Je, Ni Kizuizi cha Kuhubiri?
1 Watu wengi huishi maisha yenye shughuli nyingi. Mashahidi wa Yehova ni miongoni mwa watu wenye shughuli nyingi zaidi—hujifunza Neno la Mungu, huhudhuria mikutano, na kwenda katika utumishi wa shambani. Kwa kuongezea, sisi tunashughulika na kazi ya kimwili, ya nyumbani au shuleni, na madaraka mengine mbalimbali ambayo huchukua wakati mwingi. Vichwa vya familia ndio hasa hukabili ugumu huo.
2 Kwa sababu ya hali ngumu za kiuchumi katika sehemu mbalimbali, huenda vichwa vya familia wakalazimika kufanya kazi kwa bidii na kwa muda wa saa nyingi ili kutafuta riziki. Wanapotumia nguvu zao nyingi na wakati mwingi kufanya kazi za kimwili, wao hubaki na muda mfupi tu wa kuhubiri. Kwa kuwa wana wajibu wa kuruzuku familia zao, huenda wengine wakahisi kwamba wanaweza kutumia wakati mchache tu katika huduma. (1 Tim. 5:8) Bila shaka, leo kuna mikazo mingi inayohusiana na kujipatia riziki. Lakini kazi ya kimwili haipaswi kumzuia mtu kuhubiri habari njema. (Mr. 13:10) Kwa hiyo, twapaswa kuchunguza hali yetu wenyewe.
3 Kwa kuwa hali ya ulimwengu inabadilika sikuzote, huenda kichwa cha familia akaelekea kutumia wakati mwingi zaidi kufanya kazi yake, akiwa na lengo la kuweka akiba ya fedha za majanga yasiyotazamiwa. (1 Kor. 7:31) Ingawa huenda kazi nyingi ya kimwili ikawawezesha kupata vitu vingi vya kimwili au fedha za ziada za tafrija na vitumbuizo, je, hiyo itafanya familia iwe na furaha na uradhi zaidi kama mambo ya kiroho na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kunapuuzwa? Kwa kweli twapaswa kuepuka chochote ambacho kitahatarisha hali yetu ya kiroho. Kutii shauri la Yesu la ‘kuweka akiba ya hazina mbinguni’ na kuwa “tajiri kuelekea Mungu” ndilo jambo la hekima.—Mt. 6:19-21; Luka 12:15-21.
4 Tafuta Masilahi ya Ufalme Kwanza: Yesu alifundisha wafuasi wake kutanguliza mambo ya kiroho zaidi ya mambo mengine yote. Aliwasihi hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tule nini?’ au, ‘Tunywe nini?’ au, ‘Tuvae nini?’” Kwa nini alisema hivyo? Alieleza hivi: “Kwa maana Baba yenu wa kimbingu ajua mwahitaji vitu hivi vyote.” Ikiwa kwa kweli twaamini maneno hayo, hakutakuwa na kitu kitakachotuzuia kufanya yale ambayo Yesu aliendelea kusema: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi [vya kimwili vilivyo vya lazima] mtaongezewa.” Mungu atahakikisha kwamba tunapata vitu ambavyo ni vya lazima! (Mt. 6:31-33) Kwa kweli huu si wakati wa kukengeushwa na mahangaiko yasiyo ya lazima kwa sababu ya kazi au tamaa ya kuishi maisha yenye starehe katika mfumo wa mambo ambao utapitilia mbali hivi karibuni.—1 Pet. 5:7; 1 Yoh. 2:15-17.
5 Kusudi kuu la kazi ya kimwili ni kujiandalia mahitaji ya kimwili. Lakini mahitaji yetu ni mengi kadiri gani? Mtume Paulo aliandika: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” Je, twajaribu kujitafutia mengi zaidi ya hayo? Ikiwa ni hivyo, huenda ikawa tunavuna matokeo ambayo Paulo alionya juu yake hivi: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.” (1 Tim. 6:8, 9; Mt. 6:24; Luka 14:33) Twaweza kujuaje kama tunazuiwa na tamaa nyingi mno?
6 Ikiwa kwa sababu ya kazi zetu za kimwili hatupati wakati wa kutosha kwenda katika utumishi wa shambani au hatuoni uhitaji wa kujinyima mambo fulani kwa ajili ya habari njema, basi twahitaji kurekebisha mambo tunayotanguliza. (Ebr. 13:15, 16) Maisha ya kiasi yatasaidia kuondoa mambo yanayotuzuia kuhubiri. Twapaswa kutanguliza masilahi ya Ufalme tunapotumia wakati wetu na nishati zetu.
7 Kazi Isiyo Bure: Maneno ya Paulo yanatutia moyo sikuzote tuwe na ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, tukijua kwamba kazi yetu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.’ (1 Kor. 15:58) “Kazi ya Bwana” iliyo kuu ni kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Ili tuhubiri kikamili iwezekanavyo, twapaswa kupanga wakati wa kwenda katika utumishi wa shambani kila juma na kujitahidi kutotumia wakati huo kwa mambo mengine. (Efe. 5:15-17) Tukifanya hivyo, kazi ya kimwili au jambo jingine lolote halitazuia huduma yetu.
8 Tunapojitoa wenyewe kufundisha wengine kweli za Biblia, twapata furaha nyingi inayotokana na kutoa. (Mdo. 20:35) Kwa kuendelea kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme, twaweza kutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika, “kwa maana Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi [yetu] na upendo [tu]lioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Ebr. 6:10.