Tupangie Mambo Gani ya Wakati Ujao?
1 Sisi sote hupangia mambo yetu ya wakati ujao. Wale walio na tumaini la kidunia wanatazamia kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. Lakini kuna mavutano yanayoweza kumnyang’anya mtu tumaini hilo la moyo wote. Jitihada yahitajiwa ili kuendelea kuelekeza maisha zetu kwenye masilahi ya Ufalme na kutokengeushwa na tamaa za mwili zenye kushawishi.—1 Yoh. 2:15-17.
2 Ulimwengu hauwezi kuelewa miradi ya watu wanaokazia fikira mambo ya kiroho. (1 Kor. 2:14) Huku wanadamu wengine waking’ang’ana kupata umashuhuri, mamlaka, au utajiri sisi twajitahidi kuweka hazina za kiroho. (Mt. 6:19-21) Ikiwa tungejaribu kurekebisha kufikiri kwetu kupatane na maoni ya ulimwengu kuhusu wakati ujao, je, kweli tungefikia miradi yetu ya kiroho? Mambo ya kilimwengu yataijaza mioyo yetu. Twaweza kuzuiaje jambo hilo?
3 ‘Mvaeni Bwana Yesu Kristo’: Njia moja ya kuamua kama twajenga wakati wetu ujao katika masilahi ya Ufalme ni kuchunguza mazungumzo yetu. Je, sikuzote sisi huongea kuhusu vitu vya kimwili na mapendezi ya kilimwengu? Ikiwa ndivyo, lazima tuchunguze kama moyo wetu unakosa kukazia fikira mambo ya kiroho. Huenda tukahitaji kuzingatia sana ‘kumvaa Bwana Yesu Kristo badala ya kupangia kimbele tamaa za mwili.’—Rom. 13:14.
4 Vijana wanaweza ‘kumvaa Kristo’ kwa kupangia siku watakayoanza huduma ya wakati wote. Kijana fulani aliyetaka kufanya upainia wa kawaida alikuwa amelelewa katika utamaduni ambao ilikuwa kawaida kwa wanaume wachanga kuimarisha hali yao ya kiuchumi. Hivyo, alijiingiza sana katika biashara kufikia hatua ya kwamba alikuwa akihudhuria mikutano na kushiriki katika huduma kijuujuu tu. Alipoanza kutumaini maneno ya Yesu yapatikanayo kwenye Mathayo 6:33 na kuacha kazi hiyo yenye kuchosha isiyokuwa na matokeo, alianza utumishi wa wakati wote. Sasa, anamtumikia Yehova kwa dhamiri safi, ‘kwa uwezo wake wote,’ kama asemavyo.
5 Biblia husema kwamba ni jambo la hekima kupangia wakati ujao. (Mit. 21:5) Sisi sote na tufanye hivyo tukitanguliza mapenzi ya Mungu.—Efe. 5:15-17.