Roho ya Huduma ya Kikristo
“Mpashwe moto kwa roho. Mtumikieni Yehova.”—WARUMI 12:11, NW.
1. Mtu anathibitishaje kwamba yeye ni mhudumu?
KUNA njia moja tu ambavyo mtu anaweza kuthibitisha kwamba yeye ni mhudumu Mkristo—kwa matendo yake. Tunaona jambo hilo katika maana yenyewe ya neno la Kigiriki la mhudumu, (minista), di·aʹko·nos. Mwandikaji mmoja anasema hivi: “Di·aʹko·nos ni neno linalomtaja mtumishi akiwa katika utendaji wake wa kazi . . . Neno hilo linataja mtu anayetimiza amri za mwingine, hasa, zile za bwana wake.” (Kitabu Studies in the Vocabulary of the Greek New Testament, cha Kenneth S. Wuest) Hapo mwandikaji anakazia kwamba maana ya kuwa mhudumu ni kuwa hasa mwenye bidii katika kufanya jambo fulani wala si kuwa na cheo fulani tu.
2. Kulikuwako uthibitisho gani kwamba Timotheo na Paulo walikuwa wahudumu wa kweli wa Mungu?
2 Kwa mfano, mtume Paulo alisema hivi juu ya Timotheo: “Lakini mnaujua uthibitisho ambao alitoa juu yake mwenyewe, kwamba kama vile mtoto pamoja na baba yeye alitumikia pamoja nami katika kuzisogeza mbele habari njema.” (Wafilipi 2:22, NW) Timotheo alitia bidii sana katika huduma. Hakuna mtu aliyeona kazi ngumu aliyoifanya bila kujipenda angeweza kutia shaka akisema kwamba hakuwa mhudumu wa kweli wa Mungu. Paulo aliwaandikia Wakristo katika Korintho pia maneno haya: “Ninyi wenyewe ndio barua yetu [ya pendekezo] iliyoandikwa juu ya mioyo yetu na kujulikana na inayosomwa na wanadamu wote. Kwa maana ninyi mnaonyeshwa kuwa barua ya Kristo iliyoandikwa nasi tukiwa wahudumu, iliyoandikwa si kwa wino bali kwa roho ya Mungu mwenye kuishi.” (2 Wakorintho 3:2, 3, NW) Kwa kuona kundi hilo lenye kusitawi na kujua kwamba Mungu alikuwa amelitokeza kupitia kazi ya Paulo ya huduma, ni nani angaliweza kutia shaka akisema kwamba Paulo hakuwa mhudumu wa Mungu?
3. Eleza namna ilivyo roho ya mhudumu wa kweli Mkristo.
3 Hata hivyo, kumbuka kwamba kusudi la kuwa mhudumu si kujionyesha tu. Tunahitaji kukuza roho ya huduma ya Kikristo. Timotheo ‘alitumikia’ (kama mtumwa) akiwa pamoja na Paulo. Mtume mwenyewe alisema hivi: “Ole wangu ikiwa sikuzitangaza habari njema!” (1 Wakorintho 9:16, NW) Tena, aliandika hivi: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili [huduma yetu isilaumiwe]; bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama [wahudumu] wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida.” Ndiyo, Paulo alidhihirisha hali ya kujitoa sana ahudumu, juhudi, uharaka na nia ya kupenda kuvumilia lo lote lililohitajiwa kabisa, hata ‘kupata hasara ya mambo yote’ ili atimize huduma yake akiwa Mkristo. (2 Wakorintho 6:3-10; Wafilipi 3:8) Wahudumu wote wa kweli Wakristo wanapaswa kuwa na roho kama hiyo.—Luka 9:23 24.
4. Mtu anawezaje kuwa mhudumu ikiwa anatumia mwingi wa wakati wake akitimiza wajibu mwingi mwingine?
4 Kama ilivyokuwa siku za mitume, wahudumu wengine leo ni wanaume au wanawake wenye jamaa na kazi ya kimwili. Wengine ni wanafunzi shuleni. Wanawezaje kusema wao ni wahudumu? Ni kweli kwamba wanatimiza wajibu mwingine-mwingine walio nao na hata kufurahia tafrija za kiasi cha kutosha. Lakini mambo hayo mengine siyo ya maana kuliko huduma yao. Wala wao hawajaribu kuitafutia huduma hiyo kinafasi kidogo tu mahali pengo dogo limepatikana katika tafrija zao, wala hawatumii wakati mchache tu kila mwezi ili tu ionekane wanahudumu. Wao ‘wanaendelea kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.’—Mathayo 6:33, NW.
