Mazoea Yako ya Kujilisha Kiroho Ni Yenye Kuridhisha Kadiri Gani?
1 Imesemwa kwamba ‘sisi huathiriwa na kile tunachojilisha.’ Kwa kweli nguvu zetu za kimwili na afya yetu huathiriwa na mazoea yetu ya kula. Kwa kuwa Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova,” mazoea yetu ya kujilisha kiroho pia hutuathiri vizuri au vibaya. (Mt. 4:4) Kwa hiyo basi, mazoea yako ya kujilisha kiroho ni yenye kuridhisha kadiri gani? Je, wewe ni mlaji mwenye kuchagua? Je, wewe hula haraka-haraka? Je, wewe hufurahia kutumia wakati kujilisha kwa ukawaida vyakula vya kiroho?
2 Chunguza Mlo Wako: Yehova huandaa ‘chakula kwa wakati ufaao’ na “karamu ya vitu vinono,” kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; Isa. 25:6) Ili kunufaika kabisa kutokana na maandalizi hayo yenye upendo, lazima tujitahidi sana kula vizuri kiroho.
3 Huenda ukajiuliza: ‘Je, mimi husoma andiko la siku na maelezo yake kila siku? Je, mimi husoma Biblia na kuitafakari kila siku? Je, mimi hutayarisha mikutano ya kutaniko kwa kujifunza mapema habari itakayozungumziwa? Je, nimesoma vichapo vyetu vya karibuni, kutia ndani mabuku yote mawili ya Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote?’
4 Yesu aliahidi: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho . . . Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa wao watashibishwa.” (Mt. 5:3, 6) Kwa hiyo, jilishe vizuri kiroho kwa kujaza akili yako na moyo wako ujuzi kuhusu Mungu.