Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 4/15 kur. 8-13
  • Wahudumu wa Mungu Ni Akina Nani Leo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wahudumu wa Mungu Ni Akina Nani Leo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mhudumu” (Minista) Katika Biblia
  • Mhudumu wa Dini Aliye Mkubwa Zaidi
  • Mhudumu Mkristo
  • Wahudumu wa Mungu Leo
  • Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Ni Nani Aliye Mhudumu?
    Amkeni!—2000
  • Ni Lazima Wakristo wa Kweli Wote Wawe Wahudumu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Roho ya Huduma ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 4/15 kur. 8-13

Wahudumu wa Mungu Ni Akina Nani Leo?

‘Tulituma Timotheo, ndugu yetu na mhudumu wa Mungu katika gospeli ya Kristo.’​—1 WATHESALONIKE 3:1, 2, AMERICAN STANDARD VERSION; ANGALIA PIA AUTHORIZED VERSION, NEW WORLD TRANSLATION.

1, 2. (a) Je! wote wanaodai kuwa wahudumu wa Mungu wanaelekea kuwa wakitimiza huduma yao inavyofaa? (2 Wakorintho 11:13-15) (b) Kwa sababu gani ni jambo la maana kuweza kutambua wahudumu wa kweli wa Mungu leo? (2 Wakorintho 5:18)

HIVI majuzi, katika Amerika ya Kati, wahudumu wa kidini walioagizwa rasmi walisaidia kutayarisha mapinduzi yaliyopindua serikali. Katika Mashariki ya Mbali mhudumu aliyeagizwa rasmi aliongoza uviziaji (maoteo) uliofanya watu wawili wakafa. Katika kusini ya Asia wahudumu walioagizwa waliwatayarisha wafanya kazi katika pambano kubwa kati yao na “waonezi” wao.

2 Watu wote hao walidai kuwa ni wahudumu wa Kikristo, lakini kweli walikuwa hivyo? Je! hilo ndilo jambo ambalo mhudumu wa Mungu anapaswa kuwa akifanya? Hilo ni ulizo la maana, kwa kuwa sana-sana watu wanajifunza habari za Mungu na kupata nafasi ya kuweza kuwa na uzima wa milele kupitia utendaji wa wahudumu wa kweli wa Mungu. (1 Wakorintho 3:5; Yohana 17:3) Tunahitaji kuweza kutambua ni akina nani walio wahudumu halisi wa Mungu. Lakini tunaweza kutambuaje? Biblia peke yake ndiyo inayoweza kutusaidia.

“Mhudumu” (Minista) Katika Biblia

3. (a) Ni nini mengine ya matumizi ya neno la Kigiriki di·aʹko·nos? (b) Ni namna gani ya huduma iliyo ya cheo cha juu zaidi?

3 Kwanza kabisa, kulingana na Biblia mhudumu ni nini? Katika lugha ya kwanza kabisa ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno la “mhudumu” (minista) lilikuwa di·aʹko·nos. Ingawa kuna maoni mbalimbali juu ya chanzo cha neno hilo, maana yake inajulikana sana. Kwa msingi, neno hilo linamaanisha “mtumishi.” Katika vile vitabu vya Injili, di·aʹko·nos na maneno mengine yanayohusiana na hilo linatumiwa mara nyingi katika maana ya kutumikia wale wanaoegemea ili wale chakula. (Luka 4:39; Yohana 2:5, 9) Walakini, katika Kigiriki cha siku za Yesu mara nyingi neno hilo lilihusianishwa na utumishi wa hali ya juu. Katika hati ya maandishi yasiyo ya Kibiblia lilitumiwa kumaanisha maafisa wa kidini, na katika tafsiri ya kwanza ya Maandiko ya Kiebrania yaliyotafsiriwa katika Kigiriki lilitumiwa kusimulia maafisa wa mahakama na wenye kutumikia mfalme Mwajemi Ahasuero. (Esta 1:10; 6:3, Septuagint Version) Bila shaka, huduma ya cheo cha juu zaidi ambayo mwanadamu anaweza kuishiriki ni kutumikia Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova.

