Namna ya Kuwa Wahudumu Wenye Matokeo
“Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu, aliye mwanangu mpendwa, mwaminifu katika Bwana, [kwa maana atawakumbusha] njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila kanisa.”—1 WAKORINTHO 4:17.
1, 2. Ili mtu avutwe kwenye ukweli, jambo moja linalohitajiwa sana ni nini? (Matendo 8:12)
ROHO takatifu ilipomiminwa wakati wa Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., kundi la Kikristo lilikua likaenea kwa haraka sana. (Matendo 2:40-42; 4:4; 6:7; 11:19-21) Kilichofanya lipate mafanikio ni nini? Kwa sababu gani Wayahudi wengi sana kisha Wasamaria na Mataifa walikubali Kristo na ujumbe wa Ufalme wa Mungu?—Matendo 8:4-8; 10:44-48.
2 Ili mtu akubali habari njema za Kikristo, ni lazima mambo fulani yahusike. Kwanza, ni lazima athamini fadhili zisizostahilika ambazo Mungu alionyesha kuelekea wanadamu kwa kuchukua hatua ya kwanza kutuma Mwanaye duniani awe dhabihu ya ukombozi. Ni kama vile Yohana mwandikaji wa Biblia alivyoeleza: “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.”—1 Yohana 4:9, 10.
3. Kwa sababu gani ni lazima mtu aone uhitaji wake wa kiroho?
3 Jambo jingine la maana sana ni nia ya kila mtu kuelekea faida za kiroho. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao. Wenye furaha ni wale wanaoona njaa na wanaoona kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watajazwa.” (Mathayo 5:3, 6, NW) Kwa kawaida mwenye kinaya, mwenye kujihesabia uadilifu mwenyewe haoni uhitaji wo wote wa kiroho na hataki tena kusikiliza ukweli. Anapotolewa ujumbe wa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi mtu wa namna hiyo atajibu, ‘Mimi sipendezwi. Nina dini yangu mwenyewe.’ Vivyo hivyo, mtu anayejitia sana katika shughuli za utafutaji wa mali hatakuwa na wakati wa mambo ya kiroho.—Mathayo 6:33, 34; 7:7, 8; Luka 12:16-21.
4. Sasa ni maulizo gani yatakayofikiriwa?
4 Lakini namna gani wale “wanaoona uhitaji wao wa kiroho” ambao wako tayari kutafuta Mungu na Ufalme wake? Wanaweza kupatikana na kutambuliwa kwa njia gani? Je! kuna lo lote ambalo sisi wahudumu wa Neno la Mungu tunaweza kufanya ili ujumbe wetu ueleweke zaidi? Tunaweza kuwaje wahudumu wenye matokeo zaidi?
Tunapaswa Kutumia Njia za Nani?
5. Kulingana na Paulo, Timotheo angefundisha Wakorintho nini?
5 Wakati mtume Paulo alipoandikia Wakristo wa Korintho barua yake ya kwanza, aliwaambia angewapelekea Timotheo, ambaye ‘angewakumbusha njia zake zilizo katika Kristo.’ Badala ya kusema “njia,” tafsiri nyingine zinataja “njia za kuishi,” “njia ya maisha” au “njia ambayo mimi naishi.” Lakini, Greek-English Lexicon of the New Testament ya Profesa Thayer inatoa fasiri hii juu ya andiko hilo: “Njia za kutendea ambazo mimi niliye mhudumu na mtume wa Kristo nafuata katika kutekeleza cheo changu.” Kwa kuwa Paulo anamalizia sentensi kwa kusema, “kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila [kundi],” ni jambo la akili kukata maneno kwamba maneno yake yanahusu pia huduma yake yenye utendaji wala si mwenendo wake wa Kikristo tu.—1 Wakorintho 4:17.
6. Kwa sababu gani huduma ya Yesu ilikuwa na matokeo?
6 Huduma ya Yesu haikufanywa shaghalabaghala (ovyoovyo). Alitumia mpango pia katika mahubiri yake. Kwa mfano, yeye aliwafundisha mitume wake kwa uangalifu, na baadaye wale waeneza-evanjeli 70, namna ya kuhubiri kwa matokeo. Matumizi yake mwenyewe ya mifano, maswali na mitajo ya Maandiko yalikuwa mfano wa kufuatwa nao. Hiyo ingali ndiyo njia bora zaidi leo.—Luka 9:1-6; 10:1-11.