Kupainia na Huduma ya Kikristo
5. Njia nzuri ya kudhihirisha roho ya huduma Kikristo ni nini?
5 Wale wanaodhihirisha roho ya namna hiyo ni wahudumu wa kweli Wakristo, hata ikiwa wana madaraka ya kijamaa au wajibu mbalimbali wa kimwili. Lakini wengine wao wana uwezo wa kuidhihirisha roho ya huduma kwa njia yenye thawabu za pekee. Namna gani? Kwa kupainia (kuingia katika kazi ya kuhubiri wakati wote), ama kwa kipindi kifupi wakiwa mapainia-wasaidizi au kwa muda mrefu zaidi. Huenda hata wakaweza kufanya kazi kwenye moja ya afisi za matawi za Sosaiti au kushiriki katika umisionari au katika huduma ya kusafiri, wakitembelea makundi mbalimbali na kuyajenga.
6. Ni nini nyingine za sababu zinazofaa za kufanya Mashahidi wa Yehova apainie ikiwa yuko katika hali ya kuweza kufanya hivyo? (Luka 6:46-49)
6 Kwa sababu gani wengi wa Mashahidi wa Yehova wanapainia na hali wangeweza kuishi maisha ya kujistarehesha zaidi wakitumia muda mchache zaidi katika kumtumikia Mungu? Ni kwa sababu wanataka kumsifu Yehova na kueleza wengine makusudi yake. Pia, wanajua kwamba “ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17, NW) Kwa Sababu ya kuliamini kwa moyo mnyofu jambo hilo pamoja na ahadi za Mungu, wanahangaikia kutumia wakati mwingi inavyowezekana wakiambia wengine habari njema, ili wale wanaoitikia waweze pia kufanya mapenzi ya Mungu na kupata uzima wa milele. Kuongezea hilo, wanajua kwamba tunaishi katika wakati ambao “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Wanakumbuka kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Wanajua kwamba leo sala hiyo inafaa kusemwa zaidi ya siku za Yesu. Lakini wanawezaje kuitoa sala hiyo kwa unyofu wa moyo ikiwa wao wenyewe wanasita-sita kuwa na ushiriki mwingi iwezekanavyo katika huduma ya Kikristo?
7. Ni ulizo gani ambalo kila mhudumu Mkristo anapaswa kujiuliza?
7 Kusema kweli, inampasa kila mhudumu Mkristo afikirie kwa kusali kama anaweza au hawezi kupainia. Mume na mke wa Afrika ya Kusini ambao wamepainia muda wa miaka kumi na mitano walisema: “Kwa sababu gani tunapainia? Tungeweza kweli kupata sababu nzuri ya kujitetea mbele za Yehova kama hatungepainia?” Ingefaa wengi ambao si mapainia wajiulize ulizo hili linalohusiana na hilo jingine: ‘Je! mimi naweza kweli kupata sababu nzuri ya kujitetea mbele za Yehova juu ya kinachofanya nisiwe painia?’
Kutumia Karama Zetu
8. Kama Timotheo, ni kwa njia gani vijana wengi huenda wakawa katika hali ya kuweza kupainia?
8 Timotheo alikuwa na karama (kipawa) ya pekee ya kiroho aliyoweza kuitumia kwa matokeo mazuri katika huduma yake. (2 Timotheo 1:6) Leo sisi hatukupokea karama za pekee za roho, lakini tuna karama nyingine, na mara nyingi karama hizo zinafungulia watu njia ya kupainia. Kwa mfano, vijana wanaohitimu masomo wana karama. Wana elimu. Pia, kama vile Timotheo, wao wana ujana. Wana afya na nguvu, na vilevile maoni ya uchangamfu na ya kusema mambo wazi. Tena wana wakati, na labda hiyo ndiyo karama kubwa kupita zote. Tukisema kwa ujumla, wao hawalemewi na madaraka mengi. Kwa hiyo ujana ni wakati bora kabisa wa kufikiria kupainia.—Mhubiri 12:1.
