Huduma Yenye Matokeo Inayoongoza Kwenye Wanafunzi Zaidi
“Hizi zilikuwa zawadi zake: wengine wawe . . . . waeneza-evanjeli, wengine wachungaji na walimu, ili kutayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya kazi katika utumishi wake.”—WAEFESO 4:11, 12, The New English Bible.
1. Kristo alijisikiaje kuelekea watu?
KRISTO YESU hakuwa mkaa-peke-yake. Huduma yake ilihusu watu kwa njia zote. Katika yale masimulizi manne ya Injili karibu nyakati zote Yesu anajishughulisha na watu. Wakati wa safari zake aliona hali halisi waliyokuwa nayo kisha akawahurumia sana. Ikiwa wewe ni mhudumu Mkristo, je! unawaonea huruma watu unaowakuta?—Mathayo 9:35, 36.
2. Mashahidi wa Yehova wanaigaje mfano wa Yesu?
2 Huduma ya Kikristo leo lazima pia ihusu watu. Kwa kujua uhakika huo, Mashahidi wa Yehova wanatumia njia zenye kubadilikana katika utumishi wanaompa Mungu. Ulimwenguni pote wanaonekana wakisema na watu—barabarani, milangoni, katika maeneo yenye watu wengi madukani, karibu na vituo vya bas na gari-moshi, katika sehemu za viwanda, afisi na biashara. Hata watu wawe wanaishi wapi, Mashahidi wanafika huko wakitumikia wakiwa waeneza-evanjeli. Kwa sababu gani ndivyo walivyo? Kwa sababu neno “evanjeli” limetokana na neno la Kigiriki euaggelion, ambalo linamaanisha “habari njema.” Kama Kristo, ni lazima kila shahidi Mkristo wa Yehova awe mhudumu wa habari njema, mweneza-evanjeli. Basi ni lazima kila shahidi ajishughulishe na watu.—2 Timotheo 4:5; Waefeso 4:11, 12.
3. Ni njia gani ya huduma ya Kikristo iliyo na matokeo kupita zote?
3 Kazi hiyo ya kueneza evanjeli inapasa kuendeshwaje kwa njia yenye matokeo? Je! njia ya kutumia redio na televisheni kama dini nyingi sana zinavyofanya ndilo jibu la kweli? Ebu jiulize mwenyewe, Je! redio na televisheni inaweza kukujibu wewe binafsi maulizo yako kwa njia ya asili? Hapana—kwa njia fulani, hivyo ni vyombo vya utangazaji wa habari visivyoweza kusema na mtu binafsi. Huduma yenye matokeo mengi zaidi ingali ni ile iliyozoewa na Yesu na wanafunzi wake, kuelekeana uso kwa uso na watafutaji wa ukweli. Lakini inachukua wakati na jitihada, na jambo hilo lilionyeshwa na Paulo kwa mfano mwepesi kufahamika: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.”—1 Wakorintho 3:5-7.
4. Ni hatua gani tatu zinazohusika katika huduma yenye matokeo?
4 Maneno hayo yanatoa wazo la kwamba kuna hatua tatu katika huduma ya Kikristo—kupanda, kupalilia na kuvuna. Namna gani hivyo? Kwanza kuna kupanda, ule upokezaji wa kwanza wa habari njema za Ufalme. Halafu kuna kupalilia, kunakotia ndani kumimina maji juu ya kilichopandwa. Jambo hilo linafanywaje? Ni kwa kufanya maongezi zaidi ili kujibu maulizo na kumaliza mashaka ya watu. Mara nyingi hilo linaongoza kwenye funzo la kawaida la Biblia linalokaza sana ukweli wa Biblia katika akili na moyo wa mtu; kwa baraka ya Mungu, ukuzi unatokea. Matokeo ya mwisho ni kuwako kwa mwanafunzi mwingine mwenye bidii wa Kristo Yesu, mhudumu mwingine. Sasa ni kwa njia gani sisi sote tulio wahudumu tunavyoweza kupata baraka hiyo inayofurahisha ya kuvuna mwanafunzi?
