Wahudumu wa Ufalme Wanaelekeana na Ubishi
“Basi Apolo ni nani? na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa.”—1 WAKORINTHO 3:5.
1. (a) Kwa njia ya kidini, ni nini kinachotiliwa shaka leo, na kwa sababu gani? (b) Ni milki gani inayoelekewa na tisho, nayo itapatwa na nini?
MAMLAKA ya wahudumu wa dini inabishaniwa leo. Zaidi na zaidi, ndivyo inavyokuwa wakati ile sehemu ya kisiasa ya ulimwengu huu inapoendelea kuigeuka dini, kutia na ile inayoitwa dini ya “Kikristo” ikiiona kuwa biashara ya kujiletea faida. Hata wenye kuhitimu masomo ya vyuo vya kidini wanakanwa kwamba hawastahili kuwa wahudumu waliopewa mamlaka kwa kufaa na wanapigwa marufuku katika mataifa ambayo yanageuka kuwa yenye kupinga dini. Ndiyo, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo inashambuliwa na kuelekewa na tisho la kupatwa na shambulio litakaloiangamiza. Mwanzishi wa kimungu wa ibada ya kweli alitabiri jambo hilo na akathibitisha wakati wake mwenyewe wa kutimizia unabii wake. Viumbe vilivyo hai katika ulimwengu wote vitafaidika kutokana na tukio hilo kubwa ajabu!
2. Kwa habari ya dini, ni nini kitakachobaki na ni nini hakitabaki?
2 Hata hivyo, sasa ni muda mfupi umebaki upingaji-dini uache kutawala dunia, lakini Muumba wa ulimwengu wote atakayekuwa amethibitishwa kuwa hana lawama atabaki! Ndiyo, na dini ya kweli ya huyo Mungu Aliye Juu Zaidi asiyekufa itabaki! Kwa sababu hiyo, ingawa mabilioni ya watu walio duniani wanakataa kuyakubali mambo ya hakika, sasa hivi wenye kuzoea ibada safi ya Mungu wako hai na ni watendaji duniani. Nayo maneno haya yaliyosemwa karne nyingi zilizopita ni ya kweli leo: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru.”—Warumi 1:20.
3, 4. (a) Inaweza kuthibitishwaje kwamba Yehova ana wahudumu duniani? (b) Tunajuaje kwamba wahudumu wa kidini wa Babuloni Mkuu watakosa kazi karibuni?
3 Wakati maneno hayo yalipoandikwa katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, Yehova Mungu alikuwa na wahudumu wake duniani. Hivyo mtume Paulo angeweza kuandika hivi: “Basi Apolo ni nani? na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu.”—1 Wakorintho 3:5-9.
4 Ni lazima Yehova awe ana wahudumu duniani hata leo. Lakini yeye hatumii wahudumu wa kidini wa Babuloni Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Kwa kweli, karibuni wao watafutwa kazi. Huo ni wakati ambao Babuloni Mkuu yenyewe itakapoondoshwa isiwepo. Likitabiri jambo hilo, andiko la Ufunuo 16:19 linasema: “Mji ule mkuu ukapasuliwa sehemu tatu, nayo miji ya mataifa ikateketea. Babuloni, mji mkuu, haukusahauliwa na Mungu. Aliunywesha kikombe cha divai ya ghadhabu yake kuu.” (HNWW)
5. Ni jambo gani lililotokea katika Babuloni wa kale mwaka 539 K.W.K., na namna gani wahudumu na wengine wenye kuunga mkono dini za Babuloni Mkuu?
5 Namna gani, basi, watu wanaobaki wakiwa wafuasi washikamanifu wa mifumo ya kidini inayotumikiwa na wahudumu wa Babuloni Mkuu waliosomea kazi yao? Basi, fikiria jambo lililotukia usiku ule wa mwaka 539 K.W.K. wakati Mfalme Belshaza na waheshimiwa aliokuwa amewaalika walipokuwa wakisifu miungu ya Babuloni kwenye karamu kubwa ajabu na kuwaonyesha ukaidi Wamedi na Waajemi waliokuwa wamewazingira. Kwanza, wala-karamu hao wenye makelele walipewa onyo walipoona mwandiko wa kimuujiza juu ya ukuta wa jumba la karamu kisha wakasikia fasiri ikitolewa na Danieli nabii wa Yehova. Halafu, Babuloni ilipoanguka usiku huo huo, mfalme na bila shaka wala-karamu wale wengine wenye kutukuza miungu ya uwongo waliuawa na washindaji wenye kushambulia. (Danieli, sura ya 5) Msiba kama huo unawangoja wahudumu na wale wanaoendelea kuwa washikamanifu kwa mifumo ya kidini ya Babuloni Mkuu.