4. Mhudumu wa kweli wa Mungu anakuwa na maoni gani juu yake mwenyewe?

4 Kwa kuwa mhudumu (minista) wa Mungu ni pendeleo la cheo cha juu namna hiyo, mhudumu wa kweli anakuwa na maoni gani juu yake binafsi? Hapaswi kuwa mtu wa kiburi wala wa kujiona kuwa mashuhuri. Kwa uhakika, yeye hapaswi kukubali apewe vyeo vya kumrairai kama vile “Baba Mtakatifu” au “Reverendi.” (Mathayo 23:8-12) Badala yake, Yesu alionyesha kwamba mhudumu Mkristo wa kweli angekuwa mnyenyekevu. Alisema: “Mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu.”​—Mathayo 20:26, 27.

5. Wahudumu wa Mungu wanatii amri za nani, na ni nani wanaofaidiwa na huduma yao?

5 Mhudumu anatii amri za bwana wake. Walakini, anapofanya hivyo, huenda kazi yake ikafaidi mtu mwingine. Kwa mfano, ikiwa bwana wake ana wageni, hapo mhudumu huyo anatii bwana kwa kutimiza mahitaji ya wageni hao. Kwa kuwa wahudumu Wakristo ni ‘wahudumu wa Mungu’ na “wahudumu wa Kristo,” wanatii amri ambazo Mungu alitoa kupitia Mwanawe, Yesu Kristo. (2 Wakorintho 6:4; 11:23) Lakini kazi wanayofanya inafaidi wanadamu wengine. Kwa mfano, Paulo alikuwa mhudumu kwa “watu wa mataifa.” (Waefeso 3:1-7, NW) Huduma yake iliwaletea baraka kubwa wale walioitikia vizuri. Tena iliwaletea heshima Yehova Mungu na Yesu Kristo, ambao yeye alikuwa akitii amri zao.

Mhudumu wa Dini Aliye Mkubwa Zaidi

6. (a) Ni nani aliyekuwa mhudumu wa dini aliye mkubwa zaidi ya wote? (b) Yeye alitii maagizo ya nani, naye alihudumu kwa ajili ya nani?

6 Lakini anapaswa mhudumu afanye nini hasa? Tunaweza kujibu ulizo hilo kwa kuangalia utendaji wa mhudumu wa dini aliye mkubwa zaidi ya wote waliopata kuishi, yaani, Yesu Kristo. Yesu alisema hivi: “Mwana wa Adamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake ukombozi badala ya wengi.” (Mathayo 20:28, NW) Akiwa mhudumu, Yesu alitii maagizo ya nani? Yeye alihudumia nani? Na kwa njia gani? Yesu aliyatii maagizo ya Baba yake wa kimbingu. (Yohana 8:28) Hapo mwanzoni-mwanzoni alihudumia Wayahudi peke yao. (Warumi 15:8) Lakini, hatimaye, huduma yake ingefaidi watu wote wenye mioyo inayofaa.​—Yohana 3:16.

7. (a) Yesu alifanya nini akiwa mhudumu? (Marko 1:38) (b) Yesu hakufanya nini?

7 Yesu alifanya nini akiwa mhudumu? Jambo moja alilofanya ni kuepuka kuhusika katika siasa. Angaa nyakati mbili alipata nafasi ya kuchukua msimamo wa kisiasa, lakini akakataa. (Marko 12:13-17; Yohana 6:15) Kwa sababu gani? Kwa sababu huduma yake ilikuwa ya cheo cha juu kuliko siasa, na faida ilizotolea watu, kutia ndani uzima wa milele, zilikuwa kubwa sana kuliko zile zenye kutolewa na siasa. Zaidi ya hilo, mhudumu wa Mungu hawezi kuwa mhudumu wa ulimwengu huu. (Mathayo 6:24) Kwa hiyo, Yesu aliendelea kuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14, NW; Yakobo 4:4) Basi, Yesu alifanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Yeye alilitangaza jina la Mungu waziwazi. Alihubiri kwamba ufalme wa Mungu ndio tumaini la pekee kwa wanadamu. Alifundisha wanafunzi wake viwango bora vya Mungu vinavyohusu adili kisha akawazoeza kumfuata yeye katika huduma. Mwishowe, alifikisha huduma yake kwenye upeo kwa kutoa uhai wake uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu.​—Mathayo 4:17; 5:27-32; 20:28; Yohana 17:3-6.

