Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 2/00 kur. 3-6
  • Kuhubiri Habari Njema kwa Usadikisho Wenye Nguvu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri Habari Njema kwa Usadikisho Wenye Nguvu
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2000
  • Habari Zinazolingana
  • Kuzungumza kwa Usadikisho
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Simameni Mkiwa Kamili kwa Usadikisho Imara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Wazazi​—Wasaidieni Watoto Wenu Wawe ‘Wenye Hekima kwa Ajili ya Wokovu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Uwe na Hakika Kwamba Umeipata Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2000
km 2/00 kur. 3-6

Kuhubiri Habari Njema kwa Usadikisho Wenye Nguvu

1 Mapema katika karne ya kwanza, Yesu Kristo aliamuru wafuasi wake wahubiri habari njema za Ufalme na “[ku]fanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 24:14; 28:19, 20) Mashahidi wa Yehova wamechukua agizo lake kwa uzito, hivi kwamba kufikia mwisho wa karne ya 20, udugu wetu wa Kikristo umeongezeka hadi kufikia zaidi ya wanafunzi 5,900,000 katika nchi 234. Hiyo ni sauti kuu ya sifa kwa Baba yetu wa kimbingu iliyoje!

2 Sasa tumeingia katika karne ya 21. Mpinzani wetu anajaribu kwa hila kuingilia kazi yetu kuu ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Yeye hutumia msongo kutoka katika mfumo huu wa mambo katika jitihada ya kukengeusha fikira zetu, kupoteza wakati wetu, na kudhoofisha nishati zetu kwa kutufanya tuwe na shughuli nyingi na mapendezi yasiyo ya maana. Badala ya kuruhusu mfumo huu utuamulie lililo la maana maishani, twajithibitishia kutoka katika Neno la Mungu jambo lililo kuu kupita yote—kufanya mapenzi ya Yehova. (Rom. 12:2) Hilo lamaanisha kutii himizo la Kimaandiko la ‘kuhubiri neno katika majira yenye kufaa na majira yenye taabu na kutimiza kikamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:2, 5.

3 Sitawisha Usadikisho Imara: Wakristo wanahitaji ‘kusimama wakiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.’ (Kol. 4:12) Neno “usadikisho” lafafanuliwa kuwa “ushawishi wenye nguvu au itikadi; hali ya kusadikishwa.” Tukiwa Wakristo lazima tusadiki kwamba neno la Mungu la kiunabii ni hakika na kwamba sasa twaishi wakati wa mwisho kabisa. Lazima tuwe na itikadi yenye nguvu kama ile ya mtume Paulo, aliyesema kwamba habari njema “kwa kweli . . . ni nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu mwenye imani.”—Rom. 1:16.

4 Ibilisi hutumia watu waovu na walaghai, ambao wenyewe wameongozwa vibaya, waathiri na kuongoza wengine vibaya. (2 Tim. 3:13) Tukiwa tumeonywa kimbele juu ya hilo, twachukua hatua kuimarisha usadikisho wetu kwamba tuna ile kweli. Badala ya kuacha mahangaiko ya maisha yadhoofishe bidii yetu, twaendelea kutanguliza masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33, 34) Wala hatutaki kupuuza uharaka wa nyakati, labda kwa kuhisi kwamba mwisho wa mfumo huu uko mbali sana. Unazidi kukaribia daima. (1 Pet. 4:7) Ijapokuwa huenda tukahisi kwamba kueneza habari njema kuna matokeo machache katika nchi nyingine kwa sababu ya ushahidi ambao tayari umetolewa, kazi ya kuonya lazima iendelee.—Eze. 33:7-9.

