Ni Lazima Wakristo wa Kweli Wote Wawe Wahudumu?
“Vyote vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho.”—2 WAKORINTHO 5:18.
1. Siku za Paulo hali ilikuwa nini kuhusu jamii ya viongozi wa kidini katika kundi?
“HAKUKUWA na tofauti [siku za mtume Paulo] kati ya viongozi wa kidini na watu wa kawaida kwa maana hakukuwa na viongozi wa kidini.” Maneno hayo ya kugutusha, yaliyotokea katika gazeti Times la London, yanaonyesha ukweli wa msingi kuhusu Ukristo wa kwanza. Hakukuwa na mgawanyiko wa viongozi wa kidini na watu wa kawaida tu. Je! maana yake ni kwamba kundi la Kikristo halikuwa na uongozi wo wote wenye kuonekana? Na je! hakukuwa na wahudumu (maminista) katika maana yo yote?
2. Ni uongozi wa namna gani uliokuwa katika kundi la kwanza? (Wafilipi 1:1)
2 Wakati fulani baada ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., hesabu ya Wakristo wapakwa mafuta ilipoongezeka kuwa maelfu, ikawa lazima kuweka wanaume wenye kustahili katika kila kundi watumikie wakiwa waangalizi na watumishi wa huduma. Lakini wao hawakuwa jamii ya viongozi wa kidini. Kuwekwa kwao hakukutegemea kuwa na masomo ya chuo kikuu wala ya chuo cha kidini. Hawakupokea mshahara kwa utumishi mbalimbali waliotoa. Walikuwa wanaume wanyenyekevu wenye sifa za kiroho, waliowekwa na roho takatifu waangalie kundi. Hata hivyo, je! wao peke yao ndio waliohubiri ‘habari njema za Ufalme’? Wao peke yao ndio waliokuwa wahudumu katika kundi?—Mathayo 24:14; Matendo 20:17, 28; 1 Petro 5:1-3; 1 Timotheo 3:1-10.
3, 4. Kulingana na Paulo, ni nani walioshiriki huduma ya Kikristo?
3 Maulizo hayo yanajibiwa na shauri la Paulo katika barua alizoandikia Wakristo katika Korintho. Angalia utangulizi wa barua yake ya pili: “Paulo . . . kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, pamoja na watakatifu wote walioko katika nchi yote ya Akaya.” Hakuna shaka kwamba yeye aliandikia jamii nzima ya Wakristo waliopakwa mafuta katika Korintho na Akaya, si wenye kuongoza peke yao. Hivyo maelezo yake juu ya huduma ya Kikristo yanawahusu sana “watakatifu wote.” Kwa kutegemea utendaji wake na wa Timotheo, aliwaza hivi: “Kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei.” “Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho . . . Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu.” Anaendelea kusema: “Hakuna njia ambayo katika hiyo tunatoa sababu yo yote ya kukwaza, ili huduma yetu isije kulaumiwa; lakini katika kila njia tunajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu, kwa uvumilivu wa mengi.”—2 Wakorintho 1:1; 4:1; 5:18-20, UV; 6:3, 4, NW.
4 Maneno hayo yana maana ya kwamba kila Mkristo aliyepakwa mafuta anapaswa kuwa mhudumu na mjumbe (balozi, NW) kwa ajili ya Kristo. Kwa sababu gani? Kwa sababu kutokana na dhambi ambayo ulimwengu unatenda, huo ‘umefarikishwa na uzima wa Mungu’ na unahitaji huduma ya upatanisho ili watu watiifu na washikamanifu kutoka mataifa yote wawe na uhusiano pamoja na Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu kupitia Kristo.—Waefeso 4:18; Warumi 5:1, 2.
5, 6. Paulo alihakikishaje maoni hayo katika barua aliyoandikia Warumi?
5 Paulo aliandikia kundi katika Rumi hivi: “Lakini hilo [Neno la Mungu] linasema nini? ‘Hilo neno li karibu na wewe, katika kinywa chako mwenyewe na katika moyo wako’; yaani, ‘neno’ la imani, ambalo sisi tunahubiri. Kwa maana ukitangaza hadharani lile ‘neno katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kuzoea imani katika moyo wako kwamba Mungu alimwinua kutoka kwa wafu, utaokolewa. Kwa maana kwa moyo mtu huamini apate uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la waziwazi la wokovu.”—Warumi 10:8-10, NW.
