Je, Una Eneo la Kibinafsi?
1 Eneo la kibinafsi ni lile ambalo umegawiwa. Linaweza kuwa mahali panapokufaa ili uweze kufika haraka na kuhubiri peke yako au ukiwa na mhubiri mwingine. Ingawa kuna manufaa ya kuunga mkono mipango ya kuhubiri pamoja katika kikundi, kuwa na eneo la kibinafsi la kuhubiri wakati mwingine kunaweza kusaidia kutoa ushahidi kamili, hasa katika makutaniko yaliyo na maeneo makubwa.—Mdo. 10:42.
2 Manufaa: Wengine wamepata manufaa zaidi wanapohubiri eneo la kibinafsi karibu na mahali wanapofanyia kazi wakati wa mapumziko ya mchana au moja kwa moja baada ya kazi. Wengine wamefurahia kuhubiri pamoja kama familia katika ujirani wao saa moja hivi kabla ya Funzo la Kitabu la Kutaniko. Marudio na mafunzo ya Biblia yanayopatikana huwa karibu na nyumbani, na hilo hufanya tusitumie nguvu nyingi, wakati, na gharama ambayo huenda ingetumika. Kwa kuwa mengi yanaweza kufanywa kwa wakati mfupi, kuwa na eneo la kibinafsi kunaweza kuwasaidia wengine kuwa mapainia-wasaidizi mara kwa mara au hata kuwa mapainia wa kawaida. Isitoshe, kuhubiri eneo la kibinafsi na kufahamiana na wenye nyumba kunaweza kuwafanya watuamini na hutusaidia kutoa utangulizi unaofaa hali zao. Hilo hufanya huduma yetu iwe na matokeo zaidi.
3 Painia mmoja ambaye alitiwa moyo na mwangalizi wa mzunguko awe na eneo la kibinafsi anaeleza hivi: “Nilikubali mashauri yake na baada ya muda nikafahamiana na wenye nyumba katika eneo langu na kufanya urafiki nao. Nilibadili wakati wangu na kuwatembelea walipopatikana. Kwa sababu hiyo, marudio yangu yakaongezeka kutoka 35 hadi 80 kwa mwezi, na nina mafunzo saba ya Biblia.”
4 Unaweza Kupataje Eneo la Kibinafsi?: Ukitaka kuwa na eneo la kibinafsi, mwambie mtumishi wa maeneo. Mwalike mhubiri mwingine ahubiri pamoja nawe, na uweke rekodi ya nyumba ambazo hakuna mtu anayepatikana. Unapaswa kukamilisha eneo hilo kwa miezi minne. Ikiwa ni vigumu kufanya hivyo, unaweza kuomba msaada kutoka kwa mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko au kutoka kwa wahubiri wengine. Miezi hiyo minne inapokwisha, unaweza kurudisha eneo hilo au kuomba ulifanyie kazi tena. Hata hivyo, usikae na eneo hilo milele bali ulirudishe ili wengine waweze kuliomba. Ikiwa kutaniko lenu halina maeneo mengi na haiwezekani kupata eneo la kibinafsi, labda unaweza kumwomba mwangalizi wa funzo lenu la kitabu sehemu fulani ya eneo.
5 Utume tuliopewa wa kuhubiri “katika dunia yote inayokaliwa” ni mgawo mkubwa ajabu. (Mt. 24:14) Tunahitaji kuwa na utaratibu mzuri sana. Zaidi ya kuhubiri katika vikundi, kuhubiri maeneo ya kibinafsi kunaweza kutusaidia kuwafikishia watu wengi inavyowezekana habari njema.
[Maswali ya Funzo]
1. Eneo la kibinafsi ni nini?
2. Tunaweza kupata manufaa gani kwa kuwa na eneo la kibinafsi?
3. Painia mmoja aliyepata eneo la kibinafsi alikuwa na matokeo gani?
4. Unaweza kupataje na kuhubiri eneo la kibinafsi?
5. Ni nini kinachohitajiwa ili tutimize utume wetu wa kuhubiri?