Jenga Wakati Ujao Wako na Tengenezo la Yehova
“Mwogope Yehova mchana kutwa. Kwa maana ndipo kutakuwa wakati ujao, na tumaini lako mwenyewe halitakatiliwa mbali.”—MITHALI 23:17, 18, New World Translation.
1, 2. Kati ya mambo mengine, mtume Yohana aliona nini karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K.?
YEHOVA huwafunulia watu wake mambo ya wakati ujao na hilo linawawezesha watende kwa hekima. (Isaya 42:9) Kwa mfano, karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K., Mungu alimpa mtume Yohana aliyezeeka njozi za wakati ujao. Tunaweza kuwa na furaha kama nini kwamba Yohana alishuhudia “mambo yote aliyoyaona” na kwamba yameandikwa katika kitabu cha Ufunuo cha Biblia!—Ufunuo 1:1, 2.
2 Kati ya mambo mengine, Yohana aliona “malaika wanne” wakizuia “pepo” ambazo zingetokeza ile “dhiki kubwa.” Malaika hao wangepaswa kuzuia pepo hizo za uharibifu kwa muda gani? Malaika mwingine aliwaambia: “Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao.”—Ufunuo 7:1-3,14; Mathayo 24:21, 22.
3. Kabla ya “pepo” zilizoachiliwa kuleta maangamizi juu ya tengenezo la Shetani, ni jambo gani litakuwa limetokea na kwa njia gani?
3 “Pepo” zilizoachiliwa zitaleta maangamizi juu ya tengenezo la kidunia la Shetani Ibilisi, na kuliharibu kabisa. (Linganisha Yeremia 25:32, 33.) Lakini kabla hilo halijatokea mabaki ya wapakwa mafuta ambao watatawala na Yesu Kristo mbinguni ni lazima watiwe muhuri. Kutiwa muhuri kwa hao “watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao” kunafanywa kupitia roho takatifu ya Mungu, au nguvu ya utendaji, ambayo Wakristo waliopakwa mafuta wanayo ikiwa ni kionyesho cha urithi wao wa kimbingu. (2 Wakorintho 1:21, 22; Waefeso 1:12-14) Kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu katika “siku za mwisho” kunakamilisha kukusanywa kwa “wateule” hao.—Mika 4:1; Mathayo 24:14, 31.
4. Ni “watumwa wa Mungu wetu” wangapi watakaotiwa muhuri ya kudumu, na unaweza kuthibitishaje jibu lako Kimaandiko?
4 Ni “watumwa wa Mungu wetu” wangapi watakaotiwa muhuri ya kudumu? Yohana, ambaye alikuwa mmoja wao, aliripoti hivi kwa uaminifu: “Nikasikia hesabu ya wale waliotiwa muhuri . . . watu mia na arobaini na nne elfu.” Wao ndio washiriki wa ‘Israeli wa Mungu,” Israeli wa kiroho, inayofanyizwa na makabila 12 yenye 12,000 kila moja. (Ufunuo 7:4-8; Wagalatia 6:16) Ni tengenezo zuri kama nini! Chini ya Mfalme Yesu Kristo, wale 144,000 watakuwa “ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao [watamiliki] juu ya nchi.”—Ufunuo 5:10; 14:1-4.
5. (a) Ni akina nani ambao sasa wanashirikiana na mabaki ya Israeli wa kiroho? (b) Wote wanaomwogopa Yehova wanafanyiza nini, na kulingana na Mithali 23:17, 18, ni jambo gani lililopo kwa ajili yao?
5 Baada ya mtume Yohana kuona Israeli wa kiroho, yeye aliona “mkutano mkubwa” na akataka kujua wao ni nani. Aliambiwa hivi: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Wale ambao ni washiriki wa “mkutano mkubwa” ndio raia za kidunia wa Ufalme huo, na ilitabiriwa kwamba “Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo, angewaongoza “kwenye chemchemi za maji yenye uhai”—ndiyo, uzima wa milele juu ya dunia paradiso. (Ufunuo 7:9, 14, 17; Luka 23:43) Sasa hivi “kondoo wengine” hao wamekuwa “kundi moja” pamoja na mabaki ya warithi wa Ufalme, na hao wote wenye kumwogopa Yehova ndio wanaofanyiza tengenezo la kidunia la Mungu. (Yohana 10:16) Kwa kubaki waaminifu kwake, watakuwa na wakati ujao wenye baraka, kwa maana tunasoma hivi: “Mwogope Yehova mchana kutwa. Kwa maana ndipo kutakuwa wakati ujao, na tumaini lako mwenyewe halitakatiliwa mbali.”—Mithali 23:17, 18, NW.
Mfumo Huu wa Kale Hauna Wakati Ujao!
6. Sasa sisi tunajikuta wapi katika mfululizo wa wakati?
6 Sasa tumesonga sana ndani ya “siku za mwisho” za huu mfumo mbovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5) Matukio ya ulimwengu yakilinganishwa na tarehe za Biblia yanathibitisha uhakika wa kwamba Yesu Kristo alianza kutawala mbinguni katika masika ya 1914. (Zaburi 110:1, 2) Ripoti za habari za kila siku zinaonyesha kwamba “ishara” yenye mambo mengi ya “kuwapo” (NW) kwa Yesu na umalizio wa huu mfumo zinaonekana. (Mathayo, sura za 24, 25) Ni kweli kwamba “kizazi” kile cha wakati mmoja na Ufalme wa Mungu uliposimamishwa mwaka wa 1914 kimesonga sana katika miaka. Lakini maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba “hakitapita” kabla “dhiki kubwa” haijakomesha ulimwengu huu wa jamii ya kibinadamu isiyo na uadilifu ambao ‘uko chini ya uwezo wa yule mwovu,’ Shetani Ibilisi. Jambo hilo litatokea upesi kadiri gani? Hakika kabla ya muda mrefu kupita, kwa maana huu ni mwaka wa 70 wa utawala wa Ufalme.—Mathayo 24:21, 34; 1 Yohana 5:19, NW.
7. (a) Ni jambo gani litakalotokea wakati wa sehemu ya kwanza ya “dhiki kubwa”? (b) Ni jambo gani litakalotokea muda mfupi baada ya uharibifu wa dini ya uongo?
7 “Dhiki kubwa” itaanza kwa ughafula wenye kustaajabisha. (Mathayo 24:36-44) Katika sehemu yake ya kwanza, uharibifu utaipata ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Kuangamizwa kwa kisehemu hicho kikuu cha mfumo wa Shetani kutakuwa na matokeo juu ya sehemu za kisiasa na kibiashara. Kwa habari hiyo, mtume Yohana alifunua kwamba ‘wafalme wa dunia’ wataomboleza hivi: “Ole, ole, mji ule ulio mkuu, Babeli, mji ule ulio na nguvu! kwa kuwa katika saa moja hukumu yako imekuja.” Na namna gani juu ya sehemu ya kibiashara? “Nao,” Yohana aongeza, “wafanya biashara wa nchi walia na kumwombolezea, kwa sababu hapana mtu anunuaye bidhaa yao tena.” (Ufunuo 18:1-19) Muda mfupi baada ya kuharibiwa kwa dini ya uongo, Yesu Kristo atatumia jeshi lake la kimbingu kuharibu sehemu iliyosalia ya huu mfumo mbovu wa mambo. Itaangamia katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni, vita inayokaribia haraka sana.—Ufunuo 16:14-16; 19:11-21.
8. Ni tengenezo gani pekee lenye wakati ujao wa kudumu, na kwa sababu gani ndivyo ilivyo?
8 Hiyo inamaanisha nini kwa wale wenye kumwogopa Yehova kwa njia inayofaa? Inamaanisha kwamba ulimwengu huu ulio chini ya uongozi wa Shetani hauna wakati ujao! Wakati wake karibu umekwisha! Kwa hiyo, tengenezo la Yehova ndilo pekee la kujengea wakati ujao wa milele.
9. (a) Kwa sababu ya yaliyo mbele, ni maulizo gani yanayofaa kuulizwa? (b) Ni shauri gani la wakati unaofaa linalopatikana kwenye 1 Timotheo 6:17-19?
9 Kwa sababu ya yaliyoko mbele, basi, je, ingeonyesha imani, au hata akili nzuri, kujaribu kujenga wakati ujao ulio salama juu ya sehemu fulani ya huu mfumo uliohukumiwa maangamizi? Kwa mfano, unaweza kujenga wakati ujao wenye kudumu ulio salama pamoja na shirika gani la kibiashara la kilimwengu? Hakuna hata moja! Basi je, si jambo la hekima kuridhika na chakula na mavazi huku ukiweka faida za Ufalme kwanza maishani? (Mathayo 6:33; 1 Timotheo 6:7-12; 2 Timotheo 2:4) Hasa, shauri la Paulo sasa ni la wakati unaofaa: “Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.”—1 Timotheo 6:17-19.
Jenga Wakati Ujao Wako kwa Hekima
10. Kwa kuwa “dhiki kubwa” inaonekana pale tu mbele yetu, hangaiko letu kuu lapasa kuwa nini?
10 Maneno hayo ya mtume yanaonyesha usawaziko wa kiroho kama nini! Katika hayo watu wa Yehova wanaona ufunguo wa kutokeza wokovu. Ndio huu: Weka vitu vya kimwili mahali pavyo panapofaa, ukitambua kwamba mkazo wapaswa kuwekwa si juu ya “utajiri usio yakini” bali juu ya kuwa “matajiri kwa kutenda mema.” Hakika hilo lingetia pia kushiriki kwa bidii na kwa ukawaida katika huduma ya Kikristo. Mawingu ya tufani ya “dhiki kubwa” tayari yakiwa yanakusanyika kule kwenye upeo wa macho, huu sio wakati wa kupangia wakati ujao wenye fanaka katika shirika fulani la biashara la kilimwengu au kupandishwa cheo. Huu ni wakati wa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, kuwaonya wasiojua juu ya hatari inayokaribia. Zaidi ya hayo, Yesu Kristo ametuagiza tuhubiri na kufanya wanafunzi. Kwa hiyo, hilo lapasa kuwa ndilo hangaiko kuu letu tukiwa Mashahidi wa Yehova.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Isaya 43:10-12.
11. Baadhi ya faida za kudumu za huduma yetu ya Kikristo zitakuwa gani?
11 Kazi nyingi zinazofuatiwa sasa na watu wa ulimwengu zitakoma milele wakati wa “dhiki kubwa.” Ni kweli kwamba kazi fulani fulani zitaanzishwa tena katika mfumo wa mambo mapya wa Mungu ulioahidiwa. Lakini je, wewe unajua kazi yo yote ya kisasa yenye mambo mengi ya faida kama huduma ya Kikristo? Ukuzi wa kiroho na maendeleo yanayoletwa na kazi hiyo iliyotolewa na Mungu utakuwa wenye faida zaidi katika Utaratibu Mpya. Uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova unaositawishwa katika huduma utaendelea mpaka mfumo wa mambo huo. Na ufundi wa kufundisha uliofanyiwa maendeleo waweza ukawa msaada katika kuelimisha mamilioni watakaofufuliwa wakati huo.—Isaya 54:13; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:12.
12. Tukiwa watumishi wa Yehova, tuna mataraja gani mazuri ajabu, lakini tunahitaji kufanya nini?
12 Ikiwa hangaiko letu kuu sasa ni lile la kumpendeza Mungu na kufanya mapenzi yake, kweli kweli tuna mataraja mazuri sana. (Zaburi 40:8; Warumi 12:1, 2) Hakika, ikiwa ‘tunamwogopa Yehova, kuna wakati ujao kwa ajili yetu na tumaini letu halitakatiliwa mbali.’ (Mithali 23:17, 18, NW) Tutapewa uzima wa milele tukiendelea kutembea kwenye “kijia cha uzima” tukiwa tunamwogopa Mungu. (Zaburi 16:11, NW) Hata hivyo, tukiwa njiani, tunahitaji kuweka na kufikia miradi ya kitheokrasi inayofaa.
Miradi Fulani Inayofaa
13. (a) Kimaandiko, kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba ibada ya Yehova imeendelea kuinuliwa? (b) Kwa njia fulani, baadhi ya miradi ambayo mamia ya maelfu wamefikia ni gani?
13 Wengine ndipo wameanza tu tunachoweza kuita kukwea kwao ‘mlima wa nyumba ya Yehova.’ Tangu miaka ya vita ya 1914-18 ibada ya Yehova, ambaye hekalu au ‘nyumba’ yake wakati mmoja ilikuwa juu ya mlima katika Yerusalemu, imeendelea kukwezwa. ‘Imewekwa imara juu ya milima’ ambayo juu yake mahekalu ya miungu ya uongo yamejengwa. Kwa hiyo ibada ya Yehova ‘imeinuliwa juu ya vilima.’ Umati mkubwa unamiminika kwenye ibada ya Yehova iliyoinuliwa juu. (Mika 4:1-4; Isaya 2:2-4) Baada ya kutwaa maarifa sahihi ya Maandiko, wanatubu, wanageuka, na kujiweka wakfu kwa Mungu katika sala na kuonyesha hilo kwa kuzamishwa majini. (Yohana 17:3; Matendo 2:38; 3:19) Kwa njia fulani, hiyo ni miradi inayofikiwa na mamia ya maelfu ya watu kutoka mataifa yote, ambao baada ya hapo wanamtumikia Yehova kwa uaminifu wakiwa sehemu ya tengenezo lake la kidunia. Wao ni wenye furaha kama nini kushiriki katika ibada iliyokwezwa ya Mungu mmoja wa kweli! Lakini namna gani wewe? Je! wewe umekwisha kuchukua hatua hizo?
14. Hata tukiisha kuanza kumwabudu Yehova, tunapaswa kusonga kuelekea nini, na hilo linaweza kufanywaje?
14 Hata tukiisha kuanza kumwabudu Yehova pamoja na watu wake, tunahitaji kusitawisha na kudumisha hamu nzuri ya chakula cha kiroho. Tukiwa tumekwisha kujifunza “fundisho la msingi juu ya Kristo,” tunapaswa kusonga “mbele kwenye kukomaa” kwa kutumia kwa faida yetu maandalizi yote ya kiroho ambayo Yehova anatoa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Waebrania 6:1-3, NW; Mathayo 24:45-47) Kwa hiyo kwa kufaa huenda ukajiuliza hivi: Je! mimi ninasoma Neno la Mungu kwa ukawaida? Je! mimi ni mwanafunzi mzuri wa vichapo vinavyotolewa kupitia jamii ya “mtumwa”?—Waebrania 5:11-14.
15. (a) Paulo alitoa shauri gani kwenye Waebrania 10:24, 25, lakini wengine wamekuwa wakifanya nini? (b) Ikiwa kuna nafasi ya kufanya maendeleo ya kibinafsi katika kuhudhuria mikutano au katika huduma ya Kikristo, ni jambo gani linalopendekezwa?
15 Halafu, pia, tunapaswa kutii shauri la Paulo: “Na tuhangaikie kila mmoja mwenzake, kuchochea itikio katika upendo na kazi njema. Msikose mikutano ya jumuiya, kama wengine wanavyofanya, bali tianeni moyo mmoja na mwenzake ili mwende; zaidi mfanye hivyo mwonapo Siku hiyo ikikaribia.” (Waebrania’10:24, 25, The Jerusalem Bible) Hudhurio la ukawaida kwenye mikutano ya Kikristo ni sehemu ya “ibada takatifu” yetu. Lakini wengine wanahudhuria hotuba ya watu wote tu kila juma, kwa kawaida wakitoka kwenye Jumba la Ufalme kabla ya funzo la Mnara wa Mlinzi kuanza. Wengine wanakosa Mkutano wa Utumishi. Je! umekuwa wenye maana ndogo kwao kwa sababu hawatendi sana katika kazi ya kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba na sehemu nyingine za huduma ya Kikristo? Ukiona kuna nafasi ya kufanya maendeleo ya kibinafsi katika yo yote ya sehemu hizo, sababu gani usisali kwa Yehova juu ya mambo hayo, na kumwomba akusaidie uwe wa kawaida na uwe mfano mwema katika mambo hayo yote ya “ibada takatifu”?—Waebrania 12:25-29, NW.
16. (a) Ni miradi gani ya kitheokrasi inayofaa ambayo inatajwa humu? (b) Hata ikiwa madaraka ya Kimaandiko yanazuia mtu asifikie makusudio hayo, bado inawezekana kufanya nini?
16 Miradi mingine ya kitheokrasi inayofaa ni gani? Daima kuna hesabu yenye kuongezeka ya watu ambao sasa wanashiriki katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia wa kawaida au wasaidizi. Je! wewe ungeweza kupanua huduma yako katika njia hizo? Bila shaka, hata ikiwa madaraka yako ya Kimaandiko yanakuzuia usifikie makusudio hayo, unaweza kuunga mkono wahubiri wa wakati wote huku wewe binafsi ukifanya mengi katika utumishi wa Mungu kwa kadiri hali zako zinavyoruhusu. Kwa ibada na utumishi wa uaminifu kwa ajili ya sifa ya Yehova, sisi sote tunaweza kuonyesha kwamba tunaweka ‘tumaini letu si juu ya utajiri usio yakini bali juu ya Mungu.’ Na kwa wale wanaoweza kushiriki katika kazi ya painia, hakika hiyo ndiyo mojapo njia bora zaidi ya kupata “uzima ulio kweli kweli.”—1 Timotheo 6:17-19.
17. (a) Vijana hasa wanaweza kufikiria pendeleo gani la utumishi? (b) Washiriki wa jamaa za Betheli wanapata uradhi gani?
