Hatua Zifaazo Ili Kufanya Maendeleo Zaidi
1 Kufikia sasa wengi wetu tumemaliza kusoma Kitabu-Mwaka cha 1992 (Kiingereza). Kujifunza kuhusu kilele cha ulimwenguni pote cha 1991 cha wahubiri wa Ufalme zaidi ya milioni nne na robo katika nchi 211—ongezeko la asilimia 6.5—kulisisimua mioyo yetu! Kwa hakika, ongezeko la Ufalme linalotukia sasa kuzunguka ulimwengu linatoa uthibitisho wenye kutokeza wa utimizo wa Isaya 2:2-4 na Mika 4:1-4.
2 Ingawa ripoti ya mwaka wa utumishi wa 1992 si kamili, ithibati ni wazi kwamba Yehova anabariki mwaka huu wa utumishi na maongezeko yenye kutokeza. Mwaliko wa kujiunga na udugu wetu wa kimataifa ulio mkubwa unaendelea kutolewa. Hesabu za waliohudhuria kwenye Ukumbusho na mkusanyiko wa wilaya zinaonyesha kwamba mamilioni ya watu wanasikiliza ujumbe wa Ufalme. Kutoka mataifa yote, wanaitikia mwaliko uliopuliziwa roho unaoita: “Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [Yehova, NW], na nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”
3 Azimia Kufanya Maendeleo: Tengenezo la Yehova linasonga mbele. Kukiwa na wengi wapya wanaomiminika wakikwea kwenye mlima wa ibada ya kweli ya Yehova, ni jambo la maana kwa kila mmoja wetu kuchukua hatua ifaayo kuelekea kufanya maendeleo zaidi ya kiroho halafu tufikie kiasi cha kusaidia wapya zaidi wafanye vivyo hivyo. Uhitaji wa maendeleo kama hayo unaonyeshwa na maneno yanayosema kwamba wale wanaoitikia mwaliko wa kuja kwenye mlima wa Yehova wasema kwa wengine, “Njoni.” Mtume Yohana aliripoti jambo linalofanana na hilo kwenye Ufunuo 22:17: “Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo!”
4 Yesu alionyesha jinsi mwaliko huo wapaswa kutolewa. Watu walipoitikia mafundisho yake, yeye aliwaalika kushiriki katika huduma yake na akawafundisha jinsi ya kufanya hivyo. (Mt. 4:19; 10:5-7, 11-14) Wanafunzi wake walijifunza njia zenye matokeo alizotumia kwa kuandamana naye na kutazama jinsi alivyofanya mambo. Halafu wakafuata kigezo cha huduma yake. Walijifunza njia zake vizuri sana hivi kwamba ushahidi wao wenye ujasiri ulivuta uangalifu wa wapinzani waliotambua waziwazi kwamba wao walikuwa wanafunzi wa Yesu. Matendo 4:13 huripoti: “Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, . . . wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”
5 Kabla ya kurudi mbinguni, Yesu alitoa amri kwamba wanafunzi wake wapaswa waendeleze huduma ya Kikristo kwa kufanya wanafunzi wapya, na kuwafundisha kama vile wao wenyewe walivyofundishwa. Kwenye Mathayo 28:19, 20, Yesu aliamuru: “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, . . . na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” Na akionyesha kwamba alimaanisha hilo lingeendelea hadi siku yetu, yeye alitoa uhakikisho huu wa ziada: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari [mfumo wa mambo, NW].”
6 Wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo hawajashindwa kutii maagizo yake ya kufunza wanafunzi wapya mambo yote aliyoamuru. Hata hivyo, ukuzi wenye kutokeza katika kundi la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova unataka tufikirie mahitaji ya kipekee ya washiriki wapya wa kundi waliobatizwa na wahubiri wasiobatizwa pamoja na watu wanaojifunza Biblia pamoja nasi na ambao labda wanaanza kuhudhuria mikutano ya kundi kwa ukawaida fulani.
