Wahudumu wa Mungu Wanathibitisha Kustahili Kwao
“Na ni nani anayestahili vya kutosha?”—2 WAKORINTHO 2:16, New World Translation.
1. Katika ulimwengu wa leo uliogawanyika kidini, ni ulizo gani linaloweza kutokezwa kwa weupe kamili wa moyo?
KATIKA ulimwengu wa leo.uliogawanyika kidini, huenda ulizo hili likaulizwa kwa unyofu wote: Ni nani kwa kweli aliye mhudumu, aliyepewa mamlaka na Mungu? Hali moja na hiyo, mtume Paulo aliuliza: “Na ni nani anayestahili vya kutosha kwa mambo haya?” Walipofanyiwa ubishi. Paulo na wafanya kazi wenzake waliweza kusema, “Ni sisi”! (2 Wakorintho 2:16, NW) Lakini leo, ni akina nani walio na msingi imara, haki, na ushujaa wa kujibu, “Ni sisi”?
2. Ni nini hasa maana ya maneno ya Paulo kwenye 2 Wakorintho 2:14-17?
2 Kabla ya kujibu ulizo hilo, acheni tufikirie maneno haya ambayo Paulo aliambia Wakristo katika Korintho: “Lakini shukrani ziwe kwa Mungu! Kwa maana . . . ko kote tuendako yeye anatutumia kuambia wengine juu ya Bwana na kueneza ile Gospeli kama manukato. Kwa kadiri ambavyo Mungu anahusika kuna harufu nzuri yenye kupendeza katika maisha zetu. Ni harufu ya Kristo akiwa ndani yetu, mnukio mzuri kwa waliookolewa hata kwa wasiookolewa wanaotuzunguka kote kote. Kwa wale ambao hawaokolewi, sisi tunaelekea kuwa mnuko wenye kuogopesha wa kifo na maangamizi, hali kwa wale wanaojua Kristo sisi ni kama manukato inayotoa uzima. Lakini ni nani anayetoshea kazi kubwa kama hii? Ni wale tu ambao, kama sisi wenyewe, ni watu wa ukamilifu, waliotumwa na Mungu, wenye kusema kwa uwezo wa Kristo, huku jicho la Mungu likiwa juu yetu. Sisi si kama wale wachuuzi wa bidhaa—nao ni wengi—ambao wazo lao katika kupeleka ile Gospeli ni kujipatia riziki nzuri kutokana nayo.”—2 Wakorintho 2:14-17, The Living Bible; ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Mei 1, 1944, kurasa 133-4.
3. (a) Inatupasa tulioneje wazo la kufanya biashara ya Neno la Mungu ili kujipatia faida ya kichoyo? (b) Paulo alifanya nini aepuke kuwa mzigo wa kifedha kwa wale aliowahubiria?
3 Ati kutembeza-tembeza Neno la Mungu ili kujipatia faida ya kibiashara—ni wazo lenye kuchukiza kama nini! Paulo hakutafuta faida ya kifedha kwa kuhubiri Neno hilo ili aishi maisha ya starehe tu, mwishowe astaafu (ajiuzulu) huduma kisha akae raha mustarehe siku zilizobaki za maisha yake. Alikuwa na nia ya kufanya kazi ya ziada ya kutengeneza mahema ili ajipatie pesa yeye mwenyewe na kusaidia washirika wenzake katika utumishi wa Yehova. (Matendo 18:1-4) Paulo hakuwa mzigo wa kifedha kwa wale ambao aliwahubiri habari njema. Kwa hiyo angeweza kuwauliza hivi Wakristo Wakorintho: “Mimi niliihubiri kwenu Habari Njema ya Mungu bila kudai mshahara; nilijinyenyekeza ili nipate kuwakweza ninyi. Je, nilifanya vibaya?” (2 Wakorintho 11:7, Tafsiri ya Habari Njema kwa Watu Wote) Ikawa lazima kujibu ulizo hilo kwa uthabiti wa kusema hapana!
