Usisite-Site!
1 Huenda sisi wenyewe tukawa kizuizi kikubwa, tunapojitayarisha kwenda kuhubiri mlango hadi mlango. Huenda tukasita-sita kuhubiria “watu wa namna zote” kwa sababu ya kuhisi kwamba hatustahili. (1 Tim. 2:4) Lakini hatupaswi kusita-sita kuhubiri habari njema. Kwa nini?
2 Ni Ujumbe Kutoka kwa Yehova: Yehova amewasilisha neno lake kupitia Biblia. Tunapowapelekea wengine ujumbe huu, tunawasilisha mawazo yake, wala si yetu. (Rom. 10:13-15) Watu wanapokataa ujumbe wa Ufalme, hawatukatai sisi bali wanamkataa Yehova. Hata hivyo, hatuvunjiki moyo. Tuna uhakika kwamba ujumbe huo utavutia mioyo ya wale wanaotamani kuona mabadiliko katika hali za ulimwengu na ambao wanahangaikia uhitaji wao wa kiroho.—Eze. 9:4; Mt. 5:3, 6.
3 Yehova Ndiye Huvuta Watu: Huenda mtu ambaye alikataa kutusikiliza awali akakubali sasa kwa sababu hali zake zimebadilika na moyo wake umekuwa mzuri. Huenda sasa Yehova akamwonyesha wema wake na ‘kumvuta.’ (Yn. 6:44, 65) Jambo hilo litukiapo, twataka kuwa tayari kutumiwa na Yehova na kuitikia mwelekezo wa malaika wa kutafuta watu kama hao.—Ufu. 14:6.
4 Mungu Hutupa Roho Yake: Roho takatifu hutuwezesha kusema kwa “ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.” (Mdo. 14:1-3) Tukikumbuka kwamba tuna utegemezo huo wenye nguvu katika huduma yetu, hatutasita-sita kuwaambia kweli majirani wetu, wafanyakazi wenzetu, wanadarasa wenzetu, watu wetu wa ukoo, au watu wenye elimu ya juu au matajiri.
5 Yesu Alitufundisha Jinsi ya Kuhubiri: Yesu alitumia maswali yenye kuamsha fikira, mifano yenye kueleweka, na sababu za Kimaandiko. Alieleza kweli kwa njia rahisi, yenye kuvutia, kutoka moyoni mwake. Hizo zingali njia bora zaidi leo. (1 Kor. 4:17) Huenda tukahubiri katika hali mbalimbali, lakini ujumbe wenye nguvu wa Ufalme ni uleule tu.
6 Tuna pendeleo la kutumiwa na Yehova kusaidia watu katika njia ya pekee na muhimu. Tusisite-site! Na tuwe jasiri na tumruhusu Yehova apate “kutufungulia mlango wa kutamka” ili tuwaambie wengine habari njema.—Kol. 4:2-4.