“Kwa Mungu Mambo Yote Yawezekana”
1 Kazi kuu ya kutaniko la Kikristo ni kuhubiri ujumbe wa Ufalme ulimwenguni kote. (Mt. 24:14) Hiyo ni kazi kubwa sana. Machoni pa watu wengi, yaonekana kana kwamba kazi hiyo yahitaji fedha nyingi kuliko zile tulizo nazo. Kwa wengine, kutimiza kazi hii hakuwezekani kwa sababu tunadhihakiwa, tunapingwa, na kunyanyaswa. (Mt. 24:9; 2 Tim. 3:12) Watu wenye kutilia shaka wanasadiki kwamba kazi hii haiwezi kutimizwa. Hata hivyo, Yesu alisema: “Kwa Mungu mambo yote yawezekana.”—Mt. 19:26.
2 Vielelezo Vinavyofaa Kuigwa: Yesu alianza huduma yake huku akipingwa na ulimwengu wote. Ili kujaribu kumzuia asifanikiwe, wapinzani walimwaibisha kupita kiasi, hatimaye wakamwua kwa njia yenye maumivu makali mno. Lakini mwishowe, Yesu alisema hivi kwa ujasiri: “Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yn. 16:33) Kweli ulikuwa ushindi mkubwa kama nini!
3 Wanafunzi wa Yesu walikuwa na moyo mkuu na bidii hiyohiyo katika huduma ya Kikristo. Wengi wao walicharazwa viboko, wakatiwa gerezani, na hata kuuawa. Ingawa hivyo, walikuwa “wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 5:41) Wakiwa na magumu mengi, walitimiza kazi ambayo ilionekana kwamba haiwezekani ya kuhubiri habari njema “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Mdo. 1:8; Kol. 1:23.
4 Jinsi ya Kufaulu Katika Siku Zetu: Sisi pia tunafanya kazi ya kuhubiri yajapokuwa yale yaonekanayo kuwa magumu yasiyoweza kushindwa. Yajapokuwa marufuku, minyanyaso, vifungo vya gerezani, na vitisho vingine vya jeuri vya kutusimamisha, tunaendelea kufaulu. Hiyo yawezekanaje? “Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema BWANA wa majeshi.” (Zek. 4:6) Kwa kuwa Yehova anatutegemeza, hakuna kitu chochote kiwezacho kusimamisha kazi yetu!—Rom. 8:31.
5 Tunapohubiri, hatuna sababu ya kuona haya au kuogopa au kuhisi hatustahili. (2 Kor. 2:16, 17) Tuna sababu zisizoshindwa za kuendelea mbele katika kueneza habari njema za Ufalme. Tutatimiza “yasiyowezekana” kwa msaada wa Yehova!—Luka 18:27.