5. Ni nini kitakachotusaidia tuwe wahudumu wenye matokeo?
5 Kama makala yetu iliyotangulia ilivyosema, Yesu alifundisha wanafunzi wake njia yenye mafaa ya kufanyia huduma yao. Na Paulo alitaja ‘njia zilizo katika Kristo.’ (1 Wakorintho 4:17) Makundi mengi sana ambayo alisaidia kuanzisha katika sehemu zenye kuzunguka Esia Ndogo na Ugiriki ni ushuhuda unaoonyesha wazi mafanikio yake. Tumekwisha kuzungumza nyingine za njia zilizotumiwa naye (na Yesu pia), lakini kuna nyingine zinazoweza kutumiwa kwa matokeo leo?
Msingi Ni Nini? na Ujumbe Ni Nini?
6. Ni nini ambacho lazima kiwe ndicho msingi wenye kutegemeza huduma yetu?
6 Ujumbe wa Kikristo unapasa kutegemea msingi gani? Je! unapasa kutegemea hekima na falsafa ya kibinadamu? Barua ambayo Paulo alimwandikia Timotheo inatoa jibu lililo wazi: “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua . . . ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho.” Kwa wazi, Biblia, Neno la Mungu, inapasa kuwa ndio msingi unaotegemeza huduma yetu.—2 Timotheo 3:14-17.
7, 8. Yesu na Paulo waliwekaje mfano katika matumizi ya maandiko?
7 Kristo Yesu aliweka mfano katika jambo hilo—yeye alitumia daima maneno ya Maandiko; mtume Paulo naye alifanya ivyo hivyo. Kwa mfano, je! yeye alifika Thesalonike akifundisha falsafa ya Kigiriki? Hapana, kwa maana ni kama vile masimulizi yanavyotuambia: “Kwa hiyo kulingana na desturi ya Paulo yeye akaingia kwao, na kwa sabato tatu akazungumza pamoja nao kwa kuwapa sababu kutoka Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa mitajo ya maandiko kwamba ilihitajiwa kabisa Kristo ataabike na kuinuka kutoka kwa wafu.”—Matendo 17:1-3, NW.
8 Matokeo yakawa nini? “Wengine wao wakawa waamini.” Basi, kwa kufuata njia ya Paulo, msingi wa mahubiri yetu leo lazima uwe ni Neno la Mungu. Ndiyo sababu katika huduma yetu tuna kichwa cha Biblia kilichopendekezwa kwa maongezi. Kwa njia hiyo ukweli wa Neno la Mungu unaweza kuvuta itikio fulani katika wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho.—Matendo 17:4.
9, 10. (a) Kichwa cha mahubiri yetu leo lazima kiwe nini? (b) Toa mifano kutokana na huduma ya Paulo.
9 Sasa ulizo lile jingine ni kwamba, Ni ujumbe gani tunaopaswa kuhubiri? Basi, kichwa cha huduma ya Kristo kilikuwa nini? Yesu alijua sana agizo alilopewa, kwa maana alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” Akielekeza kwenye siku za mwisho za mfumo wetu wa sasa, alisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Luka 4:43, UV; Mathayo 24:14, NW.
10 Mkazo uo huo unapatikana katika mahubiri ya Paulo. Kwa mfano, kwa Wayahudi katika sinagogi ‘alinena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akihojiana nao, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu.’ Kwa wale waliokuwa Roma, ‘aliwaeleza kwa taratibu na kuushuhudia ufalme wa Mungu. ‘ Basi pasipo shaka “ufalme wa Mungu” ndio unaopasa kukaziwa katika huduma yetu ya Kikristo leo.—Matendo 19:8; 28:23, 31.
Wewe Unashambulia au Unavutia Watu?