5 Maswali muhimu wakati huu uliosonga sana ni haya: ‘Je, mimi huchukua kwa uzito amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi? Ninapohubiri habari njema, je, mimi huonyesha usadikisho wenye nguvu kwamba Ufalme ni halisi? Je, nimeazimia kushiriki kwa kadiri kubwa iwezekanavyo katika huduma hii ya kuokoa uhai?’ Tukitambua pale ambapo tumefikia wakati huu wa mwisho, lazima tujichunguze wenyewe na utume wetu wa kuhubiri na kufundisha. Kufanya hivyo kutatuokoa sisi wenyewe na wale watusikilizao. (1 Tim. 4:16) Sisi sote twaweza kuimarishaje usadikisho wetu tukiwa wahudumu?

6 Waige Wathesalonike: Mtume Paulo, alipokuwa akikumbuka kazi yenye bidii ya akina ndugu katika Thesalonike, aliwaambia hivi: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu, kama vile nyinyi mjuavyo ni watu wa namna gani sisi tulipata kuwa kwenu kwa ajili yenu; nanyi mkawa waigaji wetu na wa Bwana, kwa vile mlilipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu.” (1 The. 1:5, 6) Naam, Paulo alilipongeza kutaniko la Wathesalonike kwa sababu kujapokuwa dhiki nyingi walihubiri kwa bidii na usadikisho wenye nguvu. Ni nini kilichowawezesha kufanya hivyo? Kwa kadiri kubwa, bidii na usadikisho walioona kwa mtume Paulo na wafanyakazi wenzake, ilikuwa na matokeo mazuri kwao. Jinsi gani?

7 Maisha ya Paulo na waandamani wenzake wasafirio yalitoa ushuhuda kwamba roho ya Mungu ilikuwa juu yao na kwamba waliamini kwa moyo wote kile walichokuwa wakihubiri. Kabla ya kuja Thesalonike, Paulo na Sila walitendwa kifidhuli huko Filipi. Walipigwa bila kufanyiwa kesi, wakafungwa jela, na kutiwa mikatale. Hata hivyo, jambo hilo lenye kuwatia jaribuni halikufisha bidii yao ya habari njema. Mwingilio wa kimungu uliathiri kufunguliwa kwao, ukaongoza kwenye kugeuzwa imani kwa mlinzi wa jela na watu wa nyumbani mwake, na ukafungulia ndugu hao njia ya kuendelea na huduma yao.—Mdo. 16:19-34.

8 Kwa nguvu ya roho ya Mungu, Paulo alikuja Thesalonike. Akiwa huko, alifanya kazi kwa jasho ili kupata mahitaji yake mwenyewe kisha akatumika kikamili akifundisha Wathesalonike kweli. Hakujizuia kutangaza habari njema katika kila fursa. (1 The. 2:9) Kuhubiri kwa Paulo kwa usadikisho wenye nguvu kulikuwa na matokeo makubwa kwa watu wa hapo hivi kwamba baadhi yao waliacha ibada ya awali ya sanamu na kuwa watumishi wa Mungu wa kweli, Yehova.—1 The. 1:8-10.

9 Mnyanyaso haukuzuia waamini wapya kuhubiri habari njema. Wakichochewa na imani yao mpya na kusadikishwa kikamili kwamba wangepokea baraka za milele, Wathesalonike walichochewa kutangaza kweli ambayo walikuwa wameikubali kwa uchangamfu. Kutaniko hilo likawa lenye kutenda kwelikweli hivi kwamba habari za imani na bidii yao zilienea kwenye sehemu nyingine za Makedonia na hata Akaya. Kwa sababu hiyo, Paulo alipoandika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike, kazi zao nzuri zilikuwa tayari zinajulikana. (1 The. 1:7) Ni kielelezo bora kama nini!

10 Kuchochewa na Upendo kwa Mungu na kwa Watu: Kama vile Wathesalonike, sisi twaweza kudumishaje usadikisho wenye nguvu tunapohubiri habari njema leo? Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Bila kukoma twazingatia akilini kazi yenu ya uaminifu na jitihada yenu ngumu kwa sababu ya upendo.” (1 The. 1:3, kielezi-chini katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References) Ni dhahiri kwamba walikuwa na upendo wenye kina kutoka moyoni kuelekea Yehova Mungu na kwa watu waliowahubiria. Ni upendo huohuo ambao ulimchochea Paulo na waandamani wake kuwapa Wathesalonike “si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi [zao] wenyewe.”—1 The. 2:8.

