“Tumehubiri Eneo Letu Mara Nyingi Sana!”
1 Je, umewahi kuhisi kwamba mmehubiri eneo lenu mara nyingi sana hivi kwamba hakuna watu walio mfano wa kondoo tena? Labda umewazia hivi: ‘Najua vile ambavyo watu wataitikia. Kwa nini niendelee kurudi kwa watu wasiopendezwa?’ Ni kweli kwamba maeneo mengi yanahubiriwa mara nyingi. Hata hivyo, jambo hilo lapaswa kuonwa kwa njia inayofaa, si kwa njia isiyofaa. Kwa nini? Angalia sababu nne zinazotolewa hapa chini.
2 Sala Zetu Zimejibiwa: Yesu alisema: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:2) Tumekuwa tukimwomba Yehova dua kwa miaka mingi atupe msaada zaidi. Katika sehemu nyingi, sasa tuna wafanyakazi zaidi, na twahubiri eneo mara nyingi zaidi. Je, hatupaswi kufurahi kwamba Yehova amejibu sala zetu?
3 Kuendelea Huleta Matokeo Bora: Hata katika maeneo yenye kuhubiriwa mara nyingi, watu wanakubali ujumbe wa Ufalme na wanapata ujuzi wa ile kweli. Kwa hiyo twapaswa kuendelea kuwahubiria tena na tena tukitumaini kupata watu wengine wenye mioyo minyofu. (Isa. 6:8-11) Kama vile wanafunzi wa kwanza wa Yesu walivyofanya, ‘nenda kwa kuendelea’ kwa watu katika eneo lenu, ukijitahidi kuwachochea wapendezwe na Ufalme wa Mungu.—Mt. 10:6, 7.
4 Katika Ureno, makutaniko mengi huhubiri eneo lao kila juma, lakini bado wanapata watu walio mfano wa kondoo. Dada mmoja hasa ana mtazamo unaofaa. Yeye anasema hivi: “Kila asubuhi kabla ya kwenda katika utumishi wa shambani, mimi humwomba Yehova anisaidie nipate mtu mwenye kupendezwa kujifunza Biblia.” Siku moja alipanga kujifunza na wafanyakazi wa saluni. Ingawa hivyo, baadaye ni mtu mmoja tu aliyekubali kujifunza. Mtu huyo alisema hivi: “Wale wengine hawapendezwi, lakini mimi napendezwa.” Kwa muda wa mwezi mmoja tu alikuwa akiongoza mafunzo mawili ya Biblia. Upesi baada ya hapo, akabatizwa, na baadaye akawa painia!
5 Kazi Inafanywa: Habari njema yahubiriwa, kama vile Yesu alivyotabiri. (Mt. 24:14) Hata mahali ambapo watu “hawataki ku[tu]sikiliza” wanapata onyo kupitia kazi ya kuhubiri. Twatazamia wengine wasisikilize au hata wapinge kweli. Hata hivyo, watu kama hao lazima waonywe vilivyo juu ya hukumu inayokuja kutoka kwa Yehova.—Eze. 2:4, 5; 3:7, 8, 19.
6 Hatujakamilisha Bado: Si juu yetu kuamua wakati wa kuacha kuhubiri. Yehova anajua wakati barabara wa kumaliza kazi hiyo. Anajua kama kungali na watu katika eneo letu ambao huenda wakakubali habari njema. Leo, watu fulani husema kwamba hawapendezwi, lakini mabadiliko katika maisha yao—ukosefu wa kazi, ugonjwa mbaya, kifo cha mpendwa wao—huenda yakawafanya wapendezwe wakati mwingine. Kwa sababu ya ubaguzi au kwa sababu tu ya kuwa na shughuli nyingi, kwa kweli watu wengi hawajasikia kamwe yale tunayohubiri. Kuwatembelea kirafiki mara kwa mara huwafanya watambue na kusikiliza.
7 Wale ambao wamekua wakubwa kiumri miaka ya hivi karibuni na ambao sasa wana familia zao wenyewe wanachukulia maisha kwa uzito na kuuliza maswali ambayo Neno la Mungu tu linaweza kujibu. Mama mmoja mchanga alialika Mashahidi wawili nyumbani kwake na kusema: “Nilipokuwa msichana mdogo, sikuweza kuelewa kwa nini mama yangu aliwafukuza Mashahidi na kuwaambia kwamba hakupendezwa, na kile walichotaka tu ni kuzungumza juu ya Biblia. Niliamua kwamba nitakapokuwa mkubwa, niolewe, na kuwa na nyumba yangu mwenyewe, nitawaomba Mashahidi wa Yehova waje kuniambia juu ya Biblia.” Alifanya hivyo, na Mashahidi waliomtembelea walifurahi.
8 Je, Waweza Kuwa na Matokeo Hata Zaidi? Huenda ikawa si wale watu tunaotembelea wanaofanya eneo letu lionekane kuwa gumu tunapolihubiri mara nyingi. Nyakati nyingine ni sisi wenyewe. Je, sisi huanza kuhubiri tukiwa na mawazo yasiyofaa? Hilo laweza kuathiri mtazamo wetu na hata sauti yetu na sura yetu. Onyesha roho na sura yenye kupendeza. Jaribu utangulizi mpya. Tumia utangulizi mbalimbali na ujaribu kuuboresha. Labda unaweza kubadilisha swali lako au kutumia andiko tofauti katika mazungumzo. Uliza ndugu na dada wengine njia wanayoona kuwa yenye mafanikio katika eneo. Hubiri na wahubiri na mapainia mbalimbali, na uangalie ni jambo gani linalofanya huduma yao iwe na matokeo.
9 Yehova hubariki kazi ya Ufalme nayo hupata kibali chake. Tunapoishiriki tunaonyesha upendo tulio nao kwake na kwa jirani yetu. (Mt. 22:37-39) Kwa hiyo acheni twendelee na kazi yetu hadi mwisho wake, bila kuchoka kuhubiri eneo letu tena na tena.