11. Mara nyingi watu wanatendaje wanapoelekewa na Shahidi, nasi tunaweza kuzuiaje jambo hilo? (Matendo 17:17, 18)
11 Katika karne ya kwanza, watu waligawanywa na dini, kabila na taifa kama walivyo leo. (Matendo 2:7-11) Ndiyo kusema watu walio wengi wanakuwa wametangulia kuwa na maoni fulani juu ya mambo ya dini. Mara nyingi wanapokutana na Shahidi wanaona kuwa wameletewa tisho kisha wanaanza kujitetea. Tunaweza kubadili maoni hayo kwa njia gani? Ni kwa kutumia fadhili, busara na hali ya kubadilikana.
12, 13. Paulo alisemaje kwa waabudu sanamu katika Athene?
12 Angalia namna Paulo alivyoshughulika na hali kama hiyo katika mji wa Athene wenye ibada ya sanamu. Alipoona sanamu nyingi sana mara ya kwanza aliudhika. Wakati aliposimama aseme katika Areopago, je! alianza moja kwa moja kushambulia ibada ya sanamu waliyofanya? Utangulizi wake ulisema: ‘Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini. Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, Kwa Mungu Asiyejulikana. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.’—Matendo 17:16-23.
13 Je! Paulo alitenganisha uhusiano wake na wasikilizaji wake kwa maneno hayo ya utangulizi? Hata kidogo. Njia yake ya kuwafikia ilikuwa yenye busara, si ya kushikilia mambo bila kubadilika. Hakuwalaumu, ingawa kwa maoni ya Mungu ibada yao ilikuwa ya bure. Lengo lake lilikuwa kuhubiri ujumbe wa Ufalme, si kuwashambulia. Alitambua walifuata dini sana akatumia huo kama msingi wa kuingia katika kichwa cha habari yake kuhusu Mungu wa kweli na mwakilishi wake, Yesu aliyefufuliwa. Matokeo ya njia hiyo ya kuwafikia kwa busara yakawa nini? Ingawa wengine wao walidhihaki, “wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo.” Ndiyo, alikaribishwa akafanye ziara ya kurudia!—Matendo 17:22-32.
14. Tunaweza kutumiaje mfano wa Paulo katika huduma yetu?
14 Tunaweza kutumiaje njia hiyo kuhusu huduma yetu leo? Kwanza, inatupasa tuwe macho kuziona ishara zinazotuonyesha moja kwa moja hali ya kidini ya mtu—labda kitu fulani cha kidini alichovaa au kinachoonekana mlangoni au katika chumba kikubwa cha makao yake. Hivyo, sawasawa na Paulo, sisi tunaweza mara nyingi kupata wazo la kutosha juu ya maoni ya kidini ya mtu huyo. Huo unakuwa uongozi wa kutuingiza katika utangulizi wa kirafiki unaoamsha kupendezwa, lakini usioleta ubishi. Kumbuka kwamba tunatembelea mtu sababu yetu hasa ikiwa ni kusema juu ya Ufalme wa Mungu—si kuhusika moja kwa moja katika mazungumzo ya mafundisho. Tunataka ushindi wa kupata watu, si kupata ushindi wa mabishano tu.—Linganisha 2 Timotheo 2:23-26.
15. Ni masomo gani mengine mazuri tunayoweza kujifunza kutokana na huduma ya Yesu? (Luka 10:38-42)
15 Tunaweza kujifunza jambo gani jingine kutokana na mfano wa Kristo? Tunapochunguza huduma yake tutaona usadiki wake na wepesi aliotumia kueleza mambo. Yeye hakutiwa wasiwasi na hali yo yote bali alinena kwa ajili ya Ufalme wa Mungu katika hali za namna zote, ziwe zilifaa au hazikufaa. Aliweza kuhubiri katika faragha ya nyumba fulani au kusimama mbele ya kundi la watu na kutoa mahubiri—bila maandishi ya habari, bila Biblia wala kikuza-sauti! Pia alijua kushughulika na watu wa namna zote. Watu wa hali za chini walijisikia kwamba wangeweza kumfikia. Vitu alivyovitaja ni vile walivyovijua, kama mashamba na mazao, nyavu na uvuvi wa samaki. Mifano yake ilikuwa myepesi sana kueleweka ingawa maana yake ilikuwa yenye kina kirefu. Je! sisi tunaonyesha sifa izo hizo nzuri katika huduma yetu?—Mathayo 4:18-25; 13:1-33; Luka 5:1-3.