11 Vivyo hivyo, upendo wetu wenye kina kwa Yehova na kwa wanadamu wenzetu hutuchochea tutake kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri ambayo Mungu ametupatia tuifanye. Tukiwa na upendo huo, twatambua kwamba kuhubiri habari njema ni daraka letu binafsi, tulilopewa na Mungu. Kwa kutafakari kwa njia inayofaa na kwa uthamini juu ya yale yote ambayo Yehova ametufanyia katika kutuelekeza kwenye “uhai ulio halisi,” twachochewa kuwaambia wengine kweli hizohizo za ajabu ambazo twaamini kwa moyo wetu wote.—1 Tim. 6:19.

12 Tunapokuwa wenye shughuli katika kazi ya kuhubiri, upendo wetu kwa Yehova na kwa watu lazima uendelee kukua. Ukuapo, tutachochewa kuzidisha ushiriki wetu katika huduma ya mlango hadi mlango na kufuatia aina nyingine zote za kutoa ushahidi zilizo wazi kwetu. Tutatumia kwa manufaa fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa watu wa ukoo, majirani, na watu tunaowafahamu. Ijapokuwa watu walio wengi zaidi huenda wakakataa habari njema tunazowapa na wengine huenda wakajitahidi kuingilia kutangazwa kwa Ufalme, twapata shangwe ya kutoka ndani. Kwa nini? Kwa sababu twajua kwamba tumefanya tuwezavyo kutoa ushahidi juu ya Ufalme na kusaidia watu wapate wokovu. Naye Yehova atabariki jitihada zetu za kupata watu wenye moyo ufaao. Hata misongo ya maisha inapotukaza na Shetani anapojaribu kudhoofisha shangwe yetu, tunaweza kudumisha usadikisho wetu wenye nguvu na bidii yetu ya kutolea wengine ushahidi. Sisi sote tufanyapo sehemu yetu, hilo hutokeza makutaniko yenye nguvu, yenye bidii kama lile la Thesalonike.

13 Usikate Tamaa Kamwe Wakati wa Jaribu: Pia usadikisho wahitajiwa tunapopatwa na majaribu mbalimbali. (1 Pet. 1:6, 7) Yesu alieleza wanafunzi wake wazi kwamba ikiwa wangemfuata, wangekuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote.” (Mt. 24:9) Paulo na Sila walipatwa na jambo hilo huko Filipi. Simulizi katika Matendo sura ya 16 husema kwamba Paulo na Sila walitupwa katika gereza la ndani na kuwekwa mikatale. Kwa ujumla, gereza kuu lilikuwa kama kitala au sebule ambayo kwenye kingo zake kulikuwa na seli zenye nuru na hewa. Hata hivyo, gereza la ndani halikuwa na nuru na hewa ya kutosha. Paulo na Sila walilazimika kukabili giza, joto, na harufu mbaya ya mahali hapo penye taabu pa kifungo. Je, waweza kuwazia maumivu waliyohisi wakiwa wamefungwa mikatale kwa muda wa saa nyingi migongo yao ikiwa imechubuka na kuvuja damu kwa sababu ya kupigwa mijeledi?

14 Yajapokuwa majaribu hayo, Paulo na Sila walidumu wakiwa waaminifu. Walionyesha usadikisho wa kutoka moyoni, ukiwaimarisha wamtumikie Yehova bila kujali jaribu hilo. Usadikisho wao wakaziwa kwenye mstari wa 25 wa sura ya 16, ambao husema kwamba Paulo na Sila walikuwa “wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” Kwa kweli, ingawa walikuwa katika chumba cha ndani zaidi, walikuwa na uhakika sana wa kuwa na kibali cha Mungu hivi kwamba waliimba kwa sauti ya juu mpaka wakasikiwa na wafungwa wengine! Lazima tuwe na usadikisho kama huo leo tunapokabili majaribu ya imani yetu.

