Timiza Huduma Yako Kikamili
1 Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Basi, enendeni, mkawafanye . . . wanafunzi, . . . kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20) Wanafunzi wa kweli wa Yesu leo wanaitikia kwa idili kazi hii yenye kuokoa uhai. Kwa habari ya wengi inaweza kusemwa kwamba ‘wanamiminwa juu ya dhabihu.’ sawa na ilivyosemwa kwa habari ya mtume Paulo. (Flp. 2:17) Kielelezo chao chenye kutia imani nguvu kinatutia sisi sote moyo tutimize huduma yetu kikamili.—2 Tim. 4:5; Ebr. 13:7.
2 Hata hivyo, jitihada zenye bidii za kutolea kila mtu ushuhuda katika eneo zinazuiwa nyakati nyingine kwa sababu ya hesabu kubwa ya watu wasiokuwa nyumbani tunapozuru. Kwa kuongezea, makundi fulani yana migawo ya eneo ambalo ni kubwa sana. Jambo hilo linafanya iwe vigumu kwao kueneza eneo mara kwa mara, kufuatia kupendezwa kikamili, au kurudia ili kuwapata wale wasiokuwa nyumbani. Wewe unaweza kufanya nini ili utimize huduma yako kikamili zaidi? Je! wewe umejaribu kukaza fikira zako kwenye sehemu za eneo ambazo zinathibitika kuwa zenye matokeo zaidi? Jaribu kufanyia kazi hizi kikamilifu mara kadhaa katika mwaka, huku ukihakikisha kwamba unaeneza eneo lote ulilogawiwa angalau mara moja kwa mwaka.
MATUMIZI YANAYOFAA YA MAANDISHI YA NYUMBA KWA NYUMBA
3 Ni jambo la maana sisi tuweke maandishi mazuri ya nyumba kwa nyumba na kuyatumia baadaye. Tunawezaje kutimiza huduma yetu kikamili ikiwa haturudi mahali ambako hakukuwa na mtu? Je! kweli tunaweza kusema kwamba tunaeneza eneo letu kikamilifu ikiwa tunakosa kurudia watu wanaopendezwa ambao tumekuta na kujitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja nao? Majibu kwa maswali haya yanatilia mkazo uhitaji wa kutumia vizuri maandishi ya nyumba kwa nyumba. Ni bora kuweka vikaratasi viwili, kimoja cha kupendezwa kulikopatikana na kingine cha anwani za watu ambao hawakupatikana nyumbani.
4 Wahubiri fulani wameliona kuwa jambo lenye mafaa kurudi kwenye nyumba ambazo hazikuwa na watu kabla ya kuondoka kwenye eneo. Kurudi saa moja au mbili baada ya ziara ya kwanza huenda kukatokeza kupata mtu fulani na kumwangushia kichapo au hata kuanzisha funzo la Biblia. Kwa habari ya makundi ambayo yana eneo dogo, kurudi ili kuwapata watu hao baada ya saa moja au mbili kunaongeza kiasi cha eneo linalopatikana na kunahakikisha uenezaji mzuri zaidi walo.
5 Wahubiri ambao hawawezi kurudi mara moja wanaweza kumpa kiongozi wao wa funzo la kitabu maandishi yao ya watu wasiopatikana nyumbani ili awape wahubiri wengine. Jambo hilo linaweza kupangwa ifaavyo mahali ambapo makundi yana vikundi vya kutoa ushuhuda vya katikati ya juma, mwisho-juma, na jioni. Bila shaka, huenda wahubiri fulani wakataka kuweka maandishi yao ya nyumba kwa nyumba na kufanya ziara fulani wanapoenda na kutoka shuleni, kazini, au kununua vitu au wanaposhughulikia mambo mengine yanayohitajiwa. Kundi moja ambalo liliwatia moyo akina ndugu wafanye hivyo lilipata matokeo mazuri, wakapata kupendezwa kuzuri katika sehemu moja ya eneo lao ambalo hapo mwanzoni halikuwa lenye matokeo.
6 Huduma yetu ina pande nyingi. Kuna mambo mengi tunayopaswa kufanya. Lakini kusudi la msingi la kazi yetu ni ‘kuhubiri neno.’ (2 Tim. 4:2) “Neno” hilo litatokeza mema kwa wale wanaolisikiliza. (Sef. 2:2, 3) Watu walio katika eneo letu wangali wanahitaji kupewa fursa ya ‘kuita juu ya jina la Yehova.’ (Rum. 10:11-13, NW) Na tujitahidi na kutafuta kila fursa ya kutimiza huduma yetu kikamili.