Namna ya Kufikia Moyo
16. Kwa sababu gani lazima tuwe walimu wanaostahili?
16 Kwa kawaida inachukua wakati na funzo la uangalifu ili mtu asadikishwe juu ya ujumbe wa Biblia unaohusu Ufalme wa Mungu. Ndiyo sababu tuna mpango wa mafunzo ya nyumbani ya Biblia yanayofanywa kwa ukawaida, bila ya mtu kulipa fedha wala kulazimishwa. Yanafanywa kwa mtu yeyote anayetaka kuchunguza ahadi za Mungu ambazo ametoa kupitia Kristo. Mafunzo hayo yanaendelea kwa muda mrefu na yanakuwa na mazungumzo ya habari nyingi na maulizo mengi. Bila shaka hiyo ni kusema ni lazima tuwe walimu wenye kustahili. Lakini ni mambo gani hasa yanayohusika katika kufundisha?—1 Timotheo 4:16.
17. Ni njia gani moja aliyotumia Yesu kufikia moyo?
17 Kwa mara nyingine tunamgeukia Yesu tupate jibu. Yeye alifundisha namna gani? Tafadhali chunguza tu maandiko yanayofuata uone kama unaweza kuutambua utaratibu mwepesi ambao Yesu alitumia kufundisha wengine: Luka 6:9, 32-34, 39-42. Ulikuwa utaratibu gani? Yeye aliuliza maulizo yenye ufahamu. Kwa sababu gani alifanya hivyo? Ili kusaidia wasikilizaji wake wafikiri kwa kuziona sababu na kujichunguza kwa msaada wa mafundisho yake. Kwa kutumia maulizo alifikia mioyo yao kwa busara. Iliwapasa kuonyesha kama kweli walitaka kuwa wafuasi wake au kama makusudi yao ya kusikiliza yalikuwa ya juu-juu tu.—Mathayo 13:10-17; Marko 8:34-38.
18. (a) Ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanatumia maulizo mara nyingi sana katika vichapo vyao? (b) Ni mazoea gani tusiyopopaswa kutumia sana tunapofundisha wengine?
18 Karibu misaada yote ya kujifunzia Biblia inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova katika huduma yao ina maulizo kwa kila fungu lenye maelezo ya andiko. Huo ni msaada wa kufundishia unaosaidia wale wanaojifunza Biblia waeleze maoni yao kwa maneno yao wenyewe. Ndipo inapokuwa wazi kama mtu anaelewa au haelewi mambo yanayofunzwa. Lakini, ingawa Yesu aliuliza maulizo katika pindi nyingi, yeye hakuzoea kugusia watu majibu kwa kuwatamkia neno la kwanza la jibu au silabi ya kwanza. Nyakati nyingine umejikuta ukiingia katika mazoea hayo unapokuwa na wanafunzi fulani wa Biblia? Kwa sababu gani hiyo si njia nzuri ya kutumia kwa ukawaida? Ni kwa sababu maarifa ya kujua Mungu na Kristo ambayo yanaongoza kwenye wokovu yanapasa kutegemezwa juu ya sababu na akili nzuri, si juu ya kukisia mambo hivi hivi tu.—Yohana 17:3; 1 Yohana 5:20.
Wanafunzi wa Nani?
19, 20. Ni uangalifu gani unaohitajiwa hapa? Kwa sababu gani?