6 Je! Paulo alielekeza maneno hayo kwa watu wachache tu? Utangulizi wake unaonyesha sivyo, kwa maana aliandika: “Kwa wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu. “Aliongeza hivi: “Namshukuru Mungu wangu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa kuwa imani yenu inahubiriwa katika dunia nzima.” Ni wazi kwamba Paulo alielekezea kundi lote mashauri na kitia-moyo chake, pamoja na sura ya 10. Pendeleo la kufanya tangazo la hadharani liliachwa wazi kwa wote. Kwa kweli, yeye alitia nguvu hoja yake kwa kuongeza hivi: “Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!”—Warumi 1:7, 8; 10:14, 15.
7. Ukristo wa kweli unatofautianaje na dini zile nyingine? (Luka 19:36-40)
7 Hilo ni jambo la kutia moyo kama nini kwa kila Mkristo aliyepakwa mafuta! Maana yake ni kwamba wote kati yao wanapaswa kuwa na furaha ya kueneza ujumbe wa Ufalme juu ya wokovu kwa kupelekea wengine. Ndiyo, machoni pa Mungu, miguu yao inaweza na inapasa kuwa “ya kupendeza macho” kwa njia ya mfano. Kwa sababu gani? Kwa sababu Ukristo wa kweli si dini inayofanya mtu ajitafutie mambo yake mwenyewe ili kujiridhisha, kujitenga na watu na kuamua kuwanyamazia kabisa. Bali, unaendeleza huduma ya bidii ya Kikristo inayoonyeshwa kwa maneno na matendo! Kwamba Paulo alifikiria sana jambo hilo inaonekana kutokana na usemi wake wenye mkazo: “Ole wangu nisipoihubiri Injili!”—1 Wakorintho 9:16, UV; Isaya 52:7, NW.
8. Ni maulizo gani ya maana sana yanayohusu watu wengi sasa?
8 Lakini namna gani mamilioni ya Wakristo wa kweli ambao hawakupakwa mafuta na roho takatifu kwa sababu tumaini lao ni kupata uzima wa milele duniani, si mbinguni? Ni lazima wao pia wawe wahudumu (maminista)?—Zaburi 37:29; 2 Petro 3:13.
Je! Wale wa “Mkutano Mkubwa” Ni Wahudumu?
9. Ni utendaji gani ambao wale wa “mkutano mkubwa” wanaushiriki?
9 Kitabu cha Ufunuo kinatoa jibu la kiasi kidogo kwa maulizo hayo. Kwa mfano, baada ya kuona katika njozi kundi lililopakwa mafuta la watu 144,000, Yohana anasema: “Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao; wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Kwa uhakika hao, wanaokusanywa sasa ili kuokoka dhiki kubwa, hawafichi kitambulisho chao cha Ukristo. Wanatangaza kwa “sauti kuu” chanzo cha wokovu wao. Wanafanya hivyo leo namna gani? Kati ya mambo mengine, ni kwa kusaidia mabaki wachache wa wapakwa mafuta katika utimizo wa unabii na amri nyingine za kihuduma zilizo za lazima.—Ufunuo 7:9, 10, 14.
10, 11. (a) Ni amri gani ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake kabla ya kupaa kwake mbinguni? (b) Ni unabii gani ambao lazima utimizwe katika wakati wetu?
10 Kwa mfano, kundi hilo lisilo na hesabu linaendesha daraka la maana sana katika kutimiza amri ya Yesu ya kuhubiri na kufundisha, ambayo aliwapa wanafunzi wake waaminifu katika Galilaya. Wakati huo Yesu alisema: “Mimi nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” Ni Wakristo wote waliopewa amri hiyo, wala si jamii ya viongozi wachache wa kidini.—Mathayo 28:18-20, NW; 1 Wakorintho 15:6.
11 Amri ya Yesu inahusiana sana pia na unabii aliotoa kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Huo mwito wa ushindani juu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote katika kizazi kimoja umekabiliwaje? Kwa uhakika maelfu yanayopungua-pungua ya Wakristo waliopakwa mafuta yasingaliweza kufanya kazi hiyo ya kuokoa uhai wakiwa peke yao. Lingalikuwa jambo lisilowezekana!—Mathayo 24:3, 14, NW; Luka 21:32.