7. Tunaweza kuelezaje watu wengi iwezekanavyo habari njema?
7 Kwa kuwa huduma ya Kikristo ni jambo linalohusu uzima wa milele au kifo cha milele, tunaweza kupelekaje habari njema kwa watu walio wengi kabisa? Ni kwa njia gani tunaweza kuwa ‘hatuna hatia kwa damu ya mtu awaye yote’? Ni kwa kutumia kila njia ya utumishi. Kama mtume Paulo alivyosema, hiyo inatia ndani huduma ya “nyumba kwa nyumba.” Kitabu kimoja cha Kispania chenye maelezo yanayohusu Matendo 20:20 kinasema: “Hiyo ndiyo njia ya kuhubiri ambayo Paulo alifuata katika Efeso.”—Matendo 20:20-27.
Kizuizi cha Kwanza
8, 9. (a) Mara nyingi kizuizi cha kwanza katika huduma kinakuwa nini? (b) Kwa sababu gani Yesu aliweza kusema kwa ujasiri?
8 Mara nyingi sana kizuizi cha kwanza tunachohitaji kushinda katika huduma ni sisi wenyewe. Wengine wana maelekeo ya kujifikiria, kujisikia hawastahili sana na hawana elimu ya kutosha ili kuweza kukabiliana na watu wanaowakuta. Lakini Yesu alikuwa na maoni gani? Je! alikuwa amehudhuria shule za walimu wa kidini? Je! alikuwa na elimu ya juu? Lakini alipohubiri, watu wake mwenyewe walionaje? Mathayo anatuambia: “Wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii?” Ni kweli kwamba Yesu alikuwa mkamilifu, Mwana wa Mungu. Lakini njia alizotumia zilikuwa zenye mafaa pia kwa wanafunzi wake ambao hesabu kubwa kati yao walikuwa “watu wasio na elimu” waliopaswa kufuata mfano wake. Walichochea maoni gani, hata kati ya adui zao wa kidini? “Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”—Mathayo 13:54; Matendo 4:13.
9 Lakini, Yesu alipata wapi mambo yote hayo aliyofunza? Kwa sababu gani alipata mafanikio mengi katika huduma yake? Je! yeye alisisimuka kupita kiasi kama wahubiri wa kisasa wanaotumia televisheni ili kuvuta wasikilizaji? Hapana. Msingi wa Yesu ulikuwa kusema kwa njia ya kueleweka vyepesi—alitumia usemi wa watu wa kawaida, alijua mahitaji yao ya kiroho na, jambo la maana kuliko yote, Yesu alitegemezwa na Baba yake. Alielewesha wazi jambo hilo alipotangaza agizo alilopewa la kufanya huduma alipokuwa katika sinagogi la mji wa nyumbani kwao, Nazareti katika Galilaya. Alisoma hivi katika kitabu cha kukunja cha nabii Isaya: “Roho [ya Yehova i] juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa [Yehova] uliokubaliwa. . . . Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu.”—Luka 4:16-21.
10, 11. (a) Inatupasa tuwe na maoni ya namna gani juu ya huduma yetu? (b) Paulo anajibuje?
10 Leo tuna tegemezo lile lile katika huduma yetu—Yehova Mungu, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Tunahubiri ujumbe wake, hekima yake. Sisi wenyewe tunategemea Neno lake na tunalitumia sana katika mazungumzo yetu. Basi, je! tunapaswa kujiona kwamba hatufai kuwahubiri hata watu wenye elimu au utajiri mwingi kuliko sisi?
11 Paulo anajibu hivi: “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? . . . Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”—1 Wakorintho 1:18-29.
12. Mafanikio katika huduma yetu yanatokana na nini? (Yakobo 4:8)
12 Mafanikio katika huduma hayatokani na elimu yetu wala ukoo wetu. Yanatokana na ujumbe wa Ufalme wenyewe ambao unavuta itikio katika moyo wa mtu anayeona uhitaji wa kiroho. Jambo jingine linaloleta mafanikio ni nia njema ya Yehova kuelekea mtu huyo, kwa maana kama vile Yesu alivyosema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka.”—Yohana 6:44.
13. (a) Paulo na Barnaba waliitikiaje upinzani? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuwa na furaha sikuzote katika huduma?