9. Ni karama (vipawa) gani ambazo huenda watu wa umri mkubwa na wengine wakawa nazo ambazo zingewawezesha kupainia?
9 Watu wenye umri mkubwa wana karama pia. Mume na mke walio na watoto walio watu wazima na ambao wamestaafu kazi huenda hata wao wakaweza kuwa na wakati wa kutumiwa katika kupainia. Mara nyingi watu wa namna hiyo wanakuwa na mapato thabiti yasiyopungua-pungua, tena wanakuwa wamejipatia ujuzi wenye thamani kubwa maishani na kujenga kumbukumbu refu la utumishi mwaminifu. (Mithali 16:31) Mambo yote hayo yangeweza kutumiwa vizuri katika kupainia. Huenda wengine wakawa na karama pia. Wake wengine wenye kufanya kazi za kinyumbani wana karama (kipawa) ya usimamizi mzuri wa mambo, kwa hiyo wanaweza kutimiza madaraka yao ya kijamaa na kupainia. Wanaume fulani wenye jamaa walio na karama kama hiyo wanaweza kupainia na vilevile watafutie jamaa zao riziki ya kiroho na kimwili pia. Je! wewe una karama ya usemaji, ya kufundisha, ya kuvuta watu katika maongezi ya kawaida? Ebu fikiria karama za namna hiyo zingepanuaje utumishi wa painia.
10. (a) Kwa sababu gani wengine wanasita-sita kupainia, lakini kijana mwanamume na mwanamke walitatuaje tatizo hilo? (b) Ni kwa njia gani utumishi wa painia huenda ukafaidi mtu anayeona ni vigumu kuhubiri?
10 Wengine wamesita-sita wasipainie, wakishangaa-shangaa kama wataweza kuwa na pesa za kujiendesha. Mwanamume na mwanamke waliochumbiana wakitazamia ndoa walizungumza hofu hiyo pamoja. “Tukaamua kwamba ukosefu wa kuutumaini uwezo wa Yehova wa kutupatia mahitaji yetu ndio uliofanya tuwe na woga huo.” Hivyo ndivyo walivyokata maneno. “Baada ya kurudia kuangalia Mathayo 6:25-33, ambapo Yesu alifundisha kwamba tukiutafuta kwanza ufalme mahitaji yote yatatimizwa, tulijiwekea mradi wa kuwa mapainia wa kawaida.” Muda mfupi baada ya hapo walioana, kila mmoja wao akaacha kazi yenye mshahara mnono kisha wakawa mapainia. Wengine wanaiona kazi yenyewe ya kuhubiri kuwa ngumu. Je! ndivyo wewe unavyoiona? Ikiwa ndivyo, kupainia kunaweza kusaidia, Kwa kweli, njia iliyo bora zaidi ya kustarehe bila woga katika huduma ya nyumba kwa nyumba ni kutumia wakati fulani ukipainia. Mhudumu mmoja aliyeshiriki katika upainia-msaidizi alisema hivi; “Kulikuwa na baraka nyingine. Mimi nilizidi kupungukiwa na wasiwasi katika kazi yangu ya nyumba kwa nyumba. Badala ya kutetema kwenye kila mlango, nilianza kutazamia kwa hamu niongee na watu.”—Angalia Wafilipi 4:13.
Kupainia Ni Jambo la Kijamaa
11. Timotheo alibarikiwaje katika mazoezi aliyopokea “tangu utoto mchanga”?
11 Timotheo alikuwa ametayarishwa kwa ajili ya huduma hatua kwa hatua “tangu utoto mchanga.” (2 Timotheo 3:14, 15, NW) Ni wazi kwamba mama yake na nyanya (bibi) yake walikuwa na roho ya huduma ya Kikristo na waliikaza sana ndani yake. Wakati Paulo alipofika Listra, Timotheo hakuwa na lo lote la kumzuia, bali alikuwa tayari kujiunga naye katika utendaji wa kuhubiri wakati wote.—Matendo 16:1-5.