12. Wapakwa mafuta wanatambua nini kwa furaha leo?
12 “Warithi washirika pamoja na Kristo” ambao wamepakwa mafuta wanafurahi kuitambua sehemu inayotimizwa na wale wahudumu zaidi ya milioni mbili wa “mkutano mkubwa” ambao wameeneza ujumbe wa Ufalme sehemu zote za ulimwengu kwa muda mfupi sana ukilinganishwa na ule wao walitumia. Hata huko nyuma katika miaka ya 1930, Wakristo wengi wa kweli walikubali daraka la huduma katika nchi nyinginezo na wakajitolea kutumikia mahali palipokuwa na uhitaji mkubwa zaidi. Kwa sababu ya mfano wa kujinyima wa ndugu na dada hao, wawe ni wa jamii iliyopakwa mafuta au wa “kondoo wengine,” kazi ya Ufalme ilitia mizizi yenye nguvu katika nchi nyingi za Ulaya, Afrika, Asia na bara zile mbili za Amerika.—Warumi 8:17.
13. (a) Yehova ameharakishaje kazi tangu mwaka wa 1943? (Isaya 60:22) (b) Ni sehemu gani ambayo wale wa “mkutano mkubwa” wameshiriki katika utendaji wa misionari?
13 Kabla ya mwaka wa 1943 jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ya Wakristo waliopakwa mafuta iliona uhitaji wa kuanza shule ya umisionari ili wahudumu Wakristo waweze kupokea mazoezi na matayarisho ya ziada kwa kusudi la kufungua na kuharakisha ile kazi ya kuhubiri katika nchi nyingine nyingi. Tangu mwanzo wa Shule ya Gileadi (“Gileadi” maana yake ni “lundo la ushahidi” kwa Kiebrania) katika mwaka wa 1943, shule hiyo imezoeza wanafunzi wenye kuhitimu kama 6,100 kufikia Machi 4, 1984, na wengi wao wametumwa kwenye migawo ya kigeni sehemu zote za ulimwengu. Ni 292 tu (asilimia 4.8) kati ya wanafunzi hao wenye kuhitimu wa Gileadi waliodai kuwa wa jamii iliyopakwa mafuta, kwa hiyo walio wengi wa wahudumu hao waliopewa mazoezi ya pekee wamekuwa wa “mkutano mkubwa.” Kama Mashahidi wa Yehova wale wengine ulimwenguni pote, wahudumu hao walikubali huduma ya Kikristo iwe sehemu iliyo kubwa zaidi ya maisha ya Kikristo wakati walipofanya wakf wao kwa Yehova kupitia Kristo Yesu.—Mathayo 24:45-47; Waebrania 10:7.
Mwito wa Kazi Unaotegemea Nini?
14, 15. Mwito wa Kikristo kwenye huduma unategemea nini? (Mathayo 22:37-40)
14 Je! hiyo maana yake ni kwamba Wakristo wana mwito wa kibinafsi kutoka kwa Mungu ili wafanye huduma? Ni kweli kwamba wengine katika Jumuiya ya Wakristo wameonyesha “mwito” wao kuwa tukio lililowachochea mno maoni ya moyoni, kama kwamba Mungu aliwaita kwenye utumishi wake moja kwa moja. Lakini je! huduma ya Kikristo inategemea hasa jambo la muda tu kama kusisimuka kwa maoni ya moyoni?
15 Wakati mtume Paulo alipotaja habari za utumishi mtakatifu anaopewa Mungu, alionyesha nini kuwa msingi wa utumishi huo? Aliandika hivi: “Kwa hiyo mimi nawasihi ninyi kwa huruma za Mungu, ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri [“kama tendo la ibada yenye akili,” Phillips; “kama viumbe wenye uwezo wa kufikiri,” The New English Bible, maelezo ya chini].” Ndiyo, utumishi mtakatifu anaopewa Mungu unategemea kufikiri. Namna gani hivyo? Kwa sababu wakf wa mtu na uhusiano wake wa kibinafsi pamoja na Yehova uko juu ya maarifa ya kumjua Mungu wa kweli. Hivyo ingawa mwito wa Mkristo kwenye huduma ni jambo la kufurahisha, hautokani na msisimuko unaoingia moyoni kwa muda tu. Ina kichochezi imara, yaani, kupenda Mungu na kupenda jirani.—Warumi 12:1, NW; Yohana 17:3.
16. Kazi ya kimwili ya wakati wote inaondoa mtu asiwe mhudumu? (Matendo 18:1-5)
16 Lakini huenda ukauliza, Wakristo hao wa kwanza walikuwa wahudumu pia hata kama walikuwa na kazi ya kimwili ya wakati wote au kama walikuwa wake wenye kufanya kazi nyumbani? Ndiyo, walikuwa. Labda waliweza kutumia kisehemu kidogo tu cha wakati wao katika huduma ya Kikristo, wakihubiri na kufundisha, lakini hilo ndilo lililokuwa kusudi lao la kwanza maishani. Walijua iliwapasa kuacha ‘nuru yao iangaze’ wakiwa wanafunzi wa kweli wa Kristo. Kwa kweli walikuwa wahudumu wenye kufanya kazi muda mrefu kabla Jumuiya ya Wakristo haijawa na mpango wayo wa mapdri wenye kufanya kazi.—Mathayo 5:16; 1 Petro 2:9.