13 Basi, tukitumainia tegemezo la Yehova, tunaweza kuendesha huduma yetu kwa usadiki kama Paulo na Barnaba katika karne ya kwanza. Walipohubiri katika Ikonio, huduma yao ilileta utofautiano mkubwa wa maoni ya watu na upinzani fulani. Je! walilegeza mwendo kwa sababu hiyo? Masimulizi ya Luka yanatuambia: “Wakakaa huko wakati mwingi, wakinena kwa ushujaa katika [Yehova], aliyelishuhudia neno la neema yake, akiwajalia ishara na maajabu yatendeke kwa mikono yao.” Nasi pia tukiwa na maoni yanayofaa kuelekea watu katika eneo letu, kisha tuache matokeo mikononi mwa Yehova, sikuzote huduma itakuwa jambo la furaha, si la mzigo.—Matendo 14:1-3; Yakobo 1:2, 3.
Namna Watu Wanavyoitikia
14. Watu waliitikiaje mahubiri ya Paulo?
14 Walipokuwa wakihubiri, wala Yesu wala Paulo hawakuitikiwa vizuri sikuzote. Kwa mfano, watu wengi waliitikiaje wakati Paulo alipohubiri katika Athene? Masimulizi yanatuambia: “Baadhi ya Waepikureo na Wastoiko, wenye ujuzi, wakakutana naye. Wengine wakasema, Mpuzi huyu anataka kusema nini? Wengine walisema, Anaonekana kuwa mtangaza habari za miungu migeni, kwa maana alikuwa akihubiri habari za Yesu na ufufuo. Wakamshika, wakamchukua Areopago, wakisema, Je! twaweza kujua maana ya elimu hii mpya unayoinena? Kwa maana unaleta mambo mageni masikioni mwetu.”—Matendo 17:18-20.
15. Watu wanaitikiaje huduma yako wewe? Lakini inatupasa tukumbuke nini?
15 Inatupasa tujue kwamba huenda pia ujumbe wetu ukasikika na watu wa kisasa kuwa wa kigeni kwa sababu ya vile unavyoelezwa na vyombo vya utangazaji wa habari. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanatangulia kufanya uamuzi juu ya jambo hilo na kutukataa kabla ya sisi kuwaeleza kwa maana uvumi unakuwa umewapa maoni mabaya. Wengine, kama Waathene wale, wanakubali kupewa habari zaidi kabla ya kufanya uamuzi. Bila shaka, wakiisha kusikiliza huenda bado wakadhihaki tumaini la Ufalme kuwa lisiloaminika. Hata hivyo, kumbuka kwamba wanapofanya hivyo wanamkataa Kristo na ujumbe wake, si wewe.—Matendo 17:32-34; Mathayo 12:30.
Tunaacha Kuwa Watu Wasiojulikana na Kuwa Rafiki
16. (a) Huenda tukaitikiaje watu tusiowajua wakitutembelea nyumbani? (b) Utangulizi wetu unapasa kutimiza nini?
16 Wewe unaonaje wakati watu usiowajua wanapokuja nyumbani kwako? Ni maulizo gani ambayo huenda yakaingia akilini mwako? Labda utajiuliza, Ni akina nani hawa? Wanataka nini? Wameniletea matata? Tunapojitokeza kama wahudumu mlangoni pa mtu, inatupasa tukumbuke hivyo. Basi utangulizi wetu unapasa kustarehesha akili zao waache wasiwasi juu ya maulizo hayo. Lakini namna gani? Haya basi, Yesu alipendekeza utangulizi gani? Alisema: “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.”—Mathayo 10:12, 13.
17. Tunaweza kufanyaje mtu aondoe wasiwasi katika utangulizi wetu?
17 “Amani yenu na iifikilie.” Hiyo maana yake nini? Ni kwamba katika huduma yetu tunatakia kila mtu na kila nyumba amani yetu. Hivyo maneno yetu ya utangulizi yanapasa kuonyesha kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu wanaopenda amani. Hata leo hii Wayahudi (au Waswahili) na Waislamu wanatumia salamu zinazosema “Amani na iwe nanyi” au “Amani” (“Shalom aleichem” au “Shalom” katika Kiebrania, na “Assalām ‘alaikum” au “Salām,” katika Kiarabu). Bila shaka, salamu yetu itakuwa tofauti nchi hii na hii kulingana na desturi ya mahali. Lakini shabaha ni ile ile moja—kufanya mtu mume au mtu mke aache wasiwasi ili asikilize ujumbe wa Ufalme. Kutaja jina lako kwanza, na hata kusema unaishi wapi, huenda kukasaidia kutimiza lengo hilo. Kunaonyesha hakuna jambo fulani unalojaribu kuficha. Kusudi lako na unyofu wako unakuwa wazi uonwe na watu wote. Hapo unakuwa ukifanya kama Paulo alivyoshauri: “Hakikisheni kwamba tabia yenu mbele ya watu wote haiwezi kuchambuliwa. Kwa kadiri ambayo daraka lenu linafikia, ishini kwa amani pamoja na kila mtu.”—Warumi 12:17, 18, Phillips.