15 Ibilisi hututia katika majaribu mengi sana. Kwa wengine, huenda ikawa ni mnyanyaso kutoka kwa familia. Ndugu zetu wengi hukabili magumu ya kisheria. Huenda tukakabili upinzani kutoka kwa waasi-imani. Kuna mizigo yenye kulemea ya kifedha na wasiwasi wa jinsi ya kupata riziki. Vijana hukabili msongo wa marika shuleni. Twaweza kukabilianaje na majaribu haya kwa mafanikio? Ni nini kinachohitajiwa ili kuonyesha usadikisho?

16 Kwanza kabisa, twahitaji kudumisha uhusiano wa karibu na wa kibinafsi na Yehova. Paulo na Sila walipokuwa katika gereza la ndani zaidi, hawakutumia wakati huo kulalamika juu ya hali yao ya maisha au kujihurumia. Walimgeukia Mungu mara moja kwa sala na kumsifu kwa wimbo. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa na uhusiano wa karibu na wa kibinafsi na Baba yao wa kimbingu. Walitambua kwamba walikuwa wakiteseka kwa sababu ya uadilifu na kwamba wokovu wao ulikuwa mikononi mwa Yehova.—Zab. 3:8.

17 Tunapokabili majaribu leo, sisi pia lazima tumtegemee Yehova. Paulo anatutia moyo tukiwa Wakristo ‘tuache maombi yetu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova hatatuacha tuvumilie majaribu tukiwa peke yetu! (Isa. 41:10) Yeye yuko pamoja nasi sikuzote maadamu twamtumikia kwa usadikisho wa kweli.—Zab. 46:7.

18 Msaada mwingine muhimu wa kuonyesha usadikisho ni kuendelea kuwa na shughuli katika utumishi wa Yehova. (1 Kor. 15:58) Paulo na Sila walitiwa gerezani kwa sababu walikuwa wakishughulika na kuhubiri habari njema. Je, waliacha kuhubiri kwa sababu ya majaribu yao? La, waliendelea kuhubiri walipokuwa gerezani, na baada ya kuachiliwa, walisafiri hadi Thesalonike na wakaenda kwenye sinagogi la Wayahudi ‘wakajadiliana nao kwa kutoa sababu kutokana na Maandiko.’ (Mdo. 17:1-3) Tunapokuwa na usadikisho au itikadi yenye nguvu katika Yehova na tumesadiki kwamba tuna kweli, hakuna chochote ‘kitakachoweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.’—Rom. 8:35-39.

19 Vielelezo vya Kisasa vya Usadikisho Wenye Nguvu: Kuna vielelezo vingi vyenye kutokeza vya watu katika siku yetu, ambao kama Paulo na Sila, wameonyesha usadikisho wenye nguvu. Dada mmoja ambaye aliokoka kwenye kambi ya mateso ya Auschwitz asimulia juu ya imani na usadikisho usiotikisika ulioonyeshwa na akina ndugu na dada waliokuwa huko. Yeye asimulia hivi: “Siku moja wakati wa kuhojiwa, ofisa mmoja alinijia akiwa amekunja ngumi. ‘Nyinyi watu tutawafanyaje?’ akasema kwa mkazo. ‘Tukiwakamata, hamjali. Tukiwapeleka gerezani, hamjali hata kidogo. Tukiwapeleka kwenye kambi ya mateso, hamhangaishwi na jambo hilo. Tukiwapa hukumu ya kifo, mwasimama bila kujali tu. Tuwafanyeje?’” Inaimarisha imani kama nini kuona imani ambayo ndugu zetu walikuwa nayo katika hali hizo ngumu! Walimtegemea Yehova daima awasaidie kuvumilia.