Wahudumu wa Mungu Wanahitajiwa kwa Haraka
6. (a) Katika kipindi hiki cha hatari, ni lazima Mungu awe ana nini kwa jamaa ya kibinadamu? (b) Majira ya Mataifa yaliisha wakati gani, na Yesu alisema nini juu ya jambo hilo?
6 Hakuna mtu anayeweza kutoa sababu ya kutia shaka kwamba sasa tunaishi katika kipindi kilicho chenye hatari kupita vyote vya historia ya kibinadamu tangu ile Gharika ya duniani pote ya siku za Noa. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo inahitajiwa kabisa kwamba sasa kuwe na wahudumu wa kweli wa Mungu wa Noa. Kwa uhakika, kama vile Yehova alivyowapa maonyo watu wa wakati wa Noa na wala-karamu wenye makelele kwenye karamu ya Belshaza, ni lazima Yeye awe alikuwa na ujumbe wa haraka kwa jamaa ya kibinadamu tangu mwaka 1914, wakati ambao vita ya ulimwengu ya kwanza ilitokea. Kwa kweli, kwa muda wa makumi manne ya miaka watumishi wa Mungu walikuwa wameonyesha kati ya watu wa mahali pengi sana kwamba mwaka huo ndio ungetia alama mwisho wa Majira ya Mataifa, ambayo Yesu aliyasema hivi: “Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia.”—Luka 21:24.
7. (a) Ni mpaka wakati gani Yerusalemu wa kidunia ulikanyagwa na mataifa yasiyo ya Kiyahudi? (b) Yesu alikuwa akimaanisha nini mwishowe aliposema Yerusalemu ‘ungekanyagwa na mataifa’?
7 Kwa miaka ipatayo 53 baada ya mwaka 1914, au mpaka ile Vita ya Siku Sita ya 1967, Yerusalemu wa kidunia uliendelea kukanyagwa na mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Lakini, ni wazi kwamba Yesu hakuwa akimaanisha Yerusalemu wa Kiyahudi uliopo leo bali alikuwa akimaanisha kile kilichofananishwa na mji huo kufika mwaka 607 K.W.K. Nao ulifananisha nini? Ulifananisha Ufalme wa Yehova Mungu kupitia Mfalme wake aliyewekwa wa nyumba ya kifalme ya Daudi!—Luka 1:32; 1 Mambo ya Nyakati 29:11.
8. Yehova angempa nani ufalme wa Daudi, na kwa sababu gani wanadamu hawangeweza kuliona tendo lililotabiriwa la kumtawaza?
8 Yesu Kristo ndiye yule ambaye Yehova Mungu angempa ufalme wa Daudi babu yake wa zamani. Alipokuwa mbele ya Pilato hakimu, Yesu alisema kwamba Ufalme Wake haukuwa wa ulimwengu huu, akimaanisha kwamba ungekuwa wa kimbingu. (Yohana 18:36) Basi, kulingana na kufikiri kuzuri, kutawazwa kwa Yesu wakati ujao katika Ufalme mwishoni mwa Majira ya Mataifa kungetukia katika mbingu zisizoonekana. Hivyo kuketishwa kwake kwenye kiti cha ufalme hakungeonekana kwa macho ya kibinadamu, na hiyo ndiyo sababu wala sisi wala mataifa yasiyo ya Kiyahudi hatukumwona akiketishwa katika Ufalme wake anaoustahili, ambao alipewa na Mungu mwaka 1914. Kwa uhakika mataifa hayo hayakuamini kwamba tukio hilo lilifanyika, ijapokuwa jambo hilo lilikuwa limetangazwa na watu wa Yehova tangu miaka ya 1870.
9. (a) Mataifa yalifanya nini kwa kupuuza kuhusu ujumbe wa Ufalme? (b) Kwa sababu ya vile mataifa yalivyofanya mwaka 1914, ni jambo gani likawa lazima?
