusaidia Tusimame Imara Katika Imani?
1 Tangu tuanze kushirikiana na tengenezo la Yehova, maendeleo yetu ya kiroho yamethibitika kuwa chanzo cha shangwe yetu! Hata hivyo, ili kuendelea ‘kutiwa mizizi na kujengwa, na kuimarishwa katika imani,’ ukuzi wenye kuendelea wa kiroho ni wa lazima. (Kol. 2:6, 7) Ijapokuwa walio wengi zaidi wamesitawi kiroho, wengine wamepeperushwa mbali kwa sababu ya kukosa ‘kusimama imara katika imani.’ (1 Kor. 16:13) Twaweza kuzuia jambo hilo lisitupate. Jinsi gani?
2 Utendaji wa Kiroho wa Daima: Weka kawaida nzuri ya mambo ya kiroho katika tengenezo la Yehova. Hapo ndipo mahitaji yetu ya kiroho yanapotunzwa kwa wingi. Mikutano ya kutaniko, makusanyiko na mikusanyiko hutuchochea kwenye ukuzi mkubwa zaidi wa kiroho na hali ya kiroho yenye nguvu, maadamu twahudhuria kwa ukawaida ili kupata manufaa. (Ebr. 10:24, 25) Utaratibu wa kawaida wa kusoma Biblia, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na vitabu ambavyo huzungumzia chakula kigumu cha Neno la Mungu utafanya mizizi yetu ya kiroho ikue kwa kina kirefu na iwe yenye nguvu. (Ebr. 5:14) Kuweka miradi ya kiroho ya kibinafsi na kuifanyia kazi kwa bidii pia kutaleta manufaa yenye kudumu.—Flp. 3:16.
3 Msaada Kutoka kwa Wakomavu: Jaribu kupanua mashirika yako pamoja na watu walio wakomavu kiroho katika kutaniko. Pata kuwajua wazee, kwa kuwa hao ndio hasa wawezao kutuimarisha. (1 The. 2:11, 12) Kubali shauri lolote au madokezo ambayo huenda wakatoa. (Efe. 4:11-16) Pia watumishi wa huduma wanapendezwa kusaidia wengine waimarishwe katika imani, kwa hiyo tegemea kitia-moyo chao.
4 Je, wahitaji msaada katika huduma? Ongea na wazee, na uombe msaada. Labda waweza kutiwa katika programu ya Mapainia Wasaidia Wengine. Je, umebatizwa hivi majuzi? Kujifunza kitabu Huduma Yetu na kutumia yaliyo ndani yake kutachochea maendeleo kuelekea ukomavu wa kiroho. Je, wewe ni mzazi? Endelea kuimarisha hali ya kiroho ya watoto wako.—Efe. 6:4.
5 Kwa kutia mizizi na kuimarishwa katika imani, twafurahia uhusiano wa karibu na Yehova na ushirika mchangamfu pamoja na ndugu zetu. Hilo hutusaidia kukinza mashambulio ya Shetani, na huimarisha tumaini letu la uhai udumuo milele.—1 Pet. 5:9, 10.