7 Mwanzoni mwa mwaka wa utumishi wa 1992, mhubiri 1 hivi kati ya 9 walikuwa wenye utendaji hudumani kwa mwaka mmoja tu. Kwa kuongezea, 1 kati ya 6 walikuwa wamekuwa wahubiri kwa muda wa miaka mitatu au chini ya hiyo; na 1 kati ya 4 wamekuwa wakishiriki katika huduma kwa muda usiozidi miaka mitano. Ingawa wapya wengi wamefanya maendeleo mazuri tangu wawe washiriki wa kundi, kwa kweli msaada zaidi katika mambo fulani ungeweza kuharakisha maendeleo yao ya kiroho.
8 Waebrania 6:1, NW hutia wote moyo ‘wasonge mbele kwenye kukomaa.’ Ukomavu wa Kikristo huwa zaidi tu ya kutoa ripoti ya utumishi. Inatia ndani kufanya maendeleo katika funzo la kibinafsi na uhudhuriaji wa kawaida wa mikutano pamoja na ushiriki wenye bidii katika huduma ya shambani. Kuwasaidia wengine waje kupata maarifa ya kweli kwa ajili ya wokovu kunatiwa ndani pia. Ni lazima tufanyie kazi kusitawisha mbinu zetu katika ‘kutoa sababu kutoka kwa Maandiko.’ (Mdo. 17:2) Kukua kufikia ukomavu hutaka wakati, na hutegemea kwa kiwango kikubwa juu ya ujitoaji wetu kwa Mungu na kupata kwetu ujuzi wenye kutumika shambani. Ingawa tuna udhibiti juu ya kina cha ujitoaji wetu kwa Mungu, ni mwendo wa hekima kuruhusu ndugu na dada wengine waliokomaa watusaidie tupate ujuzi wenye kutumika. Tunaweza kujifunza kwa ujuzi wao, hasa katika huduma ya shambani. Si lazima tujifunze kila kitu kivyetu kwa kujaribu na kukosea.
9 Msaada kwa Wale Wasio na Ujuzi: Kigezo cha kutoa msaada kiliwekwa mwanzoni mwa kundi la Kikristo. Yesu aliwaagiza wanafunzi wake. (Mk. 3:14; Lk. 9:1; 10:1) Wao nao waliwafundisha wengine. Timotheo alipokea kitia-moyo na msaada wa pekee kutoka kwa mtume Paulo, naye mwanafunzi Apolo alifanya maendeleo kwa msaada wa binafsi wa Akila na Prisila wenye ujuzi zaidi. (Mdo. 18:24-27; 1 Kor. 4:17) Washiriki waliokomaa wa kundi la Kikristo hufuata mifano hiyo leo, wakifundisha na kutia moyo wale wasio na ujuzi mwingi, hasa wapya na vijana. Kama vile Warumi 15:1, 2 isemavyo, “Imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu.”
10 Wazazi wana daraka la kuchukua hatua zifaazo kusaidia watoto wao waendelee kiroho. Hilo linatia ndani funzo la familia, kuwafunza watoto jinsi ya kujifunza binafsi, hudhurio na ushiriki wa kawaida wa mikutano, na ujuzi katika kutumia yale wanayojifunza. (Efe. 6:4; 1 Tim. 5:8) Viongozi wa Mafunzo ya Vitabu ya Kundi hasa wapaswa kuongoza katika kufanya mipango ili kusaidia wote katika funzo lao la kitabu na vikundi vya utumishi wa shambani kufanya maendeleo kwa njia ya kiroho. Mwangalizi wa utumishi na wazee wengine pamoja na watumishi wa huduma na washiriki wengineo wa kundi wanaweza kusaidia pia.
11 Andaa Yale Yanayohitajiwa: Huenda uhitaji ukawa kutoa msaada kwa ajili ya utendaji fulani wa Kikristo, kama vile funzo la kibinafsi. Huenda mtu akahitaji madokezo ili kuanzisha ratiba inayotumika ya funzo. Huenda mtu mwingine akahitaji msaada kutayarisha maelezo au migawo. Labda wengine wanahitaji kujifunza jinsi ya kufanya utafiti wa habari za Biblia.