20 Hakika twakumbuka usadikisho wa wengi wa ndugu zetu wanaokabili chuki ya kikabila ambayo imetokea miaka ya hivi majuzi. Wajapojikuta katika hali zenye hatari, ndugu wenye madaraka hukusudia kuona kwamba ndugu na dada zao wanalishwa kiroho. Wote wanaendelea kwa uaminifu wakiwa na usadikisho wenye nguvu kwamba ‘kila silaha itakayofanyika juu yao haitafanikiwa.’—Isa. 54:17.

21 Wengi wa ndugu na dada zetu walio na wenzi wasioamini pia wanaonyesha imani na uvumilivu wenye nguvu. Ndugu mmoja huko Guadeloupe alikabili upinzani mkali kutoka kwa mke wake asiyeamini. Ili amvunje moyo na kuingilia kuhudhuria kwake mikutano ya Kikristo, mke wake hakuwa akimtayarishia milo yake au kufua, kupiga pasi, na kushona nguo zake. Hangemzungumzia kwa muda mrefu. Lakini kwa kuonyesha usadikisho kutoka moyoni kwa kumtumikia Yehova na kumwendea kwa sala apate msaada, ndugu huyo aliweza kuvumilia yote hayo. Kwa muda gani? Kwa miaka 20 hivi—ambapo baadaye mke wake alibadili mtazamo wake. Hatimaye, angeweza kuwa na shangwe kikweli kwa sababu alikubali tumaini la Ufalme wa Mungu.

22 Hatimaye, tusisahau kamwe usadikisho wenye nguvu wa ndugu na dada zetu wachanga ambao huhudhuria shule kila siku na kushughulika na msongo wa shule na magumu mengineyo. Kuhusu msongo wa kujipatanisha na shule, msichana mmoja Shahidi asema hivi: “Unapokuwa shuleni, kila mtu anakutia moyo uasi kidogo. Watoto wanakuheshimu zaidi unapofanya jambo linaloelekea kuwa uasi.” Vijana wetu wanakabili msongo kama nini! Wengine karibu wameharibu uhusiano wao na Yehova kwa sababu walishindwa na msongo wa kutaka kujipatanisha. Azimia kwa uthabiti akilini na moyoni kukinza kishawishi.

23 Wengi wa vijana wetu wanaendelea vizuri katika kudumisha uaminifu-maadili wao yajapokuwa majaribu. Kielelezo kimoja ni cha dada mmoja kijana anayeishi Ufaransa. Siku moja baada ya chakula cha mchana, wavulana fulani walijaribu kumlazimisha awabusu, lakini alisali na kukinza kwa nguvu, kwa hiyo, wavulana hao wakamwacha. Baadaye, mmoja wao alikuja na kumwambia kwamba alipendezwa na moyo wake mkuu. Aliweza kumtolea ushahidi mzuri juu ya Ufalme, akimweleza viwango vya juu ambavyo Yehova huwekea wote wanaotaka kushiriki baraka zake. Mwaka wote alipokuwa shuleni, alieleza pia darasa lote itikadi zake.

24 Tuna pendeleo lenye thamani kama nini kuhesabiwa miongoni mwa wale ambao Yehova anapendezwa kutumia kuongea kwa usadikisho imara juu ya mapenzi yake! (Kol. 4:12) Kwa kuongezea, tuna pendeleo zuri ajabu la kuthibitisha uaminifu-maadili tunaposhambuliwa na Mpinzani wetu aliye kama simba, Shetani Ibilisi. (1 Pet. 5:8, 9) Usisahau kamwe kwamba Yehova anatumia ujumbe wa Ufalme kuleta wokovu kwetu tunaouhubiri na wale wanaousikiliza. Maamuzi tunayofanya na njia yetu ya kila siku ya maisha na ithibitishe kwamba twautanguliza Ufalme. Na tuendelee kuhubiri habari njema kwa usadikisho wenye nguvu!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki