Panga Kimbele!
1 Tengenezo la Yehova huandaa programu ya kawaida ya utendaji wa kitheokrasi ambayo imekusudiwa kutosheleza mahitaji yetu ya kiroho. Uthamini hutusukuma kujinufaisha kikamili na kila jambo lililopangwa, kama vile ziara za mwangalizi asafiriye, makusanyiko na mikusanyiko, na utendaji mwingineo wa pekee tuliopangiwa. (Mt. 5:3) Hata hivyo, watu fulani hukosa manufaa za maandalizi haya mengi ya kiroho kwa sababu ya mipango mingine ambayo wamefanya. Ni jambo gani liwezalo kufanywa ili kuzuia hilo? Twaweza kuhakikishaje kwamba shughuli zisizo za kitheokrasi haziingilii “mambo yaliyo ya maana zaidi?”—Flp. 1:10.
2 Mpango Wenye Hekima Ni Muhimu: Mithali 21:5, Biblia Habari Njema, hutuonya kwa upole hivi: “Mipango ya mtu wa bidii huleta mali kwa wingi [“faida,” NW], lakini kila aliye na pupa huishia patupu.” Ili kupata “mali kwa wingi [“faida,” NW]” ya kiroho, twahitaji kupanga kimbele kwa bidii, tukikumbuka utendaji wa kitheokrasi ambao umepangwa. Twapaswa kupangia shughuli zetu za kibinafsi wakati ambao hautaingilia kuwapo kwetu ili tupate baraka za kiroho. Tukiharakisha kupanga mambo tunayotaka kuyafanya kibinafsi, bila kufikiria matukio yajayo ya kitheokrasi, yaelekea kwamba tutakuwa “patupu” kiroho.
3 Usikose Manufaa! Sisi sote hufanya mipango ya wakati ujao, kutia ndani likizo, safari za kibiashara, kutembelea watu wa jamaa, na kadhalika. Kabla ya kujiingiza au kukamilisha mipango yako, angalia ratiba uone utendaji ufuatao wa kiroho. Ukiona kwamba mwangalizi wa mzunguko anakuja au kusanyiko limepangwa wakati uleule ambao huenda ukawa hauko, jitahidi kupanga tena mambo yako ili uweze kushiriki. Twajulishwa mapema juu ya matukio makubwa yaliyo katika ratiba ya wakati ujao. Wazee katika kutaniko lako wanaweza kukuambia mambo ambayo yamepangwa kwenu.
4 Kwa kuona kimbele na kupanga kimbele mambo yaliyo ya maana zaidi, ‘tutajazwa matunda ya uadilifu, . . . kwa utukufu na sifa ya Mungu.’—Flp. 1:11.