Uthibitisho wa Huduma Yao
17, 18. (a) Ni kanuni gani ya ujumla ambao Kristo aliweka kuhusu Wakristo wa kweli? (b) Sifa ya kweli ya mhudumu ni nini?
17 Mashahidi wa Yehova wanathibitishaje kwamba wao ni wahudumu ikiwa hawana cheti au digrii ya chuo kikuu? Wakristo wa kwanza walithibitishaje kwamba walikuwa wahudumu? Kristo mwenyewe alitoa ufahamu huu: “Kila mti mwema huzaa matunda mazuri.” Wahudumu Wakristo wanapaswa kuzaa “matunda mazuri,” na hiyo ni pamoja na kushiriki kazi ya kufanya wanafunzi.—Mathayo 7:17.
18 Mtume Paulo alieleza jambo hilo kwa njia hii: “Je! tunaanza tena kujisifu wenyewe? au tunahitaji, kama wengine, barua zenye sifa kuja kwenu, au kutoka kwenu? Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa [roho ya] Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama.” Uandikaji huo wa mioyo ulitimizwaje? Ni kwa kuhubiri neno la imani lililo mfano wa mbegu ambalo lilipandika katika moyo. Halafu mbegu hiyo nayo ikamsukuma mpokeaji pia ahubirie wengine ujumbe wa wokovu.—2 Wakorintho 3:1-3.
19. Ni sifa gani thabiti ambayo Mashahidi wa Yehova wanayo kuwapendekeza kuwa wahudumu?
19 Je! Mashahidi wa Yehova wana uthibitisho wa ‘barua ya Kristo waliyoiandika wakiwa wahudumu’? Mambo ya uhakika yako wazi. Mwaka wa 1931, walipokubali mara ya kwanza jina lao lisilo na kifani, kulikuwa na Mashahidi karibu 50,000 wenye kuhubiri ulimwenguni. Ripoti ya mwaka wa 1983 inaonyesha kilele cha wahudumu zaidi ya 2,652,000 wanaohubiri habari njema za Ufalme kwa kushirikiana na makundi 46,235. Ndiyo, sasa hesabu ya makundi inakaribia kulingana na hesabu ya Mashahidi waliokuwako mwaka wa 1931! Kwa kweli ukweli umeandikwa juu ya mamilioni ya mioyo kwa muda wa makumi machache ya miaka iliyopita—na huo ni uthibitisho usiokanushika wa huduma ya Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12.
20. Sisi wahudumu Wakristo tunahitaji nini leo? Ni maulizo gani yanayobaki kujibiwa?
20 Wahudumu Wakristo leo wanahitajiwa kwa haraka zaidi ya wakati mwinginewo wote. Muda ni mfupi na mavuno ni mengi. Basi, sababu inaongezeka ya sisi kuwa wahudumu wanaostahili walio hodari wa kazi, ambao wanahubiri na kufundisha kwa njia yenye mazao. Tunaweza kufanyaje hivyo? Tunaweza kuwaje wahudumu wenye matokeo zaidi? Je! mifano ya Kristo na mitume ina mafaa kwetu leo?—Waefeso 5:15, 16; Mathayo 9:37, 38.
Mambo ya Kurudia Kujikumbusha
◻ Tunajuaje kwamba ilikuwa lazima wafuasi wote wa Kristo waliopakwa mafuta wawe wahudumu?
◻ Ni sehemu gani ambayo “mkutano mkubwa” umeshiriki katika huduma ya kisasa?
◻ Mwito wa Kikristo kwenye huduma unategemea nini?
◻ Ni uthibitisho gani ambao Mashahidi wa Yehova wanao juu ya huduma yao?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Nyakati za mitume kulikuwa na jamii ya Wakristo waliokuwa viongozi wa kidini?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mwaka wa 1943 Shule ya Gileadi ilifunguliwa katika South Lansing, New York. Mwaka wa 1961 shule hiyo ilihamishwa ikapelekwa Brooklyn, New York
[Picha katika ukurasa wa 11]
Sasa katika majengo mapya karibu na Daraja la Brooklyn, Shule ya Gileadi inaendelea kutayarisha wahudumu kwa ajili ya utumishi wa kigeni