“Ningewezaje . . . Isipokuwa Mtu Fulani Angeniongoza?”
1 Mweneza-evanjeli Filipo alipomuuliza towashi Mwethiopia kama alielewa alichokuwa akisoma kutoka Neno la Mungu, mtu huyo alijibu hivi: “Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?” Filipo alifurahia kumsaidia aelewe habari njema kuhusu Yesu, hiyo ikisababisha mtu huyo abatizwe mara hiyo. (Mdo. 8:26-38) Filipo alikuwa akitii utume kutoka kwa Kristo wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza na kuwafundisha.’—Mt. 28:19, 20.
2 Lazima tutii utume wa kufanya wanafunzi, kama Filipo alivyotii. Hata hivyo, maendeleo hayo ya kiroho ya haraka ambayo towashi Mwethiopia alifanya hayaonekani mara nyingi miongoni mwa watu tunaojifunza nao Biblia. Mwanamume huyo, mgeuzwa-imani wa Kiyahudi aliyekuwa na ujuzi mwingi sana wa Maandiko, alikuwa na moyo mpokezi naye alihitaji tu kukubali kwamba Yesu ndiye aliyekuwa Mesiya aliyeahidiwa. Ni jambo gumu ikiwa wale tunaojifunza nao hawaijui Biblia, wameongozwa vibaya na mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli, au wamelemewa na matatizo magumu ya kibinafsi. Ni nini kitakachotusaidia tuwe na mafanikio ya kuwaongoza wanafunzi wa Biblia wajiweke wakfu na kubatizwa?
3 Fahamu Mahitaji ya Kiroho ya Mwanafunzi wa Biblia: Nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Agosti 1998 ilizungumzia muda ambao huenda tukatumia kujifunza na watu broshua Anataka na kitabu Ujuzi. Ilitoa mwelekezo huu: “Ni muhimu kukadiria mwendo wa funzo kulingana na hali na kipaji cha mwanafunzi. . . . Hatutaki kumzuia mwanafunzi kupata uelewevu ulio wazi kwa sababu tu ya kumaliza kitabu haraka. Kila mwanafunzi huhitaji msingi imara wa imani yake mpya katika Neno la Mungu.” Kwa sababu hiyo, haifai kuharakisha habari iliyo katika kitabu Ujuzi huku tukijaribu kumaliza kitabu kwa miezi sita. Huenda ikahitaji zaidi ya miezi sita kusaidia watu wafanye maendeleo kiasi cha kubatizwa. Unapoongoza funzo kila juma, tumia wakati wowote unaohitajika kumsaidia mwanafunzi aelewe na kukubali yale anayojifunza kutokana na Neno la Mungu. Katika visa fulani, huenda majuma mawili au matatu yakahitajiwa ili kumaliza sura moja ya kitabu Ujuzi. Hilo litaruhusu wakati wa kusoma na kuelewesha maandiko mengi yaliyotajwa bila kunukuliwa.—Rom. 12:2.
4 Hata hivyo, vipi ikiwa baada ya kumaliza kitabu Ujuzi, unatambua kwamba uelewevu wa mwanafunzi kuhusu kweli wahitaji kuongezwa au kwamba bado hajachochewa kikamili kuchukua msimamo kwa ile kweli na kuweka maisha yake wakfu kwa Mungu? (1 Kor. 14:20) Unaweza kufanya nini zaidi ili umwongoze kwenye barabara inayoongoza kwenye uhai?—Mt. 7:14.
5 Tosheleza Mahitaji ya Kiroho ya Mwanafunzi wa Biblia: Kama ni dhahiri kwamba mtu huyo anafanya maendeleo, ingawa polepole, na kwamba anathamini yale anayojifunza, basi endeleza funzo la Biblia kupitia kitabu cha pili baada ya kumaliza broshua Anataka na kitabu Ujuzi. Hiyo si lazima katika kila kisa, lakini inapohitajiwa, endeleza funzo kwa kitabu Amani ya Kweli, Umoja Katika Ibada, au Neno la Mungu. Wahubiri wengi wana nakala za kibinafsi za vitabu hivyo ikiwa kutaniko halina. Wakati wote, broshua Anataka na kitabu Ujuzi ndivyo vitakavyotumiwa kujifunzia kwanza. Funzo la Biblia, ziara za kurudia, na wakati unaotumiwa kuendeleza funzo wapaswa kuhesabiwa na kuripotiwa, hata kama mwanafunzi amebatizwa kabla ya kumaliza kujifunza kitabu cha pili.
6 Je, hilo lamaanisha kwamba wale ambao walibatizwa karibuni lakini walijifunza kitabu kimoja tu wanapaswa kupewa msaada mpya wa kujifunza kitabu cha pili? Si lazima. Hata hivyo, huenda wamekuwa si watendaji au hawajafanya maendeleo katika kweli, nao huenda wakahisi kwamba wanahitaji msaada wa kibinafsi ili kutumia kweli zaidi katika maisha yao. Inafaa kuwasiliana na mwangalizi wa utumishi kabla funzo halijaanzishwa upya na mhubiri aliyebatizwa. Hata hivyo, ikiwa unajua watu fulani ambao walijifunza kitabu Ujuzi zamani lakini hawajafikia kujiweka wakfu na kubatizwa, unaweza kuchukua hatua ya kuona kama wangependa kurudia funzo lao la Biblia.
7 Ni ishara ya upendo wa Kikristo kutoa uangalifu wa kibinafsi kwa kila mtu mwenye kupendezwa tunayejifunza naye. Lengo letu ni kusaidia mwanafunzi afikie ufahamu wenye kina zaidi wa kweli ya Neno la Mungu. Kisha aweze kuchukua msimamo kamili, wenye ujuzi wa kweli na aweke maisha yake wakfu kwa Yehova, akionyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji.—Zab. 40:8; Efe. 3:17-19.
8 Je, wakumbuka lililotokea baada ya towashi Mwethiopia kubatizwa? “Alifuliza kwenda njia yake akishangilia” akiwa mwanafunzi mpya wa Yesu Kristo. (Mdo. 8:39, 40) Na tupate shangwe sisi na vilevile wale tunaoongoza kwenye njia ya kweli kwa mafanikio katika kumtumikia Yehova Mungu—sasa na hata milele!