Sanduku La Swali
◼ Ni kanuni gani za Biblia tunazoweza kutumia ambazo zinahusu matumizi ya simu za mkononi wakati wa mikutano na tunaposhiriki katika huduma?
“Kuna Wakati Uliowekwa wa Kila Kitu.” (Mhu. 3:1): Simu za mkononi huwawezesha watu kutuma ujumbe mfupi au kuongea na wengine karibu kila wakati. Hata hivyo, kuna nyakati ambazo Wakristo wasingependa kukengeushwa na simu zao. Kwa mfano, mikutano yetu ni wakati wa kumwabudu Yehova, kupokea maagizo ya kiroho, na kufurahia ubadilishanaji wa kitia moyo. (Kum. 31:12; Zab. 22:22; Rom. 1:11, 12) Je, haingekuwa vizuri kuzima simu zetu na kusoma jumbe tulizotumiwa baada ya kutoka mkutanoni? Ikiwa tutalazimika kutozima simu zetu kwa sababu huenda tukapigiwa simu ya dharura, tunapaswa kuziweka katika njia ambayo haitawasumbua wengine.
‘Fanya Mambo Yote kwa Ajili ya Habari Njema.’ (1 Kor. 9:23): Nyakati nyingine, kuna sababu za msingi za kutumia simu katika huduma. Kwa mfano, ndugu anayeongoza anaweza kutumia simu ili kujua hali ya wale wanaohubiri katika eneo. Wakati mwingine wahubiri hutumia simu zao za mkononi kuwapigia watu wanaopendezwa au wanafunzi wa Biblia kabla ya kuwatembelea, hasa ikiwa wanaishi mbali. Ikiwa tumebeba simu wakati wa utumishi, tunapaswa kuwa waangalifu ili zisitukengeushe tunapozungumza na mwenye nyumba. (2 Kor. 6:3) Tunapowangojea wahubiri wengine, badala ya kupiga simu au kutuma ujumbe kwa rafiki, je, haingekuwa vizuri kukazia fikira huduma na wale tunaohubiri nao?
Wafikirie Wengine. (1 Kor. 10:24; Flp. 2:4): Tusingependa kamwe kuwa wazembe kwa kuchelewa kufika kwenye mikutano ya utumishi wa shambani, tukifikiria kwamba sikuzote tunaweza kupiga simu au kumtumia ujumbe mtu fulani ili kujua kikundi kinahubiri wapi. Tunapochelewa, mara nyingi kikundi hupangwa upya. Ni kweli kwamba, pindi fulani hali zisizozuilika zinaweza kusababisha tuchelewe. Hata hivyo, tunapokuwa na kawaida ya kufika kwa wakati, tunaonyesha kuwa tunaheshimu mpango wa Yehova, ndugu anayeongoza na wahubiri wenzetu.