17 Kutumikia katika mojapo makao ya Betheli ulimwenguni pote pia ni pendeleo zuri sana, pendeleo ambalo vijana hasa wanaweza kulifikiria kwa njia ya sala. Utumishi wa Betheli unatoa mazoezi mazuri sana katika kuwa na uhusiano mzuri na wanadamu, kwa maana wafanyi kazi wa Betheli wanashirikiana karibu karibu ili kusogeza mbele faida za Ufalme. Ufundi fulani unaositawisha katika Betheli waweza kuwa wenye manufaa sana katika kazi kubwa sana ya kufundisha itakayofanywa katika Utaratibu Mpya. Bila shaka, kwa kuwa wengi wanaingia katika utumishi wa Betheli mapema maishani, hawana vitu vingi vya kimwili. Lakini wanaridhika na chakula na mavazi na wana uradhi mkubwa wa kujua kwamba kazi yao inawafaidi wengine wengi kiroho.—Mhubiri 3:12, 13.
18. Kushiriki katika utumishi wa wakati wote kunaweza kumfundisha mtu nini, na jambo hilo linaungwaje mkono na Maandiko?
18 Kushiriki katika sehemu mbalimbali za utumishi wa wakati wote kwaweza kumfunza mtu amtegemee Yehova Mungu zaidi. Walimwengu wanaotumaini “utajiri usio yakini” mara nyingi wanakuwa na maoni kwamba ni lazima mtu ajiangalie yeye mwenyewe. Lakini hasa mhudumu wa wakati wote anajifunza kwamba Yehova anatoa uandalizi wa kutosha kwa wale wanaotafuta “kwanza ufalme wake, na haki yake.” (Mathayo 6:25-34) Maelfu ambao wametumikia wakiwa mapainia kwa miaka mingi watashuhudia uhakika wa kwamba hawajapata kamwe kukosa mambo ya lazima maishani. Zungumza na wao na utaona kwamba wanakubaliana kwa moyo wote na mtunga-zaburi Daudi, ambaye alitangaza hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zaburi 37:25.
Jenga Wakati Ujao Salama
19, 20. (a) Kwa kuwa wakati ni mfupi sana kwa mfumo wa mambo huu, sisi tunapaswa kuwa tukifanya nini? (b) Kwa hiyo tunaweza kutendaje kwa hekima kuhusiana na wakati ujao?
19 Ikiwa sisi ni mashahidi washikamanifu wa Yehova, tunatambua kwamba wakati uliobaki kwa mfumo huu ni mfupi sana. Kwa hiyo sisi tunapaswa kuwa tukifanya nini? Tunapaswa kuwa tukitenda kwa hekima kwa kupatana na maneno haya ya mtume Petro: “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, mkingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia kwayo mbingu zikiwa katika moto zitafumuliwa na vitu vya asili vikiwa na moto mwingi sana vitayeyuka!—2 Petro 3:11, 12, NW.
20 Pia, mtume Yohana alionyesha wazi kwamba ulimwengu huu unapita. (1 Yohana 2:15-17) Karibuni, mfumo huu wa kale utaangamia. Kwa hiyo, wale wote wanaomwogopa Mungu sasa wanapaswa kuwa wakishiriki ‘vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, wakingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ Usisahau kamwe kwamba ni tengenezo la Mungu tu litakalookoka mwisho wa mfumo huu unaokufa. Basi, tenda kwa hekima, na kufanya mipango ya uzima wa milele kwa kujenga wakati ujao wako pamoja na tengenezo la Yehova.—Kutoka w7/15/84.
Kwa Kurudia
◻ Wote wanaomwogopa Yehova wanafanyiza nini, na Mithali 23:17, 18 inawapa uhakikisho gani?
◻ Ni tengenezo jipi peke yalo lililo na wakati ujao, na kwa sababu gani unajibu hivyo?
◻ “Dhiki kubwa” ikiwa inakaribia sana, hangaiko kuu la Mashahidi wa Yehova lapasa kuwa nini?
◻ Baadhi ya miradi ya kitheokrasi ambayo wengi wanaweza kufikia ni gani?
[Blabu katika ukurasa wa 14]
Leo, wote wenye kumwogopa Mungu kweli kweli wana Yesu akiwa Mchungaji wao na wanatumikia pamoja katika umoja wakiwa tengenezo la kidunia la Yehova
[Blabu katika ukurasa wa 16]
Je! wewe unatengeneza wakati ujao wako na tengenezo la Yehova? Utendaji wa painia na utumishi wa Betheli ni kati ya miradi ya kitheokrasi ambayo wengi wamefikia
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kwa sababu ya baraka za kimungu kuwa juu ya kazi ya kuhubiri Ufalme, watu wengi wanamiminika kwenye ibada ya Yehova iliyoinuliwa