8. Kwa sababu gani wahudumu wa kweli wa Mungu wa kisasa wanachunguza sana huduma ya Yesu?

8 Yesu ni kielelezo ili watu wote ‘wafuate sana hatua zake.’ (1 Petro 2:21) Ni wale tu wanaoiga sana huduma ya Yesu Kristo wanaoweza kujiita kikweli kuwa wahudumu wa Mungu leo. Tukichunguza utendaji wa wahudumu Wakristo katika miaka iliyofuata kifo cha Yesu tutaona huduma yao ilitia ndani mambo gani.

Mhudumu Mkristo

9. Yesu na Paulo pia walistahili namna gani kuwa wahudumu?

9 Kwanza, siku hizo mtumishi wa Mungu alikuwa akistahili namna gani kuwa mhudumu? Leo, wahudumu walio wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanapokea hati (vyeti) fulani za seminari au chuo kikuu yenye kutangaza cheo chao. Hati hizo ndizo zinazowastahilisha kuwa wahudumu. Walakini, Yesu hakuwa na hati ya namna hiyo. Yeye alikuwa mhudumu mwenye kustahili kwa sababu Mungu alimtia mafuta awe hivyo. (Luka 4:18, 19) Vivyo hivyo, mtume Paulo alisema: “Kustahili kwetu vya kutosha kunatoka kwa Mungu, ambaye kwa kweli alitustahilisha sisi vya kutosha tuwe wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:5, 6, NW) Hivyo, Mungu anastahilisha wahudumu wake mwenyewe. Kwa njia gani?

10. Timotheo alipokeaje mazoezi yake ya msingi ya kuwa mhudumu?

10 Fikiria mfano wa Timotheo, aliyekuwa “mhudumu wa Mungu katika habari njema juu ya Kristo.” (1 Wathesalonike 3:2, NW) Paulo alimwandikia hivi: “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.’​—2 Timotheo 3:14, 15; angalia pia mistari 16 na 17.

11. Ni nani aliyesaidia Timotheo kustahili kuwa katika huduma?

11 Je! hiyo maana yake ni kwamba Timotheo alisoma tu Biblia na hivyo akawa mhudumu? Hapana. Kwanza, ‘alivutwa aamini kwa usadikishi’ wa wahudumu wengine. Hao walikuwa akina nani? Kwa kuwa alikuwa ameyajua Maandiko “tangu utoto” mchanga, bila shaka alipokea angaa mafundisho ya msingi kwa mama na nyanya (bibi) yake, kwa kuwa inaelekea kuwa wazi kwamba baba yake hakuwa mwamini. (2 Timotheo 1:5, NW) Tena, wakati Paulo alipomkuta Timotheo mara ya kwanza, huyo alikuwa tayari ‘ameripotiwa vizuri na akina ndugu katika Listra na Ikonio.’ (Matendo 16:2, NW) Kwa hiyo, imani yake ilikuwa imekuzwa zaidi kwa kushirikiana kwake na Wakristo wenzake katika makundi hayo. Tena, siku hizo ndugu mbalimbali wenye vyeo, na hasa baraza yenye kuongoza ya kundi la Kikristo katika Yerusalemu, walikuwa wakiandikia barua makundi yale mbalimbali ili kuyatia nguvu katika imani, na waangalizi wenye kusafiri walikuwa wakiyajenga kwa ziara zao.​—Waebrania 10:23; Matendo 15:22-32; 1 Petro 1:1.

12. Timotheo alikuwa mhudumu wakati gani, na ni kwa njia gani alizidi kufanya maendeleo baada ya hapo?

12 Kufikia wakati fulani, imani ya Timotheo iliyotiwa nguvu na funzo na ushirika wa namna hiyo ilimsukuma akabatizwa kuonyesha amejiweka wakf kwa Mungu, atumie sehemu yote iliyobaki ya maisha yake kumtumikia Yeye. (Mathayo 28:19, 20; Waebrania 10:5-9) Ni jambo la akili nzuri kuwaza kwamba wakati huo alipata kuwa mhudumu wa Mungu. Lakini maendeleo yake hayakukomea hapo. Uwezo wake wa huduma ulitiwa nguvu zaidi na karama (zawadi) maalumu ya kiroho na mafundisho na mazoezi ya kibinafsi aliyopewa na mtume Paulo. Naye Timotheo alizidi kufanya maendeleo kwa funzo lake la kibinafsi na kwa kushirikiana na Wakristo wengine. (1 Timotheo 4:14; 2Timotheo 2:2) Hivyo, Timotheo alikuwa ‘mhudumu wa habari njema.’ Akiwa hivyo, yeye alifanya nini?