12. Wazazi wengi wameonyeshaje kwamba wana roho ya huduma ya Kikristo?
12 Leo Wakristo wengi wanafurahi kwamba wazazi wao wameonyesha roho kama hiyo. Alice, mhudumu Mghana, alisema hivi: “Karibu Mashahidi wote waliokuja kukaa nyumbani kwetu walikuwa wahubiri wa wakati wote. . . . Nilikuwa na pendeleo kubwa la kulelewa katika jamaa hiyo ya kitheokrasi, we! Baba alikazia ndani ya watoto wake wote tamaa ya kazi ya kuhubiri wakati wote, akiwataja ndugu na dada wenye kufanya kazi hiyo kama mfano ya jambo hilo. Basi ilikuwa vyepesi baada ya shule nikajiandikisha moja kwa moja niwe painia wa kawaida.” Edi mhudumu kijana katika United States (Amerika), alisema hivi: “Mimi nafikiri kilichonisaidia sana ni kwamba wazazi wangu wote wawili walikuwa wamisionari katika Amerika ya Kusini kwa miaka kumi na miwili na walikuwa wamekuwa mapainia kabla ya hapo. Kwa hiyo sikuzote walinionyesha furaha na mapendeleo ya kupainia, na baraka ambazo Yehova anamiminia mapainia. . . . Hilo ni jambo ambalo wazazi wote wanapaswa kufanya kwa sababu lilinisaidia mimi kwa uhakika. Wanaweza kuwatia moyo watoto wao wamtumikie Yehova kwa nafsi yote na kwa Kadiri inayowezekana.”
13. Mapainia wanasaidiwaje washinde magumu?
13 Huenda kupainia kukahitaji mtu ajinyime mambo fulani, lakini wahudumu wa kweli wana nia ya kupenda kujinyima hivyo kwa sababu ya upendo wao kwa Yehova. Zaidi ya hilo, thawabu ni kubwa. Michael na Teresa, ambao ni watu waliooana wa United States, walitoa maoni haya: “Ikiwa unataka kuwa na nguvu nyingi zaidi za kiroho, hapo ndipo unapopaswa kuwa—-katika upainia. Ukiwa hivyo unamtegemea Yehova zaidi na kuzidi kuacha kujitegemea mwenyewe. Ingawa sisi tumekuwa na matatizo ya kipesa tulipokuwa tukipainia, sikuzote Yehova ametutimizia mahitaji yetu. Hapo ndipo mahali salama zaidi ambapo mtu anaweza kuwa.”
14, 15. (a) Nyakati nyingine huenda hata wazazi wa mapainia wakajinyima mambo kwa njia gani? (b) Tuna mifano gani ya nyakati za Biblia ya kutuongoza katika jambo hili? (c) Wazazi wanaweza kuonyeshaje roho ya huduma ya Kikristo leo?
14 Huenda hata wazazi wa mapainia wakajinyima mambo fulani. Huenda wakatatizwa kwa kuwaona watoto wao wakiondoka nyumbani wakapainie wakiwa mahali pengine, labda hata katika nchi ya ugeni. Kwa njia fulani-fulani wazazi hao ni kama Hana na Elkana, ambao walipeleka mzaliwa wa kwanza wao, Samweli, akatumikie Yehova kwenye hema takatifu katika Shilo. (1 Samweli 1:1-3). Au tungeweza kuwalinganisha na Yeftha, ambaye alimtoa binti yake wa pekee awe katika utumishi wa Yehova, na kwa njia hiyo akajinyima taraja lo lote la kuona akiwa na wajukuu baadaye. (Waamuzi 11:36-40) Kwa uhakika Yehova anakumbuka na kuthawabisha ukosefu wa uchoyo wa wazazi hao.
15 Huenda hata kujinyima pesa kukahusika. Katika nchi fulani wazazi wanategemea watoto wao wawatunze wakiwa katika uzee wao. Walakini, wazazi walio kweli kweli na roho ya huduma ya Kikristo hawasiti-siti kuwatia watoto wao wapainie kwa sababu ya jambo hilo. Wakati kijana mwanamume Mghana anayeitwa Justice alipotaka kupainia, mama yake alimpa idhini ya kufanya hivyo na akakubali kumtegemea Yehova amsaidie kupata riziki. Baadaye, mama huyo alimwambia mwanaye kwamba Yehova alikuwa amemruzuku ajabu tangu alipofanya uamuzi huo. Hiyo, pia, ni njia ya ‘kutafuta kwanza ufalme wa Mungu,’ na Yehova hawaachi wale wanaofanya hivyo.—Mathayo 6:33, 34, NW.