4. Mashahidi wa Yehova wanafuataje mfano wa Paulo kuhusiana na Neno la Mungu?
4 Leo Mashahidi wa Yehova wanaiga mfano mzuri wa mtume kwa kutokufanya biashara ya Neno la Mungu, huku wakilifanya liweze kupatikana na watu wote. Wao hawauzi kitu hicho kitakatifu. Hivyo hawana viongozi wanaolipwa mshahara, wasemaji wao wanaohutubu mbele ya watu wote hawatozi pesa kwa hotuba zao, wala sahani ya sadaka haipitishwi kamwe kwenye mikutano yao. Mtu ye yote akitaka kuchanga pesa za kazi, anaweza kutoa kiasi cho chote, hata kinachofanana na zile “sarafu mbili ndogo” za mjane, ndani ya kisanduku cha mchango kwenye Jumba la Ufalme au mahali penginepo. (Luka 21:1-4, HNWW) Michango hiyo ya hiari ya mtu inatumiwa kulipia gharama wala si kutajirisha mtu ye yote. Hata nyumba za watu binafsi zinatolewa bila malipo zitumiwe kwa mikutano ya Mashahidi wa Yehova.—Filemoni 1, 2.
‘Tunastahili vya Kutosha’
5. Ni nani amestahilisha Mashahidi wa Yehova wafanye utumishi mtakatifu?
5 Lakini ni nani leo ambaye amestahilisha Mashahidi wa Yehova kuendelea kufuata kiolezo hicho cha Kimaandiko yajapokuwako mateso na upinzani wote wanaoupata daima? Si mwingine ila Mtu yule aliyewastahilisha vya kutosha Paulo na washiriki wenzake kwa ajili ya utumishi mtakatifu. Tafadhali angalia namna kusudi la Paulo lilivyokuwa safi, tofauti na mfanya biashara wa kidini. Yeye alieleza hivi: “Kama kwa weupe wa moyo, kama kutoka kwa Mungu, mbele za Mungu, twanena katika Kristo.” (2 Wakorintho 2:17) Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova wanavyosema leo. Lakini je, tunajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu? Je! tunahitaji kuchapisha barua zilizoandikwa na watu wengine kutupendekeza?
6. (a) Kwa sababu gani viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanafikiri ‘wanastahili vya kutosha’? (b) Lakini ni nini msingi wa mtu kuwa anastahili vya kutosha kuifanya huduma ya kweli ya Kikristo?
6 Paulo alikana kwamba kustahili kwake kuifanya huduma si jambo alilositawisha. Alisema: “Kustahili kwetu vya kutosha kunatokana na Mungu, ambaye kweli ametustahilisha sisi vya kutosha tuwe wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:4-6) Tofauti na Paulo, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanadai kuwa ‘wamestahili vya kutosha’ kwa sababu walihitimu katika vyuo vya ualimu wa kidini. Kwa hiyo wanakana wakisema kwamba wale ambao hawakuhitimu katika vyuo vya kidini hawastahili kuwa wahudumu wenye mamlaka ya kufundisha. Lakini masomo ya pekee ambayo Paulo alijipatia katika dini ya Kiyahudi hayakumfanya astahili kuifanya huduma ya Kikristo inayohusiana na agano jipya. Wala Yesu hakuanza chuo cha ualimu wa kidini ili mitume wake 12 au mtu mwingineye yote ahudhurie. Ndivyo ilivyo leo. Kustahili kwa mtu vya kutosha aifanye huduma ya Kikristo lazima kutokane na Yehova, yule Mwalimu mkubwa zaidi. Bila shaka, mhudumu huyo angepaswa kutoa uthibitisho usioweza kukanwa.
“Ni Nani Aliyekupa Mamlaka Hii?”
7. Viongozi wa kidini walitofautianaje na Nikodemo katika maoni yao juu ya mamlaka ya Yesu?
7 Viongozi wa kidini walibisha juu ya haki ambayo hata Mwana wa Mungu alikuwa nayo kuhubiri habari njema na kufanya miujiza. Katika hekalu, “wakuu wa makuhani na wanaume wazee wa watu wakamjia alipokuwa akifundisha wakasema: ‘Ni kwa mamlaka gani wewe unafanya mambo haya? Na ni nani aliyekupa mamlaka hii?’ “(Mathayo 21:23, New World Translation) Walikataa kukata maneno kama vile alivyofanya Nikodemo mtawala wa Kiyahudi wakati alipomwambia Yesu: “Rabi, twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye.”—Yohana 3:1, 2.
8. Baada ya miaka zaidi ya mitatu ya huduma ya Yesu, viongozi Wayahudi walikuwa na maoni gani juu ya kitambulisho chake na mamlaka yake?
8 Kama Yesu angalitaka angaliweza kuwaambia wabishi wake hivi, ‘Acheni matendo yangu yajisemee yenyewe!’ Baada ya kufanya kazi yake kwa miaka zaidi ya mitatu, wakuu wa makuhani na wanaume wazee walikuwa wameona ishara nyingi za kuwapa msingi wa kukata maneno kwa usahihi Yesu alikuwa nani na namna alivyokuwa na haki ya kufanya miujiza na kufundisha ukweli juu ya Ufalme wa Mungu. Wao walikuwa tu wenye shingo ngumu wasitake kukubali ushuhuda wote uliokuwa ukitolewa na Yehova kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa.