19 Kufikia hapa, kuna jambo linalopasa kuonwa kwa uangalifu. Tukihubiri na kufundisha kwa njia yenye matokeo katika eneo lenye mazao, mwishowe tunatokeza wanafunzi. Lakini ni wanafunzi wa nani? Je! tunapaswa kufikiri hao ni “kondoo zangu mimi”? Na je! sisi tulio wahudumu tunapaswa kujiruhusu tuwekwe katika hali ya kusifiwa kupita kiasi? Angalia namna Paulo na Barnaba walivyoona wakati watu wa Listra walipotaka kuwatendea kama miungu. Walipaza sauti wakaliambia hivi kundi la watu hao: “Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai.”—Matendo 14:14, 15.
20 Paulo na Barnaba hawakujaribu kuvuta fikira za watu ziwaelekee wao wenyewe. Ingawa Paulo alishauri Wakristo wafuate mfano wake, kama alivyofuata wa Kristo, hakuwataka wawe wafuasi wake. Huduma tunayofanya lazima sikuzote iwe kwa utukufu wa Mungu, si wanadamu.—1 Wakorintho 3:6, 7; 11:1.
21. Kwa sababu gani wanafunzi wanakuwa wahudumu pia?
21 Baada ya muda, wanafunzi wanakuwa wahudumu. Kwa sababu gani inakuwa hivyo? Basi, inakuwaje tunapokuwa na habari zilizo njema kweli kweli za kuambia wengine? Je! tunaweza kunyamaza tu tusiwaambie? Badala ya kufanya hivyo, tunajisikia tukiwa tumekazika sana tukitaka kuambia mtu habari hizo. Ni kama Yesu alivyosema: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, . . . kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.” Ndivyo ilivyo kuhusu habari njema za Ufalme. Mwanafunzi ambaye moyo wake umeguswa anataka kufundisha wengine na kujiunga katika huduma kwa ukawaida na kwa kujitolea. Halafu kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa kunafuata. Hivyo kunaendelea kuwa na mfululizo usiokwisha wa wahudumu, kupatana na kanuni ya shauri ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”—Luka 6:45; 2 Timotheo 2:2.
22. (a) Kwa sababu gani Yehova ametokeza tengenezo la walimu na waeneza-evanjeli? (b) Kuna kazi gani ambayo ni lazima bado ifanywe wakati ujao?
22 Leo, duniani pote, Yehova Mungu ana tengenezo lililopewa mazoezi bora zaidi lenye walimu, waeneza-evanjeli, wahudumu wa karne ya 20. Kunao 2,600,000 wanaoshiriki katika ushuhuda wa kumalizia unaotolewa kabla mwisho haujaja juu ya mfumo huu mbovu. Lakini kikosi hicho kinachoendelea kuongezeka kinatayarishwa kwa ajili ya mwito mkubwa zaidi wa ushindani—kuelimisha mabilioni ya watu watakaorudi katika ufufuo. Wewe uko tayari katika pendeleo kubwa hilo? Je! huduma yako ina mazao sasa? Na tusali kwamba nuru yetu ing’ae kwa utukufu wa Mungu, tunapotumikia tukiwa wahudumu wenye matokeo.—Mathayo 5:16; Yohana 5:28, 29.—Kutoka u?8/15/84.
Mambo Ambayo Umejifunza
◻ Ni njia gani yenye matokeo zaidi ya kuhubiri habari njema?
◻ Lazima msingi wa kufundisha kwetu uwe nini? Ujumbe tunaotoa ni nini?
◻ Ni sifa gani zinazohitajiwa kufanya watu watusikilize?
◻ Yesu alifikiaje moyo wa wasikilizaji wake?
◻ Ni uangalifu gani unaohitajiwa tunapofundisha wengine?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mashahidi wa Yehova wanahubiri po pote watu walipo
[Picha katika ukurasa wa 21]
Tunapotoa ushuhuda, imetupasa tuangalie tuone viishara vinavyoonyesha mtu ana dini gani