9 Kwa kuupuuza ujumbe wa Ufalme, katika vuli ya mwaka 1914 mataifa yalijiingiza sana katika vita. Kama ilivyotabiriwa kwenye Zaburi 2:1-12, walijithibitisha kuwa adui za Yesu, wakakataa ‘kubusu’ Mfalme aliyekuwa ametawazwa muda mfupi tu uliotangulia, hivyo waonyeshe wananyenyekea na kutii. Kwa hiyo, ilikuwa lazima kutenda yaliyosemwa kwenye Zaburi 110:1, 2, ambapo tunasoma: “Neno la [Yehova] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. [Yehova] atainyosha toka Sayuni fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako.”
10. (a) Ni chini ya hali gani Yesu alianza kutawala katika mwaka 1914? (b) Ni akina nani wamekuwa wakimwakilisha Yehova katika karne ya 20?
10 Wapinzani wa Kiyahudi walionyesha uadui wao kuelekea mitume wa Yesu wakati Yesu alipoketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu angoje wakati wa kuanza kutawala katikati ya adui zake. (Matendo 4:24-26) Kwa hiyo, ilikuwa katikati ya adui kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa akaanza kutawala mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka 1914. Hivyo katika karne hii ya 20, kama ilivyokuwa zamani, ni katikati ya adui kwamba Yehova amekuwa na watu wa kupeleka ujumbe wake, wale wahudumu wa kweli wa Ufalme. Wao ni mashahidi wake.—Isaya 43:10-12.
Kutetea Kustahili Kwetu Kuwa Wahudumu
11. Ni nani wamebisha juu ya mamlaka ambayo Mashahidi wa Yehova wanayo ya kuwa wahudumu wa Ufalme walioagizwa rasmi na Mungu?
11 Muda wote, imekuwa lazima wahudumu wa kweli wa Ufalme walioagizwa rasmi na Mungu watetee kwamba wamepewa mamlaka ya kuifanya huduma. Kwa uhakika ndivyo wamefanya Mashahidi wa Yehova katika karne hii ya 20. Kustahili kwao kuwa wahudumu wa Mungu walioagizwa rasmi kwa njia inayofaa kumebishaniwa na kukanwa kuwa hakufai. Na nani? Hasa na watu wenye kuhitimu masomo ya kidini ya vyuo vya Jumuiya ya Wakristo wanaopokea cheti cha kuagizwa rasmi na kuwa viongozi wa kidini wenye kulipwa mshahara. Wao wanajihesabu kuwa wamepata uanachuo unaofaa na ndio peke yao wanaostahili vya kutosha kuwa wahudumu wataalamu wa yule Mungu wa Biblia.
12. Ni mamlaka ya Mkristo gani mashuhuri wa karne ya kwanza iliyofanyiwa ubishi, na mtu ye yote mwenye kuleta habari njema za namna tofauti alipaswa kuonwaje?
12 Hali hiyo ilikuwa ivyo hivyo katika karne ya kwanza W.K. Katika mkoa wa Kiroma wa Galatia, hata mwandikaji aliyeongozwa na Mungu wa karibu nusu ya vile vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo alielekeana na tukio lililoleta ubishi juu ya kustahili kwake kuwa mtume wa Yesu Kristo, kwa maana tukio hilo lilitia shaka juu ya usahihi wa kile alichokuwa akifundisha kuwa ni Ukristo. Kwa hiyo alilazimika kuwaambia hivi Wagalatia: “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili ya namna nyingine. Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na katika kuigeuza injili ya Kristo. Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe.”—Wagalatia 1:6-9.
13. Kwa sababu gani Wagalatia wasingalipaswa kutilia shaka mamlaka ya Paulo?
13 Ni kweli kwamba mwandikaji huyo, mtume Paulo, hakujifunza mafundisho ya Kikristo kwa kuonana kibinafsi na Yesu Kristo, wala mitume Wake 12. Baadaye, Paulo alitumia wakati fulani akiwa na mtume Petro, au Kefa. (Yohana 1:42; Wagalatia 1:18, 19) Lakini kwa kutetea kwamba yeye alikuwa mhudumu anayestahili wa zile habari njema zilizotoka kwa Mungu kupitia Kristo, Paulo aliweza kuwaambia hivi Wakristo hao Wagalatia wasiokuwa na msimamo imara: “Tena walipokwisha kuijua ile neema niliyopewa; Yakobo, na Kefa, na Yohana, wenye sifa kuwa ni nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika; ili sisi tuende kwa Mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara.” (Wagalatia 2:9) Kwa hiyo Wagalatia hao wangalipaswa kujiuliza hivi: Ikiwa mitume wa Yesu, Petro, Yakobo, na Yohana walimtambua Paulo kuwa mchukuaji wa habari njema za kweli, sisi tuna msingi gani wa kubisha juu ya ujumbe wake na kuuepuka?