16. Kwa sababu gani wale walio katika utumishi wa wakati wote wanapaswa kutiwa moyo waendelee nao maadamu hali zinawaruhusu?
16 Inasikitisha mara kwa mara kupata habari za wazazi wanaojaribu kusadikisha watoto wao waache kupainia—si kwa sababu wanahitaji msaada wao, bali kwa sababu maoni yao ni kwamba watoto wao wamekuwa katika migawo yao muda wa kutosha, na sasa wakati umefika wa kurudi nyumbani, wawe na jamaa na kuishi maisha ‘ya kikawaida.’ Lakini hizi si nyakati za kikawaida, na wakati mwisho wa mfumo huu ukaribiapo zaidi, maisha ya kila mtu yatazidi kupungukiwa na hali ile ya kikawaida. Mapainia, washiriki wa jamaa za Betheli, wahudumu wanaosafiri na wamisionari wanapaswa kutiwa moyo wavumilie katika kazi yao.—Tito 2:12.
Kuidhihirisha Roho ya Huduma
17. (a) Kazi ya mapainia na watumishi wengine wa wakati wote inayasaidiaje makundi? (b) Wote wanaweza kuonyeshaje kwamba wana roho ya huduma ya Kikristo? (Waebrania 13:15, 16)
17 Mtume Paulo aliandika hivi: “[Mungu] aliwapa wengine kama mitume, wengine kama manabii, wengine kama waeneza evanjeli, wengine kama wachungaji na waalimu, kwa kusudi la kurekebisha upya watakatifu, kwa kazi ya huduma, kwa kujengwa kwa mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:11, 12, NW) Leo, kuna wahudumu wanaosafiri, mapainia na wamisionari wanaotumia mwingi wa wakati wao ‘wakieneza evanjeli,’ na vilevile washiriki wa jamaa za Betheli ambao kazi yao ya huduma inatia ndani kutumikia makundi katika njia nyingine. Hao wanasaidia kuyajenga makundi. (Linganisha Matendo 16:4, 5.) Kwa hiyo, wahudumu wote Wakristo wanapaswa kupendezwa na utumishi wa wakati wote. Ikiwa wako katika hali ya kuweza kuwa mapainia inawapasa wafanye hivyo. Ikiwa wao wenyewe hawawezi kupainia inawapasa wawatie moyo wale wanaoweza.—Warumi 12:11.
18. Kwa sababu gani huduma ya Kikristo inahitajiwa sana leo?
18 Kuna uhitaji mkubwa wa kupata mashahidi walio wakf wa Yehova wenye roho kama hiyo. Maelfu ya watu wangali wanaitikia kazi ya kuhubiri habari njema, hata katika maeneo ambayo yamepewa ushuhuda mara nyingi muda wa miaka yote iliyopita. Jambo la kwamba mhudumu Mkristo alitafuta wakati wa kuwatembelea na kuwaambia habari za makusudi ya Mungu liliwafungulia watu hao wenye kuitikia nafasi ya kupata uzima wa milele. (Warumi 10:13,14; 1 Timotheo 4:16) Kama tunaweza au hatuwezi kushiriki katika utumishi wa painia, acheni tuwe na hisi ya kwamba uharaka unatajiwa na roho ya kujinyima. Na tuwe na nia ya kupenda kutia bidii katika huduma ya Kikristo.—Wagalatia 6:10.—Kutoka The Watchtower, November 15 1982.
Je! wewe unafahamu kiukamili
□ Maana ya kuwa na roho ya huduma ya Kikristo?
□ Maana ya huduma ya kufanya saa chache tu, na ubaya wa huduma hiyo?
□ Kwa sababu gani wahudumu wote Wakristo wanapaswa kupendezwa na kupainia?
□ Namna Mashahidi wote waliojiweka wakf wanavyoweza kuonyesha roho ya painia?
□ Kwa sababu gani huduma ya Kikristo inahitajiwa sana leo?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Wahudumu wote wa kweli Wakristo wana roho ya Paulo na Timotheo