9, 10. (a) Kwa sababu gani isishangaze Mashahidi wa Yehova kwamba kustahili kwao kuwa wahudumu kunatiliwa shaka leo? (b) Yesu alishughulikaje na viongozi wa kidini waliofanya ubishi juu ya mamlaka yake, na hiyo ikawa na matokeo gani juu yao?
9 Kwa sababu ya mambo yaliyompata Yesu, Mashahidi wa Yehova hawashangai kuona kwamba kustahili kwao kuwa wahudumu waliopewa mamlaka na Baba yake kunatiliwa shaka na viongozi wa kidini leo. Kwa kuwa wale waliobisha juu ya mamlaka ya Yesu walipuuza miujiza yake mingi, yeye alitokeza ulizo lililowababaisha. Nao wanafunzi wake wa kisasa wanaweza kufanya ivyo hivyo kwa habari ya wale wanaopuuza kazi zao kwa makusudi.
10 Wakati wakuu wa makuhani na wanaume wazee walipomuuliza Yesu, “Ni nani aliyekupa mamlaka hii?” yeye hakutokeza ulizo ambalo si halisi, bali alisema: “Na mimi nitawauliza neno moja; ambalo mkinijibu, nami nitawaambia ni kwa amri gani ninatenda haya. Ubatizo wa Yohana ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu?” Masimulizi hayo yanaongeza hivi: “Wakahojiana wao kwa wao, wakisema, Tukisema, Ulitoka mbinguni, atatuambia, Mbona basi hamkumwamini? Na tukisema, Ulitoka kwa wanadamu, twaogopa mkutano; maana watu wote wamwona Yohana kuwa ni nabii. Wakamjibu Yesu wakasema, Hatujui. Naye akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa amri [mamlaka, NW] gani ninatenda haya.” (Mathayo 21:23-27) Leo, Mashahidi wa Yehova wanaweza kuwauliza viongozi wa kidini maulizo yenye matokeo ya namna hiyo, kwa kutumia Maandiko.a
11. Ni kazi gani ambayo watu wa Yehova walifanya kabla ya mwaka 1914, na wenye kuwalaumu walinyamazishwaje?
11 Kuanzia mwaka wa 1876, watu wa Yehova walijulisha ulimwengu, na hasa Jumuiya ya Wakristo, kwamba Majira ya Mataifa yangeisha katika vuli ya mwaka 1914. (Luka 21:24) Viongozi wa kidini waliona hawangeweza kuipuuza kazi hiyo ya utangulizi ya karibu miaka 40—kazi ambayo ililingana na ile ya Yohana Mbatizaji. Viongozi hao wa kidini walingojea kwa hamu nyingi ya kumrukia mhariri wa jarida hili iwapo kwamba mwaka 1914 ungepita na kusionekane matukio makubwa sana ya kulingana na yale aliyowaonya watu. Lakini ng’o, wakanyamaza kimya-a-a wakati amani ilipovurugwa Julai 28, 1914 na kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza!
12. Ni magumu gani yaliyokuja pamoja na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na kuifuata?
12 Uharibifu wa vita na kutoka kwa wanaume wengi kwenye shughuli za ukulima kulitokeza upungufu wa chakula. Matetemeko ya ardhi yalitikisa sehemu mbalimbali za dunia, yakaleta uharibifu mkubwa na taabu nyingi. Mwaka 1915 tetemeko la ardhi huko Avezzano, Italia, liliua watu 29,970, na tetemeko kubwa ajabu mwaka 1920 likaua watu 200,000 katika Mkoa wa Kansu, China. Mwaka 1923, watu zaidi ya 140,000 waliuawa na tetemeko la ardhi lililotokea katika Kanto Kuu, Japani. Ile vita ilifuatwa upesi na homa kali ya Kihispania ambayo kwa muda wa mwaka mmoja iliua watu wengi kuliko wale waliouawa na vita hiyo ya miaka minne. Pia hayatasahauliwa yale mateso yaliyopata watumishi wa Mungu wakati wa hilo pigano la ulimwengu la kwanza, yakafikia upeo kwa kuwafunga isivyo haki msimamizi na katibu-mweka-hazina wa Sosaiti yetu na sita kati ya wafanya kazi wenzao.
13. Mashahidi wa Yehova wameuwauliza nini viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo, na ingewapasa viongozi hao wenye kulaumu wakubali nini kama wangejibu kwa usahihi?
13 Tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Mashahidi wa Yehova wamewauliza hivi viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo: ‘Je! matukio yenye msiba ambayo yameipata dunia yetu tangu mwaka 1914 ni utimizo wa unabii wa Yesu kwenye Mathayo 24:3-13?’ Viongozi hao wakisema ndivyo kwa unyofu, ingemaanisha wanakubali kwamba Yesu Kristo alikuja katika Ufalme wake wa kimbingu mwaka wa 1914. Basi ni jambo la wazi kwamba, kwa kuwa Yesu alisema ‘ulimwengu haungemwona tena’ na sasa yeye ni mtu wa kiroho asiyeweza kufa, “kuja” au “kuwapo” kwake hakuonekani. (Yohana 14:19; Mathayo 24:3, UV, 1 Petro 3:18) Lakini kukubali yote hayo kungezuia viongozi wa kidini wasiseme kwamba matukio yenye kuutikisa ulimwengu ya miaka 1914-1918 yalikuwa mapigano ya kikawaida tu ambayo yamekuwa desturi ya mataifa muda wote wa historia.
14. (a) Kama viongozi wa kidini wangekubali mambo iwapasavyo, kufanya hivyo kungewalazimisha washiriki katika kazi gani? (h) Ni kisingizio gani cha Ufalme ambacho wangepaswa kukikana, lakini wao wamefuatia mwendo gani?
14 Zaidi ya hilo, kama viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wangekubali kwamba matukio ya 1914-1918 yalitia alama mwisho wa mfumo wa kale wa mambo, wangelazimika kukubali sehemu zile nyingine za “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu na wangepaswa kushiriki katika utimizo wa maneno yake: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14, NW) Hiyo ingemaanisha kuhubiri, si ile Gospeli ambayo wamehubiri kwa karne nyingi, bali zile habari njema za Ufalme uliosimamishwa mbinguni mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka 1914. Ingemaanisha waukatae Ushirika wa Mataifa wasiuone kuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani” kisha wauone huo na mrithi wake, Umoja wa Mataifa, kuwa ‘chukizo la uharibifu lenye kusimama katika patakatifu.’ (Mathayo 24:15) Lakini kufikia mwaka wa 1985, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanakataa kuuita Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa kuwa lile “chukizo.”
15. Ni wakati ujao wa namna gani unaowangoja viongozi wa kidini, lakini Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya nini?
15 Kwa hiyo viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanakataa kuchukua msimamo wao upande wa Ufalme wa Yehova kupitia Yesu Kristo. Kwa sababu hawauungi mkono, wataharibiwa katika ile “dhiki kubwa” ambayo iko karibu sana. Lakini tofauti na wao, Mashahidi wa Yehova wameacha Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, nao wanahubiri ujumbe wa Ufalme katika nchi 203. Kazi hiyo isiyopata kuwa na ulinganifu ni sehemu ya kutokeza ya ile “ishara” inayothibitisha kwamba katika mwaka 1914 Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa kimbingu, atawale katikati ya adui zake.—Mathayo 24:3, 14, 21; Zaburi 110:1, 2; Ufunuo 18:1-5.
Je! Kuna Uhitaji Wo Wote wa Pendekezo?
16. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya pendekezo, na Paulo alisema nini juu ya jambo hilo?
16 Je! sisi tunajipendekeza wenyewe bila msingi kuwa mashahidi wa Yehova waliopakwa mafuta? Au tunaongoza mambo kwa werevu ili tuthibitishie “kondoo wengine” wa Yesu pendekezo hilo? (Yohana 10:16) Paulo hakufanya jambo kama hilo bali aliweza kuwaambia hivi Wakorintho waliokuja kuwa Wakristo kwa sababu ya jitihada zake za kutokuchoka: “Je! tunaanza tena kujisifu wenyewe? au tunahitaji, kama wengine, barua zenye sifa kuja kwenu, au kutoka kwenu? Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa [roho ya Mungu iliyo] hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama.—2 Wakorintho 3:1-3.
17. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba Paulo alistahili vya kutosha kuifanya huduma, na katika habari hiyo ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya Mashahidi wa Yehova?