13. Madaraka ya huduma ya Timotheo yalikuwa nini?

13 Alikuwa na kazi za pekee, kwa kuwa alikuwa mwenzi-msafiri wa Paulo. Kwa sababu Timotheo alikuwa mzee, alifanya bidii kufundisha na kutia nguvu Wakristo wenzake. Hiyo ilikuwa sehemu ya huduma yake. (1 Timotheo 4:6) Lakini kama ilivyokuwa imekuwa kwa habari ya Yesu, sehemu kuu ya huduma yake ilikuwa ni kuzihubiri habari njema. (Mathayo 4:23) Mtume Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Wewe, lakini, endelea kuwa na fahamu zako katika mambo yote, patwa na uovu, fanya kazi ya mweneza-evanjeli, timiza kiukamili huduma yako.”​—2 Timotheo 4:5, NW.

14. Maandiko yanaonyeshaje uhusiano kati ya imani na huduma ya kuhubiri?

14 Hata hivyo, ni akina nani zaidi ya Timotheo na Paulo waliotazamiwa kushiriki katika huduma ya Kikristo? Je! ni wazee peke yao au wajumbe wa pekee wenye kusafiri? Hapana. Mtume Paulo aliuonyesha uhakika wa kwamba kazi ya kuhubiri habari njema ilichochewa na imani ambayo Wakristo wote wanatazamiwa wawe nayo. Yeye alisema hivi: “Kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.”​—Warumi 10:10.

15, 16. Ni nani waliokuwa na daraka la kushiriki katika huduma ya Kikristo, na kwa sababu gani unajibu hivyo?

15 Je! hiyo maana yake ni kwamba wote wanaodai kikweli kuwa wana imani ya Kikristo wanapaswa kuwa wahudumu Wakristo, wawe wakishiriki katika kuzihubiri habari njema? Ni hivyo. Paulo alielekeza maneno yake kwa kundi zima la huko Rumi, wala si kwa wazee peke yao. (Warumi 1:1, 7) Kundi zima la huko Efeso lilipaswa ‘kufungiwa miguu utayari tupatao kwa habari njema za imani.’ (Waefeso 6:15; 1:1) Na wote waliosikia ikisomwa barua ile waliyoandikiwa Waebrania walipaswa ‘kulishika sana tangazo la waziwazi la tumaini lao bila kuyumba-yumba.’ (Waebrania 10:23, NW) Kumbuka, pia, kwamba siku ya Pentekoste kila mtu, wanaume kwa wanawake, walijiunga katika kutangaza waziwazi “matendo makuu ya Mungu.”​—Matendo 2:1-21; 1:14.

16 Kuongezea hayo, muda mfupi kabla Yesu hajapaa kwenda mbinguni, yeye aliwaambia hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Wenye kuitikia katika mataifa yote mbalimbali hawakupaswa kuwa watu wa kusikiliza tu. Walipaswa kuwa wanafunzi, kuwa watu wa kufanya mambo yote yaliyohusiana na uanafunzi.​—Luka 10:1; 14:27, 33; Yohana 13:35; 15:8; Matendo 1:8.

Wahudumu wa Mungu Leo

17. Ni mengine gani kati ya mambo ya maana yaliyo katika huduma ya Kikristo? (Mathayo 22 : 37-39)

17 Kufikia hapa, tumekwisha kuona kwamba mhudumu wa kweli Mkristo anaepuka siasa, tena anakuwa amejitenga na ulimwengu. Yeye ni mnyenyekevu na anadumisha viwango bora vya adili ambavyo Yesu alifundisha wafuasi wake. Yeye ni mhudumu wa Mungu, mwenye kuiga Kristo. Kwa hiyo, hapaswi kufuata maoni yake mwenyewe wala kupunguza thamani ya kweli ili ikubalike zaidi kwa wengine. Hata hivyo, kazi yake ya huduma inafaidi wanadamu wenzake, walio waamini na wasio waamini.​—Mathayo 20:28; 26:39; 1 Petro 4:8-10.

