Endelea “Kufanya Lililo Bora”
1 Ulifanya jambo bora ulipoamua kuwa mtumishi wa Yehova Mungu. Hata hivyo, sasa ugumu uliopo katika nyakati hizi za hatari ni kuendelea “kufanya lililo bora.” (Gal. 6:9) Ijapokuwa hiyo yataka ujitahidi sana, unaweza kufaulu. Jinsi gani?
2 Sitawisha Mtazamo wa Akili wa Yesu: Kama vile Yesu, unaweza kuvumilia majaribu ukiendelea kukazia macho tumaini la Ufalme. (Ebr. 12:2, 3) Na uwe na uhakika kwamba Yehova anakupenda na kwamba anataka ufanikiwe. (2 Pet. 3:9) Mtumaini kabisa, ukiwa na uhakika kwamba atakusaidia. (1 Kor. 10:13) Dumu katika sala, ukimwomba Yehova akusaidie uvumilie. (Rom. 12:12) Ni shangwe kujua kwamba uvumilivu wako utaongoza kwenye hali ya kukubalika machoni pa Mungu. (Rom. 5:3-5) Uaminifu wako katika kusitawisha “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu” utakufanya uridhike na uufurahishe moyo wa Yehova.—Rom. 15:5; Mit. 27:11.
3 Endelea Kufanya Kazi Bora: Jinufaishe kikamili na maandalizi ambayo Yehova amewapa watu wake ili kuwasaidia waendelee kufanya yaliyo bora. Sitawisha ratiba nzuri ya kibinafsi ya kusoma Neno la Mungu na kujifunza vichapo vinavyozungumzia Biblia vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Endelea kutayarisha, kuhudhuria, na kushiriki mikutano yote ya kutaniko kwa uaminifu. Kabla na baada ya mikutano ya Kikristo, shirikiana sana na ndugu na dada zako wa kiroho. Weka miradi unayoweza kufikia katika huduma yako ili uweze kushiriki kikamili katika utumishi wa shambani na kuboresha ustadi wako wa kuwahubiria wengine habari njema.
4 Hivyo ndivyo unavyoweza kuendelea kufanya lililo bora na upate shangwe kubwa sana vilevile. Kuhusiana na hilo, ndugu mmoja kutoka Italia alisema: “Jioni inapofika, nami narudi nyumbani baada ya kushinda mchana-kutwa katika utumishi wa Yehova, kwa kweli najisikia nimechoka. Lakini nina furaha, na namshukuru Yehova kwa kunipa shangwe ambayo hakuna mtu yeyote awezaye kuninyang’anya.” Vivyo hivyo, endelea kufanya lililo bora nawe pia utakuwa na shangwe kubwa.