12 Wapya wengi wanahitaji msaada katika huduma ya shambani. Huenda mhubiri akataka kuwa mwenye matokeo zaidi katika kazi ya nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia, au kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia. Huenda kufanya mazoezi machache kwa kutumia matangulizi yaliyodokezwa na utoaji mbalimbali kutoka kitabu Kutoa Sababu au kutoka Huduma ya Ufalme Yetu kukatosha. Nyakati nyingine, huenda madokezo ya ratiba inayotumika kwa ajili ya utumishi wa shambani na msaada wa kushikamana nayo yakawa ndiyo yanayohitajika. Kufanya mipango hususa ili kuhubiri pamoja na mtu anayehitaji msaada kutamwezesha yeye kufanya maendeleo kuelekea miradi hususa.
13 Neno la Mungu hututia moyo tuache maendeleo yetu ya kiroho yawe wazi kwa wengine. Hilo ndilo shauri ambalo Paulo alimwandikia mfanyakazi mwenzake Timotheo. (1 Tim. 4:15) Kwa kupatana na kitia moyo hicho, mtume alikazia uhitaji wa kujizoeza kama vile katika shindano la mbio katika riadha au katika kupata mafanikio katika vita ya kiroho. (1 Kor. 9:24-27; 2 Kor. 10:5, 6) Tunapaswa kuwa wenye haraka kutumia yote tunayojifunza kuhusu mapenzi ya Mungu ili watazamaji waone kwamba sisi ni mifano ya kweli ya imani ya Kikristo. Vivyo hivyo, tunapaswa tufanyie maendeleo stadi zetu za kufundisha wengine wawe wanafunzi waliojiweka wakfu wa Yesu Kristo.—Yak. 1:22-25; 1 Tim. 4:12-16.
14 Maendeleo Yanatia Ndani Kuvumilia Majaribu: Hata Yesu Kristo alijifunza masomo ya maana kwa mambo aliyoteseka. (Ebr. 5:8) Hata sisi twaweza. Kupatana na hayo, maendeleo ya kiroho hufanywa tunapokuwa na mtazamo ufaao uliopendekezwa kwenye Yakobo 1:2, 3: “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali, mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi.” Hivyo, iwe tunalazimika kukabiliana na magumu ya magonjwa ya kudumu, matatizo ya kiuchumi, kuishi katika nyumba iliyogawanyika, upinzani katika eneo, au hesabu yoyote ya hali nyinginezo mbaya, tuna uhakikisho wa Yehova kwamba kwa msaada wake tunaweza kushinda na kuendelea kufanya maendeleo katika ibada yetu kwake. (1 Kor. 10:13; 2 Kor. 12:9; 1 Pet. 5:8-11) Mafanikio hupatikana kwa ustahimilivu chini ya hali zote, ‘tukisema juu ya mausia ya Mungu, na katika kuhudumu, tukihudumu kwa nguvu tulizojaliwa na Mungu, ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo.’—1 Pet. 4:11.
15 Kubali Msaada Ili Kufanya Maendeleo Zaidi: Ikiwa ni wewe unayehitaji msaada ili kufanya maendeleo zaidi ya kiroho, kubali msaada kutoka kwa mshiriki wa kundi mwenye ujuzi zaidi. Hata ikiwa hujafikiwa kupewa msaada, usiruhusu haya ikunyang’anye fursa yako ya kupata msaada. Uliza msaada. Jihisi huru kutafuta msaada wa yeyote wa wale walio na ujuzi kundini. Au waweza kumwuliza msaada kiongozi wenu wa Funzo la Kitabu la Kundi, mwangalizi wa utumishi, au wazee wowote wengineo.—Linganisha Mwanzo 32:26; Mathayo 7:7, 8.
16 Kwa hakika, ni pendelo la ajabu kutiwa ndani ya “mkutano mkubwa” wa kimataifa unaozidi kuongezeka unaomiminika kwenda juu kwenye mlima wa Yehova wa ibada safi. (Ufu. 7:9) Pia ni pendeleo kuwaalika wengine waandamane nasi katika mkweo huu. Kwa uthamini wa moyoni, na tuendelee kuchukua hatua zifaazo ili kufanya maendeleo zaidi, kujenga hali yetu ya kiroho na kufanya yale tuwezayo kusaidia wengine wafanye maendeleo pamoja nasi katika utumishi wa Yehova.