Kuweka Kando Wakati kwa Ajili ya Maandalizi ya Kitheokrasi
1 Yehova amekuwa mkarimu sana katika kutimiza ahadi zake kwa kufanya hekima ya kimungu ipatikane kwa watumishi wake leo. (Isa. 55:1; Dan. 12:4; Rum. 11:33; 1 Kor. 2:8-10) Je! sisi tunaweka kando wakati ili kupata faida kamili ya programu yake ya kutufundisha sisi katika njia ya ukweli?
2 Inahitaji jitihada fulani na kujiweza kwa upande wetu ili tuweke kando wakati unaofaa kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kujitayarishia mikutano. Lakini je! hatuhisi tukiwa tumeburudika, ndiyo, tumethawabishwa sana, tunapoukomboa wakati unaohitajiwa sana kila juma kwa ajili ya elimu ya kitheokrasi? (Efe. 5:15-17) Ni nini mengine ya maandalizi ya ajabu ambayo Yehova ametufanyia sisi ili kutufundisha?
KILE AMBACHO YEYE AMEPANGA
3 Jambo la kwanza kabisa, tuna Biblia ambayo ni kitabu chetu kikubwa cha mafundisho. Programu nzuri ya usomaji wa Biblia imeratibiwa kwa kila juma. Je! sisi tunafuatana nayo? Je! kuna uhitaji wa kuweka wakati kando kwa ajili ya hiyo katika ratiba yetu ya kibinafsi?
4 Je! kuna jambo zaidi linalohitajiwa, au je! kusoma Biblia kunatosha? (Yak. 1:5, 6) Tunahitaji pia tengenezo lionekanalo ambalo Yehova anatumia kututolea wingi wa chakula cha kiroho kwa ukawaida. “Chakula [hiki cha kiroho] kwa wakati wake” kinatolewa kwa namna ya vichapo vinavyotegemea Biblia, mipango ya mikutano ya kundi, makusanyiko ya mzunguko, na mikusanyiko ya wilaya.—Mt. 24:45.
5 Mwingine wa maandalizi ya Yehova wa kupata elimu ya kitheokrasi ni ule wa wachungaji wenye upendo. (Mdo. 20:28) Wanapotutembelea, huenda wazee wakawa na habari mahususi ambayo wanataka kuzungumzia. Je! sisi tuko chonjo kutumia mara moja madokezo wanayotoa? Waangalizi wenye kudhamiria wanajifunza kwa bidii yenye kuendelea ili kwenda sambamba na tengenezo. (2 Tim. 2:15) Wao wanatambua kwamba wana daraka zito mbele za Yehova kulisha na kulipa kundi himaya. Sisi sote tunaweza kunufaika na ujuzi wao na wakati wanaotumia kwa ajili yetu.
KUWASAIDIA WATOTO WETU NA WENGINE
6 Kuwafundisha watoto wetu katika kweli ni upande wa maana sana wa elimu ya kitheokrasi. Wazazi Wakristo hawalioni kuwa jambo tu la hiari ya watoto wao. Kutoa “nidhamu na rekebisho la akili” kwa ustadi ni jambo la maana sana. (Efe. 6:4, NW) Mara nyingi kunaonyesha tofauti kati ya ukuzi wao kuelekea ukomavu wa kiroho au kuacha ukweli kabisa. Wakati unahitajiwa kwa agizo hili. Hakuna badala.
7 Wapya wanaweza kusaidiwa wathamini ubora wa wakati wanaoweka kando kwa ajili ya funzo lao la Biblia la kila juma. Tunapaswa kuwatia moyo wajitayarishe vizuri kwa ajili ya kila funzo. Tangu mwanzo tunataka ‘wafunzwe neno’ kikamili. (Gal. 6:6, NW) Tukifanya sehemu yetu katika kuwafunza, hautachukua muda mrefu kabla hawajaanza kushiriki nasi katika kazi ya kueneza evanjeli wakiwa na hamu nyingi. Elimu ya kitheokrasi haifikii ukomo wanapojifunza “mambo ya msingi.” (Ebr. 5:12–6:3, NW) Tunataka tuwasaidie “wakaze mwendo kuelekea ukomavu.” Hii inachukua wakati.
8 Haya ni machache ya maandalizi ya Yehova kwa ajili ya kutufundisha kile tunachohitaji. Maandalizi mengine ni ziara ya mwangalizi wa mzunguko, Shule ya Utumishi wa Painia, na Shule ya Huduma ya Ufalme.
9 Shukrani zote zinapasa kumwendea Yehova kwa kuandaa elimu ya pekee ambayo itatupa himaya na kutuongoza kupitia siku hizi za mwisho. Na tupige moyo konde ili tuweke wakati kando ili kufaidika kikamili na maandalizi ya kitheokrasi ambayo Mkufunzi Mtukufu wetu ametufanyia. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunapofanya hivyo, tutazidi kufanya maendeleo katika njia ya uhai wa milele.—Isa. 30:20, 21; Flp. 3:13-16.