18. Ni akina nani walio wahudumu wa kweli wa Mungu leo, na kwa sababu gani unajibu hivyo?

18 Kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu na Timotheo, sehemu inayohitajiwa sana ya huduma ya kisasa ya Mkristo ni kazi ya kuhubiri. Yeye anahubiri nini? Kwamba wokovu ungali unategemea dhabihu ya Yesu. Na kwamba wale wanaotaka kuokolewa wangali wanapaswa kuliita jina la Yehova. (Matendo 4:12; Warumi 10:13) Kuongezea hilo, anahubiri kwamba ufalme ungali ndio tumaini la pekee kwa jamii ya kibinadamu inayotaabika. Kwa hiyo, Yesu alitoa unabii huu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Wahudumu wa kweli wa Mungu ndio wale wanaotimiza unabii huo na kufundisha watu kweli hizo. Nao ni akina nani wanaofanya kazi hiyo yenye kupewa na Mungu. Ni Mashahidi wa Yehova tu.​—Isaya 43:10-12.

19. Ni mambo gani tofauti yanayohusika katika kuwa kwa mtu mhudumu wa Mungu leo?

19 Mtu anastahili namna gani kuwa mhudumu? Kwa njia ile ile alivyostahili Timotheo: Kwa kujenga imani imara katika makusudi ya Mungu, yenye kutegemea funzo la Biblia; kwa kuitia nguvu imani hiyo kupitia ushirika pamoja na Wakristo wengine; kwa kubatizwa katika maji kuonyesha wakf uliofanywa kwa sala aliyompelekea Mungu moja kwa moja kumwambia atamtumikia yeye tangu hapo na kuendelea; na kwa kukubali mwongozo na mwelekezo kutoka kwa Baraza Inayoongoza ya kundi la Kikristo. (Waebrania 10:23-25; Mathayo 24:45-47) Ni akina nani wanaoishiriki huduma hii? Ni wote walio na imani ya unyofu wa moyo, imani yenye bidii katika makusudi ya Mungu, ‘inayotegemea maarifa sahihi. Kushiriki katika huduma ukiwa shahidi Mkristo wa Yehova ni uthibitisho wa kwamba imani yako ni ya kweli.​—Yakobo 2:17.

20, 21. (a) Ni kwa sababu ya mambo gani ambayo Jumuiya ya Wakristo imeshindwa kufanya katika huduma yake ni vizuri kwamba Mungu ametokeza wahudumu leo? (b) Huduma yao ina mweneo gani?

20 Katika siku za mwisho hizi, wahudumu wengi wa dini katika Jumuiya ya Wakristo wana shughuli nyingi za kuhubiri “gospeli ya kijamii,” wakijichangamanya na siasa au kutilia mashaka kuwako kwa Mungu na ufaaji wa Biblia. Nao waenda kanisani wa Jumuiya ya Wakristo hawapendezwi sana na kuwa wahudumu. Kwa hiyo, sisi tunapiga asante kwamba Mungu ametokeza wahudumu wanaoliweka daima jina lake mbele ya wanadamu na kusaidia watu wenye mioyo minyofu wajifunze kweli zinazohitajiwa kabisa za Neno la Mungu, Biblia. Kuna milioni zaidi ya mbili za wahudumu hao ulimwenguni pote na kwa msaada wa Mungu wanahudumia wanadamu wote.

21 Lakini ni kwa njia gani mtu anaweza kuthibitisha kwamba yeye ni mmoja wao? Makala inayofuata itazungumza jambo hilo kwa urefu zaidi.

Maandiko yanayofuata yanatuambia nini juu ya huduma ya Kikristo?

□ Marko 1:38

□ 1 Timotheo 4:6

□ 2 Timotheo 4:5

□ Warumi 1:1, 7; 10:10

□ Mathayo 24:14; 28:19, 20

□ Warumi 10:13

□ Yohana 17:16

[Picha katika ukurasa wa 9]

Hivi ndivyo wahudumu wa Mungu wanavyopaswa kuwa wakifanya?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kazi ya huduma huenda ikahusu kufundisha ndani ya kundi

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wote walio na imani ya kweli wanapaswa kutumikia wakiwa wahudumu Wakristo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki