Sanduku La Swali
◼ Twapaswa kukumbuka nini tutumiapo simu za mkononi na peja?
Vifaa hivyo vyaweza kutusaidia kuwasiliana na wengine mahali popote pale tulipo. Ingawa ni vyenye msaada, lazima tuwe waangalifu tusiruhusu matumizi ya simu za mkononi na peja nyakati zisizofaa kama vile kutukengeusha na huduma au mikutano yetu ya Kikristo. Hilo lawezekanaje?
Fikiria jinsi ambavyo ingekuwa kama simu yetu ya mkononi au peja ingelia tukiwa katika huduma ya shambani tukihubiri. Mwenye nyumba atafikiria nini? Wenye nyumba wangefikiria nini kama ingetubidi tuache kuzungumza ili tujibu simu hiyo? Kwa kweli hatungependa kufanya chochote ambacho kingezuia wengine kusikiliza ujumbe wa Ufalme. (2 Kor 6:3) Kwa hiyo, ikiwa tunabeba simu ya mkononi au peja, tunapaswa kuirekebisha katika njia ambayo haitatukengeusha sisi au wengine tunapoendelea kuhubiri.
Vipi ikiwa tunangojea huku wengine wakihubiri? Ikiwa tumetenga wakati wa utumishi wa shambani, kwa nini tusikazie fikira utumishi huo? Kwa sababu ya kuheshimu utumishi wetu mtakatifu, tafadhali shughulikia mambo ya kibinafsi au shughuli nyinginezo wakati mwingine. (Rom. 12:7) Bila shaka, hiyo haimaanishi kwamba hatutatumia simu kuhubiri au kupanga ili kutoa ushahidi.
Lazima tuwe waangalifu zaidi kuhusu kutumia simu tunapoendesha gari, kwa kuwa uchunguzi kadhaa waonyesha kwamba kufanya hivyo huzidisha hatari ya kupata aksidenti. Tunapaswa kutii sheria zozote zinazokataza kutumia simu ya mkononi tunapoendesha gari.
Tunaenda kwenye mikutano ya Kikristo, makusanyiko, ili kumwabudu Yehova na kufundishwa naye. Je, uthamini wetu kwa mambo matakatifu haupaswi kutufanya turekebishe simu za mkononi na peja ili tusikengeushwe fikira au kukengeusha wengine? Ikiwa twahitaji kushughulikia jambo la dharura, twapaswa kufanya hivyo nje ya mahali pa kukutanikia. La sivyo, tupange kushughulikia mambo ya kibinafsi na mambo yasiyohusisha ibada yetu wakati usiokuwa wa ibada.—1 Kor. 10:24.
Njia ambayo tunatumia simu za mkononi au kifaa chochote kile na ionyeshe kwamba sikuzote twawajali wengine na kuthamini sana mambo ya kiroho.