17 Kwa msaada wa roho ya Yehova, Paulo aliandika hesabu kadha ya vitabu vya Biblia na kugeuza watu wengi wafuate Ukristo. Basi kwa uhakika alijithibitisha kuwa alistahili vya kutosha kufanya huduma ya Kikristo, Katika ulinganifu wa kisasa, hasa tangu jarida hili lilipochapishwa mara ya kwanza mwaka 1879, mabaki waliopakwa mafuta wa wanafunzi wake Kristo wamechapisha vitabu vingi vya Kibiblia, ingawa hawakuviandika kwa kutiwa pumzi ya Mungu kama Paulo. Tangu mwaka 1920, wao wamechapisha maelfu ya mamilioni ya vitabu, vijitabu, magazeti, na trakti katika lugha nyingi. Vitabu hivyo vimeenezwa kwa bei ya chini, na walio maskini wamepewa vingi kati yavyo bila malipo. Sosaiti yetu pia imepanga kuwe na hotuba za Biblia bila malipo na kutuma wamisionari kwenye maeneo yasiyopata kutumikiwa sehemu zote za dunia. Makumi ya maelfu ya watu wameuitikia ujumbe wa vitabu na kinywa wakaonyesha wakfu wao kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa, hasa tangu mwaka 1935 ilipoonyeshwa wazi mara ya kwanza kwamba “mkutano mkubwa” na kikomo wa “kondoo wengine” wa Yesu unaweza kutazamia uzima wa milele katika paradiso itakayorudishwa duniani.—Ufunuo 7:9-17; Luka 23:43, ZSB.
18. Wakifanyiwa ubishi wathibitishe kustahili kwao kuwa wahudumu, mabaki wapakwa-mafuta wanaweza kuonyesha nini?
18 Kwa hiyo, namna gani kama viongozi wa kidini wanafanya ubishi kwamba mabaki wapakwa mafuta watoe vyeti vya kuonyesha kwamba wao ni wataalamu wa kidini? Watumishi hao wa Yehova wanaweza kutoa ushuhuda mkubwa hata zaidi! Wanaweza sasa kuelekeza kwenye “kondoo wengine” zaidi ya milioni mbili na nusu na kusema: ‘Hiyo ndiyo barua ya kutuunga mkono!’ Wanaweza kutumia maneno ya Paulo na kuwatangazia hivi washiriki wa ule “mkutano mkubwa”: “Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote.” (2 Wakorintho 3:2) Acheni viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo waisome barua hiyo iliyo hai ya Wakristo walio wakfu na kubatizwa ambao wanamtumikia Yehova Mungu mchana na usiku kwenye hekalu lake, huku wakisaidia ‘kuzihubiri habari njema hizi za ufalme katika dunia yote kwa ushuhuda kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14, NW) Kama mabaki wapakwa mafuta, wao wanajithibitisha wenyewe kuwa wanastahili vya kutosha kuifanya huduma ya Kikristo.
19. Ni barua gani isiyo na kifani itakayohifadhiwa iipite Har–Magedoni?
19 Barua hiyo ya pendekezo isiyo na kifani haitafutiliwa mbali katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokaribia sana katika mahali pa mfano panapoitwa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14-16) Bali, italindwa na kuhifadhiwa na yule Mungu Mweza-Yote ikaonyeshwe katika mfumo wa mambo utakaoifuata Har–Magedoni chini ya Kristo Mfalme. “Mkutano mkubwa” huo utakuwa barua yenye nguvu kama nini kwa mabilioni ya wafu wa kibinadamu ambao Yehova Mungu, kupitia Yesu Kristo, atawafufua wakati huo watoke katika makaburi ya ukumbusho sehemu zote za dunia! Kwa hiyo endeleeni kuandika, enyi mabaki wapakwa mafuta! Pia endeleeni kuwasaidia, enyi “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema!
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, ona mafungu 13 na 14 hapa chini.
Wewe Una Maelezo Gani?
◻ Mashahidi wa Yehova wanafuataje mfano wa Paulo wa kutofanya biashara ya Neno la Mungu?
◻ Ni nini msingi wa mtu kuwa anastahili vya kutosha kuifanya huduma ya kweli ya Kikristo?
◻ Kama viongozi wa kidini wangekubali ukweli wa mambo, wangelazimika kushiriki katika kazi gani?
◻ Mabaki wapakwa mafuta wanaweza kuonyesha barua gani isiyo na kifani inayothibitisha kwamba wao ni wahudumu wanaostahili vya kutosha?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Yesu alifundisha wanafunzi wake wawe wahudumu, lakini hakuanzisha chuo cho chote cha ualimu wa kidini
[Picha katika ukurasa wa 19]
Wakiwa ni wahudumu wanaostahili, Mashahidi wa Yehova wanahubiri habari njema za Ufalme uliosimamishwa. Je! wewe unafanya hivyo?