18. Ni kiwango gani tunachopaswa kufikia sikuzote katika huduma yetu?
18 Kama tuko katika huduma ya nyumba kwa nyumba au tuko barabarani, watu wote wanatutazama. Mazungumzo na tabia yetu yanapasa sikuzote kuwa yasiyoweza kulaumiwa na yasiyoudhi watu. Lakini, ingawa njia yetu ya kuhubiri inapasa kuwa na upole na yenye amani, haipasi kuwa ya kuomba watu msamaha bila sababu. Sisi hatuoni aibu juu ya kuwa wahudumu wa Mungu mbele ya watu wote.—Marko 8:38.
19, 20. (a) Anapokuwa barabarani, mtu anaweza kufikiaje watu wasiojali sana mambo ya wengine? (b) Kwa sababu gani Yesu alikuwa mwenye matokeo katika ile njia ya kufikia watu kiasili, bila kufuata mpango fulani?
19 Katika mataifa fulani watu wana hali ya kushughulikia zaidi mambo yao wenyewe bila kujali mambo ya wengine. Wengine wanaona haya kufikiwa barabarani na mtu anayeonyesha magazeti. Ikiwa ndivyo ilivyo, mbona usitumie njia ya akili zaidi ya kufikia watu? Unaweza kuanza kwa busara mazungumzo na mtu asiye na haraka kisha utoe vitabu vya habari za Biblia kiasili bila kuonyesha wazi unatoa kitabu.
20 Bila shaka Yesu alikuwa mwepesi wa kutumia namna hiyo ya mahubiri. Kwa kuwa kwa kawaida Wasamaria na wanawake walidhihakiwa na Wayahudi, Yesu alitumia akili katika njia yake ya kumfikia mwanamke yule Msamaria mwenye ukosefu wa adili kwenye chemchemi ya Yakobo. Mazungumzo yake ni kiolezo cha kutolea ushuhuda wa vivi hivi na wa barabarani. Pia ni mfano mzuri wa kufundisha kwa huruma na kwa njia yenye kujenga.—Yohana 4:5-30.
21. Ni jambo gani la maana sana linaloonyeshwa katika huduma ya Paulo?
21 Jambo jingine moja la maana sana lazima lifikiriwe tunapoanza utangulizi wa kujulisha habari njema za Ufalme. Paulo alikuwa fundi wa kulifanya. Ona kama unaweza kulijua kutokana na nyingi za tangulizi zake zilizo katika Matendo 13:16-20; 17:22 na 22:1-3. Angalia kwamba katika kila pindi alitafuta mambo ambayo angeweza kukubaliana na wasikilizaji wake. Alijishirikisha nao pamoja na malezi yao. Matokeo ni kwamba walisikiliza hata kama hawakukubaliana naye. Vivyo hivyo utangulizi wetu unaweza kugusa jambo linaloleta ushirikiano wa kibinadamu kati yetu na mwenye nyumba. Labda unaona kwamba kuna watoto katika nyumba, nawe pia u mzazi. Basi hapo ninyi wawili mna hali moja, msingi wa kirafiki. Unakuwa na jambo la mazungumzo linaloweza kukuelekeza utoe ujumbe wa Ufalme!—Mathayo 18:1-6.
22. Ni maulizo gani ambayo sasa yanafaa kujibiwa?
22 Lakini mapendekezo hayo ni mwanzo tu. Ni hatua gani zaidi zinazohitajiwa ili kutokeza mwanafunzi mwingine mwishowe? Ni mambo gani mengine yanayohitajiwa ili kusaidia mtu mwingine awe na uhusiano pamoja na Mungu kupitia Kristo? Ni sifa gani zitakazofanya huduma yako iwe na matokeo zaidi?
Wewe Ungejibuje?
◻ Ni mengine gani kati ya mambo yanayohusika katika kukubali kwa mtu ujumbe wa Ufalme?
◻ Woga na kujifikiria kunaweza kushindwaje katika huduma?
◻ Shabaha ya tangulizi zetu katika utumishi wa shambani inapasa kuwa nini?
◻ Mfano wa Yesu na msaada wa Paulo unaweza kutusaidiaje katika njia yetu ya kufikia watu?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Yesu alifundisha wanafunzi wake njia zenye matokeo za kutumia katika huduma
[Picha katika ukurasa wa 16]
Ni Maulizo gani yanayoingia akilini mtu usiyemjua anapokuwa mlangoni pako?