14. Kwa sababu gani si jambo geni kwamba uhudumu wa Mashahidi wa Yehova unafanyiwa ubishi?
14 Lakini namna gani watu wa Yehova leo? Kwa kuwa mtu kama Paulo alilazimika kutetea sifa zake za kustahili kuwa mhudumu wa Mungu na Mkristo, mbona sisi, tushangae ikiwa sisi, mashahidi wa Yehova tuliojiweka wakfu na kubatizwa tunafanyiwa ubishi na kulazimika kutetea msimamo wetu wa kuwa wahudumu wa Ufalme? Bila shaka, kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo, ubishi huo ni kazi bure tu.
Hata Yesu Alifanyiwa Ubishi
15. Ni nani pia, mwenye cheo cha juu kuliko mitume, aliyefanyiwa ubishi juu ya mamlaka ya kufundisha kwake, naye alihesabia nani ustahili wa mamlaka aliyotumia?
15 Bwana Yesu Kristo mwenyewe alifanyiwa ubishi na kukabiliwa na maoni ya watu wake mwenyewe ya kutotaka kukubali alikuwa mhudumu wa Mungu aliyepewa mamlaka. Kwa mfano, tunasoma hivi: “Hata ikawa katikati ya sikukuu [ya mahema] Yesu alikwea kuingia hekaluni, akafundisha. Wayahudi wakastaajabu wakisema, Amepataje huyu kujua elimu, ambaye hakusoma?” Yesu aliuelekea ubishi huo moja kwa moja, akatamka “Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka. Mtu akipenda kuyatenda mapenzi yake, atajua habari ya yale mafunzo, kwamba yatoka kwa Mungu, au kwamba mimi nanena kwa nafsi yangu tu. Yeye anenaye kwa nafsi yake tu hutafuta utukufu wake mwenyewe; bali yeye anayetafuta utukufu wake aliyempeleka, huyo ni wa kweli, wala ndani yake hamna udhalimu.”—Yohana 7:14-18.
16. Kwa sababu gani viongozi wa dini ya Kiyahudi walijisikia kwamba walikuwa na sababu za kutilia shaka uwezo wa Yesu wa kufundisha?
16 Viongozi wa dini ya Kiyahudi walimwona Yesu kuwa kabwela tu wa Galilaya. Bila shaka, sababu yao ya kufikiri hangeweza kusoma haikuwa kwamba yeye hakuwa amehudhuria shule, hasa kitu kama chuo cha mafunzo ya ualimu wa kidini. Yesu alikuwa tayari ameonyesha kwamba angeweza kusoma maandishi ya Maandiko ya Kiebrania. (Luka 4:16-21) Jambo lililokuwa lisilokubalika kwa Wayahudi hao wa Yudea na Yerusalemu ni kwamba mtu huyo aliyekuwa seremala hapo kwanza hakuwa mwalimu aliyesomea uanadini na hangeweza kupangwa katika cheo kimoja na waandishi, Wafarisayo, na Wasadukayo wa taifa lao. Basi, mbona yeye ajionyeshe mbele ya watu kwamba alijua maana ya Maandiko ya Kiebrania na namna yalivyotumika, akisema kwa mamlaka kama alivyofanya? Jambo hilo ndilo lililofanya Wayahudi hao wawe na uziwi mwingi mno kiroho wasitake kuusikia ukweli wa kimungu. Walikuwa wenye kiburi mno wasikubali mambo waliyoelezwa na mtu ambaye hakuwa amehitimu shule ya ualimu wa kidini.
‘Watafundishwa na Yehova’
17. Kuhusiana na Yesu Kristo, viongozi wa kidini Wayahudi hawakufikiria Mwalimu gani, na Yesu alikuwa mwanachuo wa namna gani?
17 Wayahudi hao wenye hekima ya kilimwengu hawakufikiria Yule aliyekuwa amekuwa akifundisha Yesu Kristo. Kwani, ufundi wa Yesu mwenyewe wa kuwa mwalimu ulikuwa umetoka kwa “yule mwalimu aliye mkubwa zaidi ya wote,” Yehova Mungu! (Ayubu 36:22, Today’s English Version) Akimtaja Mungu kuwa hivyo, Yesu alisema: “Mtakapokuwa mmekwisha kumwinua Mwana wa Adamu, ndipo mtakapofahamu ya kuwa mimi ndiye; na ya kuwa sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Kwa hiyo Yesu alijithibitisha kuwa mwanafunzi aliye mzuri zaidi katika shule ya ulimwengu mzima ya yule Mwalimu bora zaidi aliyeko. Jambo hilo lilimletea sifa Yule aliyemfundisha. Si ajabu kwamba Wanazareti walisema hivi juu ya huyo aliyekuwa mwana-mji wa kwao: “Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii?”—Mathayo 13:54.
