Je, Waweza Kutumikia Mahali Palipo na Uhitaji Mkubwa Zaidi?
1 Je, umepata kufikiria kuhamia mahali palipo na uhitaji wa wahubiri zaidi wa Ufalme? Ukialikwa ‘uvuke uingie . . . usaidie,’ je, ungeitikia kama mtume Paulo? (Mdo. 16:9, 10) Katika makutaniko mengi, kuna uhitaji wa familia zilizokomaa, mapainia wa kusaidia kuhubiri eneo fulani, au wazee na watumishi wa huduma wanaostahili ili wasaidie kusimamia mambo. Huenda eneo hilo likawa na miji midogo-midogo na soko zilizotapakaa kotekote katika sehemu kubwa za mashambani. Huenda Jumba la Ufalme likawa mbali sana. Huenda kusiwe na kazi za kimwili za kutosha. Huenda hali ya hewa isipendeze sikuzote. Je, utakuwa tayari kwa magumu hayo? Unawezaje kufanikiwa?
2 Imani na Tumaini Zahitajiwa: Abramu alipoelekezwa na Mungu, aliacha mji wa nyumbani kwao wa Uru na kusafiri kilometa 1,000 kwenda Harani pamoja na mke wake, mpwa wake, na baba yake mzee, Tera. (Mwa. 11:31, 32; Neh. 9:7) Baada ya Tera kufa, Yehova alimwamuru Abramu, ambaye sasa alikuwa na umri wa miaka 75, aondoke Harani na kuacha watu wake wa ukoo, asafiri hadi kwenye nchi ambayo Mungu angemwonyesha. Abramu, Sarai, na Lutu “wakatoka ili kwenda.” (Mwa. 12:1, 4, 5) Bila shaka, Abramu hakuhama ili kutumikia mahali palipokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa wahudumu. Lakini kuhama kwake kulihitaji jambo fulani. Jambo gani?
3 Abramu alihitaji kuwa na imani na tumaini ili achukue hatua hiyo. Alihitaji kubadili kufikiri kwake na njia yake ya maisha. Ilimbidi aache usalama wa watu wake wa ukoo. Lakini alimtumaini Yehova amtunze na aitunze familia yake. Leo, wengi wamemtumaini Yehova kwa njia hiyohiyo.
4 Migao ya Muda Mfupi: Je, umepata kufurahia baraka nyingi zinazotokana na kuhubiri eneo lisilogawiwa mtu? Mwaka uliopita, makutaniko mengi yaligawiwa kwenda kwenye maeneo yasiyohubiriwa kwa ukawaida. Iliwabidi wengine wasafiri mbali. Je, jitihada zao zilikuwa na matokeo yoyote?
5 Naam, bila shaka. Baadhi ya wahubiri wasiotenda walipatikana katika baadhi ya maeneo hayo na kuchochewa upya. Vikundi kadhaa vilianzishwa katika sehemu nyingine na vinaelekea kuwa makutaniko. Mwaka jana, akina ndugu wengi walipata shangwe na kitia-moyo kwa kuhubiri maeneo hayo yasiyogawiwa mtu au yasiyohubiriwa kwa ukawaida.—Zab. 100:2.
6 Kukubali mgao wa kutumikia kwa muda mfupi mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi kwaweza kutimiza kusudi jingine. Wale wanaofanya hivyo wanaweza kupata habari za maana zitakazowasaidia “kupiga hesabu ya gharama” ya kuhamia eneo lingine nchini.—Luka 14:28.
7 Yehova anataka habari njema zitangazwe “katika dunia yote inayokaliwa” kabla ule mwisho haujafika. (Mt. 24:14) Ukijua hivyo, je, utakuwa tayari kuhamia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi ukiweza? Kuna uhitaji katika sehemu nyingi.
8 Kuhamia Mahali Palipo na Uhitaji Mkubwa Zaidi: Je, umestaafu? Je, una fedha za kutosha? Ikiwa sivyo, je, waweza kupanga uwe na kazi yako mwenyewe? Ikiwa huwezi kuhama, je, waweza kusaidia mshirika mmoja wa familia atumikie mahali pengine? Ikiwa waishi jijini, je, kule nyumbani kwenu kuna kutaniko lililo karibu? Je, waweza kupanga uhubiri huko unapokuwa likizoni, labda pamoja na mhubiri mwingine? Hivyo ndivyo makutaniko mengi katika maeneo yasiyogawiwa mtu yalivyoanzishwa.
9 Ikiwa baada ya kutoa sala na kufikiria kwa uzito unaona kwamba waweza kukubali mwito huo wa ushindani wa kuhamia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi, zungumzia jambo hilo pamoja na familia yako na wazee wa kutaniko lenu. Kisha, andika barua na uwape wazee ili watie ndani maoni yao na mapendekezo yao kabla ya kuituma kwenye ofisi ya tawi.
10 Utaandika nini katika barua yako? Umri wako, tarehe ya ubatizo, madaraka katika kutaniko, iwapo umeoa au la, na kama una watoto wadogo. Taja mahali unapotaka kutumikia, patakapofaana na afya yako. Kwa mfano, je, waweza kuishi mahali penye joto? Waweza kuvumilia mahali penye baridi? Je, waweza kuishi milimani? Je, wewe huzungumza lugha nyingine?
11 Je, una bidii na nia? Hali zako zakuruhusu utumikie mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi? Ikiwa zakuruhusu, basi jionee jinsi ambavyo Yehova huendelea kubariki sana wale wanaomtumaini wanapoonyesha roho ya kujitolea!—Zab. 34:8; Mal. 3:10.