18. (a) Inatupasa tutake mwalimu wa namna gani? (b) Yesu alisema nini juu ya Mwalimu mkuu zaidi na juu ya wale wenye kufundishwa na Huyo?
18 Ili kuifahamu Biblia, tunataka na kuhitaji mwalimu bora zaidi awezaye kuwako. Naye mwalimu huyo ndiye ameongoza kwa roho Yake Kitabu hicho kisichoweza kushindwa na kingine. Akisema na wale waliokuwa washiriki wa tengenezo linaloonekana la kidunia la Mwalimu huyo wakati wa maisha yake ya hapa duniani, Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.” (Yohana 6:44, 45) Hapo Yesu alikuwa akitumia maneno ya Isaya 54:13, ambayo yanasema: “Na watoto wako wote watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.”
19. Ni “watoto” wa nani wangefundishwa na Yehova?
19 Lakini, sisi tunauliza: Ni “watoto” wa nani wangekuwa ‘wamefundishwa na Yehova’? “Mwanamke” wa usemi wa mfano, aliyetazamiwa kuwa mama ya “watoto” fulani, ndiye aliyepewa ahadi hiyo ya kiunabii. “Mwanamke” huyo ndiye anayeambiwa maneno ya Isaya 54:1, ambapo panasemwa hivi: “Imba, wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema [Yehova].”
20. Kulingana na 2 Wakorintho 13:5, ni lazima Wakristo walio wakfu waendelee kufanya nini, na jambo hilo lina uhusiano gani na kustahili kwao kuwa wahudumu wa Ufalme?
20 Kwa kuwa Yehova ndiye anayesema na “mwanamke” huyo na ndiye atakayekuwa Mwalimu wa “watoto” wake, ni lazima awe ndiye Mume wake wa usemi wa mfano, na lazima huyo awe ni tengenezo lake la kimbingu lililo mfano wa mwanamke. “Watoto” wake, au wana, ni wanafunzi wa “yule mwalimu aliye mkubwa zaidi ya wote.” Bila shaka, inahitajiwa kabisa kwamba “watoto” hao, wafuasi wa Yesu waliopakwa mafuta, na wenzi wao, ule “mkutano mkubwa,” waendelee kutumia mafundisho wanayopewa na Yehova. (Ufunuo 7:9) Kwa uhakika hiyo ni njia moja ya kutii onyo hili la upole la Paulo: “Endeleeni kujijaribu kama mu katika imani, endeleeni kujithibitisha wenyewe mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5, NW) Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa wakiendelea kufanya hivyo na kubaki wakiwa wanafunzi wenye bidii wa yule Mwalimu aliye mkubwa zaidi ya wote, wanapaswa kuwa na ustahili unaohitajiwa kama wahudumu wa Ufalme waliopewa mamlaka na Yehova. Sasa tutaona namna wahudumu wa Mungu wanavyothibitisha kustahili kwao.
Wewe Ungesema Nini?
◻ Unaweza kuthibitishaje kwamba leo Yehova ana wahudumu duniani?
◻ Ni nini kilichofananishwa na Yerusalemu ‘uliokanyagwa na mataifa’?
◻ Kwa sababu mataifa yameupuuza Ufalme, Yesu amelazimika kufanya nini?
◻ Kwa sababu gani si ajabu kwamba uhudumu wa Mashahidi wa Yehova unafanyiwa ubishi?
◻ Ni jambo gani ambalo halikufikiriwa na viongozi wa kidini Wayahudi ambao walibisha juu ya uwezo wa Yesu wa kufundisha?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kama vile Yehova alivyomtumia Danieli kuwatolea onyo wala-karamu wenye makelele kwenye karamu ya Belshaza, ndivyo Yeye amekuwa na wahudumu wa kupelekea watu ujumbe wa haraka leo
[Picha katika ukurasa wa 13]
Viongozi wa kidini walikuwa wenye kiburi mno wasiweze kumkubali hata Yesu Kristo kuwa mhudumu wa Mungu